Na Mwandishi wetu
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. Jakaya Mrisho
Kikwete, amewaongoza Watanzania kuuaga mwili wa aliyekuwa Msajili wa kwanza wa
vyama vya siasa, Jaji George Liundi.
Hafla hiyo ilifanyika kwenye viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam
jana.
Viongozi wengine walioshiriki ibada hiyo ni Makamu wa Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. Mohammed Gharib Bilal, Makamu wa Kwanza wa
Rais wa Zanzibar, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad.
Wengine ni Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe.Benjamin William Mkapa, Mwenyekiti
wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba mpya, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Mwenyekiti wa
CUF, Mhe. Ibrahim Haroun Lipumba, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Mhe. Philip
Mangula na Waziri wa Nchi-Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu na Bunge), Mhe.
William Lukuvi.
Viongozi hao walipata nafasi ya kutoa heshima za miwsho mbele ya
jeneza lenye mwili wa marehemu Liundi,
na baadae kufuatiwa na wananchi na wanafamilia.
Waombolezaji walijawa na majonzi na wengine kumwaga machozi, wakati
mjukuu wa marehemu, ambaye ni mtoto wa mtangazaji, Taji Liundi, alipokuwa
akisoma wasifu wa marehemu.
Jaji Liundi alifariki dunia juzi mchana nyumbani kwake Keko Juu jijini
Dar es Salaam baada ya kuugua malaria, shinikizo la damu na maumivu ya mgongo.
Jaji huyo alitarajiwa kuzikwa jana katika makaburi ya Chang’ombe.
Enzi za uhai wake marehemu Liundi alikuwa msajili wa kwanza wa vyama
vya siasa, na ameacha watoto watatu na wajukuu wanne.
Akiwa jaji, Liundi alipitia hatua ngumu kwenye maisha yake, baada ya
mkewe Agnes Doris Liundi kushitakiwa na Jamhuri mwaka 1979 kwa kosa la kuwaua
watoto wake watatu kwa kuwanywesha sumu Februari 21,1978 nyumbani kwao jijini
Dar es Salaam.
Katika kesi hiyo iliyokuwa mbele ya Jaji Lewis Makame, Agness
aliyeolewa na Liundi mwaka 1967 alihukumiwa kunyongwa hadi kufa.
Wakati huo huo, Maalim Seif alikwenda hospitali ya taifa Muhimbili,
kumjulia hali Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Haroun Ali Suleim alielazwa kutokana na kusumbuliwa
na ugonjwa.
Maalim Seif alimtakia Waziri huyo afya njema na akamuombea kwa
Mwenyezi Mungu amjaalie apone haraka.
Waziri Haroun alimweleza Makamu wa Kwanza wa Rais kwamba afya yake
imekuwa ikiimarika siku hadi siku na kwamba anatarajiwa kupelekwa Afrika Kusini
kwa matibabu zaidi.
Wapelekeni viongozi kutibiwa nje alafu sisu tuliowachagua katika hospitali zetu hakuna hata asprini ccm oyee
ReplyDelete