Habari za Punde

Sera hifadhi ya jamii kunufaisha wazee


Na Mwanajuma Mmanga
SERIKALI ya Mapinduzi  Zanzibar (SMZ) imewataka wazee wa mjini na vijijini kukaa mkao wa kula wakati wakisubiri kukamilika sera ya hifadhi ya jamii kwa  maslahi.

Kauli hiyo ameitowa Waziri wa Nchi Afisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dk. Mwinyihaji Makame wakati wa sherehe ya siku ya wazee duniani zilizofanyika nyumba ya wazee Sebleni.

Dk. Mwinyihaji  alisema serikali iko katika mchakato wa kuandaa sera ya hifadhi ya jamii ambayo itazungumzia maslahi ya makundi yote katika jamii ikiwa ni pamoja na wazee.

Alisema hatua hiyo kwa kiasi kikubwa itasaidia wazee kutokana na wao kuwa ni miongoni mwa watu wanaohitaji huduma na matumizi bora.



"Hatua hii itawezesha kuwasaidia wazee kwa kuwapunguzia umasikini, ambao faida itakuwa kwa wazee wote waliofanya kazi katika serikali na wale waliofanya kazi zao za binafsi," alisema Dk.Mwinyi.

Alisema katika kuhakikisha serikali inaweza kutimiza hilo tayari imeanza kuwajengea uzio wazee hao katika nyumba wanazoishi sebleni.

Nae Waziri wa Ustawi wa Jamii, Maendeleo, Vijana, Wanawake na Watoto, Zainab Mohammed alisema Mapinduzi ya mwaka 1964 yaliweka misingi imara ya kuwatunza, kuwaenzi na kuwathamini wazee bila ubaguzi.

Hivyo alisema wazee wanahitaji matunzo na misaada kutoka kwa watoto waliowazaa, ndugu, jamaa, mashirika na serikali.

Nae afisa kutoka shirika la kimataifa la kusaidia wazee  (Help Age),Amlesset Teworos alisema hali ya afya bora kwa wazee ni jambo la msingi kwani ni rasilimali muhimu kwa taifa.

Siku ya wazee duniani huadhimishwa kila ifikapo Oktoba 1.                            

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.