Habari za Punde

Yaa Rabb tuokoe na janga hili la madawa ya kulevya


 A K Simai

Nilibahatika kukutana na makala  kwenye facebook chini Voice of Zanzibar zenye kuanza kuwataja wauzaji wa madawa ya kulevya katika visiwa vya Zanzibar.

Lengo na madhumuni ya kuwataja wahusika wa madawa ya kulevya pamoja na kuweka picha zao ni baada ya kuona serikali pamoja na jitihada zake za kupambana na maeawa ya kulevya imeonekana kama ni mojawapo ya sehemu ya tatizo badala ya kuwa suluhisho.


Hili limejitokeza kwa sababu mara nyingi imeonekana wanaokamatwa na kete za unga huwa vidagaa na si papa wakati wauza unga wote wanajulikana kwa majina na wanapouzia.


Mara kadhaa Polisai ambao ndio wamekabidhiwa ulinzi na usalama huonekana kwa madealers wakipewa chao ili kusitokee chochote. Ni Polisi hawa hawa kukitokea Operesheni kamata wauza madawa wao hutoka kinyemela na kuwatonya wauza madawa kwamba ‘kesho’ wazee wanakuja kwa hivyo walale mbele.
Ni Polisi hawahawa sasa wakionekana wao wenyewe wakishiriki katika kuuza baada ya kukamata.




Ujasiri walioonesha Voice of Zanzibar kwa kuwataja moja kwa moja bila ya kificho na kubainisha jinsi wanavyouza madawa haya ni wa kupigiwa mfano kwa upande mmoja. Kwani kuwaname and shame these people kunaweza kuwaadhirisha na kama ni binadamu wenye akhlaaq, haya na staha wanaweza kusikia aibu na asaa Mola awahidi waachane na biashara hii. La wakiwa hawana chembe ya  akhlaaq, maadili au staha basi wataendelea na shughuli yao kama kawaida.


 Kwa upande mwengine kulijitokeza changamoto nyingi katika mtandao wa facebook wakati wengi walipinga watu hawa kutajwa hadharani kwa kuomba kuwepo ushahidi tosha wa kuwatia hatiani na si dhana na tuhuma ambazo mwishowe ni kuhusudiana tu badala ya kusaidiana na wengine wakidai every one should mind his/her own business.


Udogo wa kisiwa cha Zanzibar hauhitaji rocket science kuweza  kuwajua wanaouza madawa ya kulevya vidagaa mpaka mapapa. Ni watu tunaoishi nao tunaocheza nao tunaoshirikiana nao na wengine kufaidi matunda yao bila ya kujali upatikanaji wa mali zao kama ni halali au haramu. Badala ya kujali madhara makubwa wanaosababisha wauza unga sasa tumeanza kufungua vitengo vya kuwatibu waathirika wa madawa ambao ni baba zetu, mama zetu, kaka zetu, dada zetu, watoto wetu au rafiki kama si majirani wetu.


Hili suala la madawa ya kulevya limefanywa kuwa gumu sana kutokana na wahusika kuifanya hii kazi kwa usiri mkubwa. Pia kuweza kuwatia hatiani watu wa aina hii kwa Zanzibar limekuwa ni ndoto kwa nchi inayodai inafuata utawala wa sheria na dhana utawala bora kwani uwezo wa fedha waliokuwa nao unawaogopesha mpaka Polisi, viongozi wa Serikali na kadhalika. Hufanya walitakalo kwa nguvu ya pesa ya haramu ya madawa ya kulevya.


Tatizo baya zaidi ni vipi jamii hii inayoathirika na madawa haya kuwasifu madealers kwamba ni watu smart, wajanja na walioula. Hata jamii ikiwa na shida ndogo ndogo basi huwafuata hawa hawa madealers kwa misaada. 


Niliwahi kujaribu kuwasiliana na mtaa mmoja ulioathirika vibaya na madawa na kukutana na wazee wa mtaa huo kujaribu kuwafahamisha kwamba suala hili sasa si la kipolisi wala serikali maana wameshindwa, lakini sisi kama Wazazi, wanajamii tunaweza kulivalia njuga suala hili ikiwa tutakuwa na dhamira ya kweli. Kwani waathirika tunawajua wauza madawa tunawajua kufikia mtoto mdogo hata akili haijapevuka lakini mtaani anajua kwamba nyumba fulani inauzwa madawa  na fulani ni teja.


Nilijibiwa kwamba kazi hii ni ngumu kwa sababu italeta fitna kubwa mtaani kwani nyumba hizi tayari imekuwa hii ni tijara ya kuwaendeshea maisha yao. Si wao bali wengine wa mtaani hufaidika na uwepo wa wauza unga (wenye biashara ndogo ndogo).


Hivi ndivyo jamii zetu zisizojiamini zilipofikia, zimekoseshwa nyenzo za kuweza kuifanyia kazi jamii. Zimeweza kuwapa wauza unga nguvu zisizo mfano huku wakijigamba ikiwa polisi wameshindwa mtaweza nyie?


Ukweli hali ni mbaya sana na inakithiri kuwa mbaya kila siku zikiendelea tuombe Mungu atusaidie na janga hili kutokana na sababu nyingi za kielimu, kimaisha na kuiga  ambazo matunda yake ni haya ambayo tunayachuma sasa kwa kuwa na Sober Houses, Waathirika wanaokwenda na kurudi ( relapse) , ndoa kuharibika, nyumba kuharibika na kadhalika ni kweli maneno ya wahenga tusipoziba ufa, tutajenga ukuta.


Yaa Rabb – Tuokoe na janga hili

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.