Habari za Punde

Mabilionea waipa Tanzania bn 24.1/-



Na Mwandishi maalum, Marekani
MATAJIRI wawili wakubwa duniani wameichangia Tanzania kiasi cha shilingi bilioni 24.1 kwa ajili ya kuendeleza afya ya akinamama na kusaidia uzazi salama hasa katika maeneo ya vijijini.

Matajiri hao, Michael Bloomberg ambaye ni Meya wa jiji la New York, Marekani na Mama Helen Agerup wa Sweden, wametangaza mchango wao huo mkubwa kwa Tanzania kwenye mkutano maalum wa waandishi wa habari uliofanyika makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani.

Pamoja na matajiri hao katika mkutano huo wa waandishi wa habari walikuwepo ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon.


Kati ya fedha hizo, Meya Bloomberg alitoa kiasi cha dola za Marekani milioni nane kupitia taasisi yake ya Bloomberg Philanthropies wakati mama Agerup alitoa kiasi cha dola milioni 7.5 kupitia taasisi yake na mumewe ya H&B Agerup Foundation.

Meja Bloomberg amekuwa anasaidia afya ya akinamama na juhudi za uzazi salama katika maeneo ya vijijini nchini Tanzania tokea mwaka 2006 wakati hiyo itakuwa mara ya kwanza kwa Taasisi ya H&B kuungana na Bloomberg Philanthropies kusaidia sekta ya afya Tanzania.

Akizungumza kwenye shughuli hiyo, Meya Bloomberg alisema yeye na taasisi yake wameamua kuendelea kuunga mkono jithada za Tanzania katika kuinua afya ya akinamama na kupunguza vifo vya uzazi kwa sababu ya matokeo mazuri ambayo yamepatikana tokea Bloomberg Philanthropies aanze kuunga mkono jitihada hizo za serikali mwaka 2006.

Alisema taasisi yake inajihusisha katika maeneo mawili makubwa.

Eneo moja ni kujenga na kukarabati vituo vya afya na zahanati katika maeneo ya vijijini na pili ni kutoa mafunzo kwa watu wasiokuwa watalaam wa afya pamoja na wakunga kuweza kusaidia uzazi salama vijijini.

Mpaka sasa taasisi hiyo imefundisha kiasi cha watu 106 kuweza kufanya kazi ya uzazi salama na ukunga chini ya msaada wake kwa Tanzania.

“Tunaona matokeo ya kuvutia sana. Hata kama idadi ya akinamama wanaopoteza maisha haijawa ya chini –akinamama 13 kati ya 1,000- kama ile ya Marekani lakini dhahiri kuwa idadi inapungua kwa kiasi cha kutia moyo,” alisema.

 “Zaidi tunaifanya kazi hii katika Tanzania kwa sababu tunashughulika na Rais Kikwete, kiongozi mbunifu, kiongozi mkweli na muadilifu, kiongozi mchapakazi na anayetaka kuonyesha tofauti katika maisha ya wananchi wake,” alisema.

Naye mama Helen Agerup alisema alitembelea Tanzania mwaka jana baada ya kushawishiwa na binti yake ambaye alikuwa ametembelea Tanzania mapema na kuvutiwa na jitihada za serikali na zile za Taasisi ya Bloomberg kuhusu afya ya akina mama.

“Nilivutiwa sana na kazi inayofanywa na serikali ya Tanzania na taasisi ya Bloomberg kuzuia vifo vinavyosababishwa na mambo yanayoweza kuzuilika yaani kutokwa damu kupita kiasi na magonjwa ya kuambukiza kutokana hasa na tatizo la ukimwi,” alisema mama huyo.

Naye Rais Kikwete alimshukuru Meya Bloomberg na mama Agerup akisema kuwa misaada yao inaleta tofauti kubwa katika afya za akinamama katika Tanzania.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.