Na Ali
Mohamed
MKURUGENZI Mwendeshaji
wa Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC),Mwanahija Almas Ali, amewataka Wakaguzi,
Wapasishaji na Makarani wa shirika hilo, kufanya kazi kwa uadilifu na busara
wanapowahudumia wakulima wa karafuu .
Akitoa
nasaha kwa watendaji hao katika mkutano wa kutathmini utendaji wao katika msimu
wa mavuno ya karafuu kwa mwaka 2013/2014, katika ukumbi wa Benjamin Mkapa Wete,
Mkurugenzi huyo alisema pamoja na mafanikio ya shirika katika manunuzi ya
karafuu bado kuna malalamiko kutoka kwa wakulima vituoni.
Alisema
katika msimu wa 2013/2014 ZSTC imevuka makadirio katika manunuzi ya karafuu
ambapo mafanikio hayo yanaongeza matumaini ya serikali na wananchi kwa shirika
katika kuimarisha uchumi na ustawi wa wananchi kupitia zao la karafuu.
“Serikali na
wananchi wana matumaini makubwa kwa ZSTC kupitia zao la karafuu katika
kuimarisha uchumi na ustawi wa wananchi kwa sababu karafuu ni zao pekee
Zanzibar lilochangia kwa asilimia kubwa pato la taifa hivyo watendaji tuwe
makini ,” alisema.
Alisema ni
lazima watendaji hao ambao wanaazimwa kutoka taasisi za serikali wawe waadilifu
na kutumia busara zaidi wanapowahudumia wakulima katika vituo vya manunuzi .
Kwa upande
wao watendaji hao walisema kwa kawaida huwa wanakabiliana na changamoto nyingi
katika vituo vya manunuzi kutoka kwa wakulima na waliahidi kutumia busara na
taaluma ya huduma kwa wateja katika kukabiliana na changamoto hizo.
Akitoa mada
ya uadilifu katika biashara, Ustadh Omar, alisema kazi ni ibada hivyo ni vyema
watendaji hao ZSTC wakazingatia adilifu katika vipimo ili kulifanya zao la
karafuu kuendelea kuwa neema kwa wananchi.
No comments:
Post a Comment