Habari za Punde

Kikwete aomboleza vifo vya Watanzania 15


Na Mwandishi wetu

RAIS Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi kufuatia ajali ya barabarani iliyohusisha lori aina ya Isuzu lililopinduka huku likiwa limebeba abiria.

Ajali hiyo ilitokea katika eneo la Relya kijiji cha Bereko, wilaya ya Kondoa Mkoani wa Dodoma Septemba 15 mwaka huu mbapo watu 15 walipoteza maisha na  wengine 72 kujeruhiwa.

“Nimeshtushwa na kusikitishwa na ajali hii ya lori ambayo, katika kipindi kifupi tangu itokee ajali nyingine iliyogharimu maisha ya watu wengi katika Mkoa wa Mara, imeondoa tena uhai wa watu wetu wengine 14 wasiokuwa na hatia,” alisema Rais Kikwete.


“Mamlaka zote zinazohusika hazina budi kuunganisha nguvu katika kukabiliana na wimbi la ajali za barabarani za mara kwa mara zinazokatisha uhai wa watu wengi wasiokuwa na hatia ambao kimsingi ni nguvu kazi muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu,” alisema.

Aidha Rais Kikwete alisema anawaombea kwa Mola wote waliojeruhiwa kwenye ajali hiyo waweze kupona haraka na kurejea katika hali zao za kawaida  na kuungana tena na familia, ndugu na jamaa zao.

Aliwaomba wafiwa wote wawe na moyo wa uvumilivu na ujasiri katika kipindi hiki kigumu cha kuomboleza vifo vya wapendwa wao.    

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.