Na
Mwandishi wetu
RAIS wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, amesema kamwe Tanzania
haitatumia nguvu kumaliza mvutano kati yake na Malawi kuhusu mpaka kati ya nchi
hizo.
Aidha,
Rais Kikwete alisema Tanzania haioni matinki ama busara yoyote kuingia vitani
na nchi yoyote jirani kwa sababu yoyote ile.
Alitoa uhakikisho
huo wakati alipohutubia mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na mamia ya wananchi
kwenye uwanja wa michezo wa mjini Mbamba Bay, mji mkuu wa wilaya mpya ya Nyasa.
Aliwambia
wananchi hao: "Nataka kuwatoeni wasiwasi. Hakuna sababu ya vita. Laleni
usingizi bila wasiwasi, kuleni samaki wenu kwa sababu Tanzania haioni busara ya
vita."
"Tanzania
haiwezi kutumia nguvu kupata suluhisho la mvutano wa mpaka.Tuna uwezo wa kupata
jawabu la tatizo hilo bila kutumia njia ya vita.Tanzania haioni busara hiyo ya
vita. Tuna uwezo wa kupata ufumbuzi kwa njia ya madiliano. Na wala msimamo huo
siyo kwa mpaka wetu na Malawi pekee bali kwa mipaka yote ya Tanzania," alisema.
Rais
Kikwete pia aliwaelezea wananchi juhudi ambazo zimekuwa zinafanywa na Tanzania
kutatua tatizo la mpaka ikiwa ni pamoja na kuliomba jopo la Marais wastaafu
kusaidia kutafuta jawabu la mpaka kati ya nchi hizo mbili.
Marais
hao Joachim Chissano wa Msumbiji, Festus Mogae wa Botswana na Thabo Mbeki wa
Afrika Kusini wanasaidiwa na jopo la kimataifa la mabingwa wa sheria katika
kazi yao hiyo.
Rais
pia aliwahakikishia wananchi wa wilaya ya Nyasa kuwa ahadi na mpango wa serikali
kununua na kuweka meli mpya katika Ziwa Nyasa uko pale pale na kwamba mipango
inafanywa ya kuhamisha chelezo cha kujengea meli kutoka Mwanza kwenye Ziwa
Victoria kuipeleka Itungi, Kyela, Mbeya ili kuanza ujenzi wa meli hiyo.
Katika kampeni
ya uchaguzi mkuu mwaka 2010 aliahidi ununuzi wa meli tatu za kutoa huduma
katika maziwa makuu ya Tanzania ya Victoria, Tanganyika na Nyasa.
Alisema
kiasi cha shilingi bilioni 23 zimetengwa tayari kwa ajili ya kuanza ujenzi wa meli
hiyo.
Alisema
michoro ya meli ya Ziwa Nyasa
imelazimishwa kubadilishwa kidogo kwa sababu ya ukweli kuwa Ziwa hilo lina
mawimbi makali na huchafuka mara kwa mara tofauti na Maziwa Victoria na
Tanganyika.
Aliwaambia
wananchi kuwa serikali inaendelea na mipango ya kujenga reli kutoka Mtwara hadi
Mbamba Bay ili kuzidi kufungua ukanda wa Mtwara na kuweza kubeba chuma na makaa
ya mawe kutoka Liganga na Mchuchuma.
Kabla
ya kuhutubia mkutano wa hadhara, Rais Kikwete ambaye alikuwa katika siku ya
pili ya ziara yake ya siku sita katika mkoa wa Ruvuma, alikuwa na shughuli
nyingi katika wilaya ya Nyasa ambako alizindua daraja la Ruhekei lililoko
kijiji cha Mkalole, kilomita nane kutoka mjini Mbamba Bay.
Alisema
ujenzi wa daraja hilo ambalo lina sehemu tatu limejengwa kisasa kabisa ikiwa ni
maandalizi ya ujenzi wa barabara ya lami kutoka Mbinga, wilaya ya Mbinga kwenda
Mbamba Bay,wilaya ya Nyasa.
"Ni
kweli mwaka 2005 wakati wa kampeni ya uchaguzi mkuu nilishindwa kuvuka hapa kwa
sababu daraja lilivunjika lakini ujenzi huu wa kisasa ni kwa sababu tunajiandaa
kujenga barabara ya lami kuunganisha Mbinga na Mbamba Bay," alisema.
Wakati
huo huo serikali imekiomba Chama cha Mapinduzi (CCM) kuipangia upya malengo ya
kusambaza umeme kwa wananchi kwa sababu malengo yaliyopangwa katika ilani ya uchaguzi
mkuu wa 2010 yamefikiwa na kupitwa hata kabla ya kumalizika kipindi cha miaka
mitano.
Aidha,
imesema upo uwezekano mkubwa kwamba usambazaji wa umeme unaweza kufikia
asilimia 50 ya wananchi wote wa Tanzania ifikapo mwakani kwa sababu umeme sasa
unasambazwa kwa kasi kubwa.
Ombi
hilo limetolewa na Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospter Muhongo, wakati alipozungumza katika
mkutano wa hadhara ambao ulihutubiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, mjini Mbamba Bay, Wilaya ya Nyasa.
No comments:
Post a Comment