Habari za Punde

CUF waitaka Zanzibar Leo kulinda GNU



Na Hafsa Golo
CHAMA cha CUF kimelishauri Shirika la Magazeti ya Serikali wachapishaji wa magazeti ya Zanzibar Leo, Zanzibar Leo Jumapili na Zaspoti  kufanya kazi zake kwa kuzingatia kuimarisha serikali ya Zanzibar iliyo katika mfumo wa umoja wa kitaifa (GNU).

Chama hicho kimelitaka gazeti hilo kuendelea kuandika habari zinazoingatia maadili, silka, mila na desturi za Wazanzibari.

Kimesema ni fahari kwa mwananchi Zanzibar kulisoma gazeti la Zanzibar Leo hata mbele ya watoto lakini inakuwa aibu kuyasoma magazeti mengine mbele ya watoto hivyo kulazimu msomaji kulisomea chumbani.

Mkurugenzi  wa Haki za Binaadamu, Habari na Uenezi wa chama hicho, Salim Dimani aliyasema hayo wakati ujumbe wa chama hicho ulipofanya ziara katika ofisi za shirika hilo, Rahaleo mjini hapa.

Aidha alisema magazeti yanayochapishwa na shirika hilo hasa Zanzibar Leo ndio chombo cha habari pekee kinachotegemewa na wananchi kwa kupata habari sahihi.


Alisema gazeti hilo limekuwa likitekeleza majukumu yake ipasavyo, hali iliyosaidia kuongeza wigo wa wasomaji wake.

Dimani alisema Wazanzibari wengi popote walipo wamekuwa wakilitegemea gazeti hilo kupata taaluma na matukio muhimu yanayotokea Zanzibar na duniani, hivyo aliahidi kwamba kwa kuwa CUF ina wajumbe wengi katika Baraza la Wawakilishi, kitatumia fursa hiyo kuhakikisha shirika linapatiwa bajeti ya kutosha pamoja na mtambo wa kuchapia.

Alisema CUF kitaendelea kulitumia gazeti la Zanzibar Leo kutoa taarifa zao za utekelezaji wa majukumu yake kwa faida za wananchi na kulitaka gazeti hilo kufanya haki kwa vyama vyote vya siasa nchini.

Naye Mwakilishi wa zamani, Najma Khalifan alisema CUF  kipo tayari kutoa ushirikiano kwa lengo la kujenga taswira za utendaji katika kuifikishia ujumbe jamii kwa kuwa gazeti ndio chombo pekee ambacho kinahifadhi kumbukumbu kwa muda mrefu.

Alisema amekuwa akifahamu ugumu wa utayarishaji gazeti hasa iwapo upatikanaji wa rasilimali zikiwemo fedha utakapokuwa haupatikani kwa wakati.

Hata hivyo,   alilishauri gazeti hilo kuendelea kutoa taarifa za vyama vya siasa bila ya ubaguzi.

Akizungumzia  changamoto zilizokuwepo katika shirika hilo, Mhariri Mtendaji wa Shirika hilo, Abdulla Mohammed alisema tatizo kubwa linalowakabili ni ukosefu wa ofisi, mtambo wa kuchapishia magazeti na uhaba wa fedha.

Alisema ukosefu wa mtambo unasababisha kuzorotesha majukumu ipasavyo kwani hata zile fedha kidogo zinazokusanywa zimekuwa zikitumika kulipia gharama za uchapaji Tanzania Bara.

"Suala la mtambo ni muhimu  kwani ndio nyenzo mojawapo ya kurahisisha shughuli zetu, iwapo tutapata mtambo wetu tuko tayari kuchapisha hata kurasa 40 za rangi,"  alisema.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.