Habari za Punde

Hutuba ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Serekali Siku ya Uzinduzi wa Jengo lao Jipya Maisara.



HOTUBA YA MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI ZANZIBAR KATIKA UFUNGUZI WA JENGO JIPYA LA AFISI YA MAISARA - TAREHE 13 SEPTEMBA 2012
 
 Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Dk. Ali Mohd Shein,
Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais,
Balozi Seif Ali Iddi,
Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
Utumishi wa Umma na Utawala Bora
Waheshimiwa Mawaziri,
Viongozi Mbali Mbali wa Serikali,
Wageni waalikwa ,
Mabibi na Mabwana.
ASSALAM ALAYKUM.
Kwanza kabisa, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kutupa afya njema na kutuwezesha kufika hapa kwa mara nyengine tena kushiriki katika hafla hii ya ufunguzi wa jengo jengine jipya la Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa ujasiri na uwezo wa kusimamia ujenzi wa jengo letu hili hadi kukamilika kwake.
Pili napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwako Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohd Shein, kwa kukubali mualiko wetu wa kuwa mgeni rasmi katika shughuli hii ya ufunguzi wa jengo hili jipya la Afisi yetu, Aidha kwa wingi wa heshima natoa shukrani zangu kwako binafsi kwa juhudi zako unazochukua kwa kuiunga mkono Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku kama ulivyowaahidi Wananchi wa Zanzibar katika Mikutano na hotuba zako mbali mbali.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Tunafahamu kuwa unakabiliwa na shughuli nyingi za kitaifa  lakini kutokana na umuhimu na uzito wa jambo hili umeamua kuugawa muda wako adhimu na  kuja kuungana nasi katika ufunguzi wa jengo la Ofisi yetu, ushiriki wako ni kielelezo tosha cha kuthamini mchango wa Afisi yetu katika maendeleo ya Taifa letu.
Aidha kwa dhati kabisa nampongeza waziri wa nchi Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora,  kutokana na mchango wake mkubwa na ukaribu katika kuhakikisha kwamba  Ofisi yetu inapiga hatua za kimaendeleo siku hadi siku.
Pia nachukua nafasi hii, kuwashukuru viongozi mbali mbali wa Serikali pamoja na waalikwa wote kwa ujumla, kwa kuitikia wito wetu na kuweza kufika katika sherehe yetu bila kukosa. Nasema ahsanteni na karibuni sana.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, imemaliza utekelezaji wa Mpango Mkakati wake wa miaka mitatu ulioanza mwaka 2007 hadi 2011.  Utayarishaji wa mpango mkakati huo ulikuwa na lengo la kuweka mfumo mzuri wa kazi na kupata dira ya kutekeleza majukumu yetu kiufanisi kwa maendeleo ya wananchi wa Zanzibar. 
Mpango mkakati huo ulikuwa na malengo yafuatayo:-
·       Kuimarisha mazingira mazuri ya kazi pamoja na wafanyakazi
·       Kutayarisha mwongozo wa kazi za ukaguzi (Regularity Audit manual ) na
·       Kujenga Afisi za kisasa Unguja na Pemba.
Jambo la kujivunia ni kwamba Ofisi yetu imekamilisha na kufanikiwa kutekeleza mpango huo   kwa kiwango cha hali ya juu na kupatikana kwa ufanisi mkubwa katika kutekeleza majukumu yake ya kikatiba.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Ofisi yetu baada ya kukamilisha utekelezaji wa Mpango Mkakati  uliyopita wa mwaka 2007-2011, tumeandaa Mpango Mkakati mwengine wa muda wa miaka mitatu kuanzia mwaka 2011 hadi 2014 ambao kwa sasa ndio tunaoufanyia kazi. Mpango huu ni muendelezo wa hatua zilizofikiwa katika kuimarisha shughuli za ukaguzi wa mahesabu ili uende sambamba na mabadiliko ya ukaguzi na teknolojia duniani kwa kufuata viwango vya ukaguzi vilivyopo kitaifa na kimataifa.
Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali  katika kipindi cha miaka mitano imefanikiwa kwa ufanisi mkubwa kutekeleza majukumu yake ya kikatiba kama yalivyoainishwa katika kifungu 112 (3 ) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na majukumu mengine yaliyoainishwa katika sheria ya fedha namba 12 ya 2005 na sheria ya namba 11 ya mwaka 2003 ya uanzishwaji  Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na sheria nyenginezo.
 Aidha Afisi kwa kiasi kikubwa imeweza kutekeleza malengo iliyojipangia katika mpango mkakati wake, ikijumuisha kuongeza uwezo wa kitaaluma kwa wafanyakazi, kuwepo kwa vitendea kazi vya kisasa vinavyokwenda sambamba na kasi ya maendeleo na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia duniani.
Aidha wafanyakazi wamepata nafasi ya kufanya kazi  katika mazingira mazuri, jambo ambalo limeongeza kasi na ari za kufanyakazi kwa ufanisi mkubwa kabisa.
 Vile vile Afisi imeweza kutayarisha stahiki na maslahi ya wafanyakazi kulingana na utaratibu uliopangwa ( scheme of service ) kwa kuzingatia umuhimu wa shughuli  za ukaguzi pamoja na taaluma za wafanyakazi , ambapo utekelezaji wake tunategemea utakubaliwa na kuanza muda mfupi ujao, kwani tunaamini Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar, inathamini mchango mkubwa na muhimu unaotolewa na Afisi yetu katika kuimarisha utawala bora na usimamizi mzuri wa rasilimali za umma, kwa maendeleo ya wananchi na Taifa letu kwa ujumla.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Jengo hili ulilolifungua leo rasmi, ukarabati wake umefanya na Kampuni ya kizalendo ya “Stars Construction” iliyopo Zanzibar, na umetugharimu jumla ya Tshs. 328,460,000/- ambapo gharama hizi zote zimetolewa na Serikali yetu tukufu ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa asilimia Mia Moja (100%).
Aidha, vifaa vya kisasa vilivyomo ndani ya jengo hili vikiwemo Samani za Ofisi, vifaa vya mawasiliano na usalama, vifaa kwa ajili ya mafunzo na kazi mbali mbali za ukaguzi, vimegharimu jumla ya Tshs. 27,200,000/-.  Jengo hili litatumika na wafanyakazi wapatao 64 ambapo kila mfanyakazi amepata sehemu ya kufanyia kazi.
Vile vile kuna ukumbi wa mkutano utakaochukuwa idadi ya wafanyakazi 85 na chumba cha kujiongezea taaluma na maarifa Maktaba ambayo itatumika kwa wafanyakazi. 
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Ni jambo la faraja na la kujivunia, kwani vifaa vya mawasiliano na usalama na vya kufundishia vimewekwa na wataalamu wetu wa ndani ya Afisi wa Kitengo cha ICT, kwa kweli wamechukua juhudi kubwa kwa kuhakikisha kuwa jengo linakuwa la kisasa linalokwenda sambamba na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia kwa ajili ya kuelekea katika mfumo mpya wa e- Government.     
Aidha Afisi ina nia ya kuanza ujenzi wa Afisi mpya kwa upande wa Pemba kuanzia mwaka wa fedha ujao wa  2013/2014 kadri hali ya uchumi wa nchi itakaporuhusu. Kwani mazingira ya Ofisi kwa Pemba yanahitaji kurekebishwa kwa lengo la kuimarisha mazingira mazuri na utendaji kwa wafanyakazi.
 Nitakuwa mwizi wa fadhila nisipotoa pongezi na shukrani za dhati kwa Kampuni ya Ujenzi ya  “Stars Construction” ambae ndie Mkandarasi wa jengo hili la Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar. Ni ukweli uliowazi  kuwa kampuni hii  ilifanya kazi usiku na mchana ili kuharakisha na kufanikisha ujenzi wa jengo hili katika muda uliopangwa na kwa viwango vinavyokubalika. Ahsanteni sana kwa hili.
Mheshiwa Mgeni Rasmi,
Ufunguzi huu wa jengo  unakwenda sambamba na uzinduzi wa maktaba ya ofisi, ambayo itatumika kwa kiasi kikubwa  kuongeza maarifa ya wafanyakazi wetu pamoja na kusaidia shughuli mbali mbali zinahusiana  na kazi za ukaguzi.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Baada ya maelezo haya, sina budi kutoa shukrani maalum kwa Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kutuwezesha kifedha  kwa asilimia mia moja ( 100%) kwa kulikarabati na ununuzi wa vitendea kazi na hatimae jengo hili limesimama imara na leo hii umelifunguwa rasmi.
Aidha, ni mategemeo yangu kuwa, Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuiunga mkono Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Saerikali  katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku na kuimarisha utawala bora na kupunguza umasikini nchini.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Baada ya kutoa maelezo haya, kwa mara nyengine tena  kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali natoa shukrani za dhati kwako Mh. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohd Shein  kwa nia yako njema ya kuitakia mema, nchi yetu kwa kudumisha amani na utulivu  kwa maendeleo ya wananchi wake.   Aidha tunamuomba Mwenyezi Mungu akujaalie kila la kheri na mafanikio mema katika jukumu zito la kuiongoza nchi yetu ya Zanzibar, Amin. 
Naomba nichukue nafasi hii kumkaribisha Waziri  wa Nchi, Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora, ili nae aje  atoe maelezo  yake na baadae  akukaribishe Mgeni wetu Rasmi  Mh.  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  uje utupe nasaha zako.
Ahsanteni kwa kunisikiliza


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.