Na
Said Ameir, IKULU
RAIS
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein,
amesisitiza umuhimu wa Wizara na Idara za Serikali kuzingatia vipaumbele katika
matumizi ya fedha za umma hususan yanapokuja masuala yanayowagusa wananchi.
Alisema
hayo wakati wa mkutano wa kujadili taarifa ya utekelezaji wa mpangokazi wa
Wizara ya Afya katika kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2013/2014.
“Tunahitaji
kuwa makini zaidi wakati tunapopanga matumizi ya fedha katika wizara na kwa
wakurugenzi hawana budi kuhakikisha kuwa maeneo yao ya kipaumbele hasa yale
yanayogusa wananchi moja kwa moja yanapewa umuhimu wa kwanza,” alisema.
Katika
mkutano huo pia alisema serikali imedhamiria kuendelea kuongeza fedha za bajeti
kwa matumizi ya kununulia chakula kwa wagonjwa wanaolazwa katika hospitali
nchini.
Aliutaka
uongozi wa hosptali hizo kuhakikisha kunakuwepo uangalizi mzuri wa matumizi ya
fedha ili ziweze kuwafikia walengwa ipasavyo.
“Serikali
tutaendelea kuongeza bajeti ya chakula kwa ajili wa wagonjwa lakini ni lazima
viongozi wa hospitali wahakikishe fedha hizo zinatumika ipasavyo kuanzia
manunuzi, upishi hadi kinavyowafikia wagonjwa,” alisema.
Aliongeza
kuwa ni muhimu kwa hospitali nchini ikiwemo ya Mnazi Mmoja kuajiri wataalamu wa
lishe kwani sio tu kutasaidia kupunguza gharama za chakula bali pia kuwapatia
wagonjwa chakula wanachostahili kulingana na mahitaji ya afya zao.
Aliiagiza
wizara hiyo kufanya utafiti wa matumizi ya tumbaku katika visiwa vya Unguja na
Pemba ili kuona mwenendo wa utekelezaji wa sheria ya Zanzibar ya afya ya jamii ya mwaka 2012
pamoja na azimio la Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) kuhusu matumizi ya
tumbaku.
Aidha
aliuagiza uongozi wa wizara ya afya kutosita kufanya manunuzi ya dharura ya
dawa au vifaa vya tiba pale inapotokezea haja ya kufanya hivyo ili kuokoa
maisha ya wagonjwa badala ya kusubiri utaratibu mwingine ukiwemo wa kusubiri
misaada.
Alisema
mfumo wa biashara wa kisasa unarahisisha kufanya mambo mengi na kwa haraka,
hivyo siyo vizuri kusubiri misaada kwa yale mambo ambayo yamo ndani ya uwezo wa
serikali.
Rais
wa Zanzibar
alirejea wito wake wa kuzitaka taasisi za umma ikiwemo wizara ya Afya kujenga
utamaduni wa kulipia huduma za umeme na maji zinazotumika kwenye taasisi zao
ili huduma hizo ziweze kuwa endelevu.
“Tunapodaiwa
ni lazima tulipe hakuna lugha nyengine ya kuzungumza kwa kuwa hiyo ni biashara
na kwamba Shirika la Umeme Zanzibar lenyewe linanunua umeme kutoka TANESCO na
lisipolipa tutakatiwa umeme na sote tutakosa huduma hiyo,” alisisitiza.
Awali
akiwasilisha taarifa hiyo ya utekelezaji, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dk.
Mohamed Saleh Jidawi, alisema kwa ujumla imeweza kutekeleza mengi ya majukumu
yake katika kipindi husika kama yalivyoainishwa katika mpangokazi wa wizara
hiyo pamoja na baadhi ya maagizo yaliyotolewa katika kikao kama
hicho kilichofanyika mwezi Novemba 2013.
Mkutano
huo ulihudhuriwa pia na Makamu wa Kwanza wa Rais, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad
na Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Yahya
Mzee.
No comments:
Post a Comment