Habari za Punde

Dk Shein: Serikali inathamini mafanikio yaliyopatikana kutoka kwa Wazanzibari wanaoishi nchi za nje

STATE HOUSE ZANZIBAR

OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

Zanzibar 

9.8.2014

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini mafanikio makubwa yalioanza kupatikana kutoka kwa Wazanzibari wanaoishi nchi za nje (Diaspora) na ndio maana ina mpango maalum wa kuandaa Sera na hatimae Sheria kwa lengo la kuendeleza zaidi mafanikio hayo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dr. Ali Mohamed Shein, aliyasema hayo leo mara baada ya chakula maalum cha mchana alichowandalia Wazanzibari wananoishi nchi za nje (Diaspora) huko katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar.

Katika ghafla hiyo iliyohudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamu wa Pili wa Rais Mhe. Balozi Seif Ali Iddi, Spika wa Baraza la Wawakilishi, Mawaziri, Wawakilishi, Wabunge Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mhe. Abdalla Mwinyi Khamis, Makatibu Wakuu na viongozi wengine.

Wazanzibari wanaoishi nchi za nje waliojumuika katika hafla hiyo iliyoandaliwa na Dk. Shein ambao wapo hapa nchini kwa mapumziko ni kutoka nchi mbali mbali zikiwemo Uingereza, Canada,
Marekani, Denmark, Sweden, Oman, UAE, Ujerumani, Uholanzi, Austria, Switzerland.

Akitoa nasaha zake mara baada ya chakula hicho cha mchana alichowaandalia Wazanzibari hao, Dk. Shein alieleza kuwa michango na misaada yao imeanza kitambo kwa kuweza kusaidia nyenzo pamoja na vifaa mbali mbali hapa nchini na kuzitaja nchi kadhaa ambazo tayari zimeshapata mafanikio kutoka kwa wananchi wake waishio nchi za nje.

Alieleza kuwa mbali ya vifaa na nyenzo hizo mbali mbali Wanadiaspora hao pia wameweza kuchangia utaalamu wao walionao ikiwa ni pamoja na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuendeleza sekta ya elimu hapa nchini kupitia Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) kwa kuweza kufundisha elimu ya Shahada ya Uzamivu.

Dk. Shein alieleza kuwa wataalamu hao wameweza kutoa utaalamu wao kwa Shahada hiyo ya Uzamivu katika lugha ya Kiswahili na tayari hivi sasa wanafunzi wanaowafundisha wanaendelea na masomo yao vizuri. Ambapo pia wapo wengine waliojitokeza kuonesha uzoefu wao wa kazi.

Alisisitiza kuwa nia na lengo la Serikali ni kufanya vizuri zaidi kwani ishara ya mafanikio imeshajitokeza kwa hivi sasa na kusisitiza kuwa kila Mzanzibari alieko nje na ndani ya Zanzibar ana fursa na nafasi ya kuijenga nchi yake. Pia,alieleza kuwa mchakato huo wa kuanzisha Diaspora
wa Tanzania wakiwemo kutoka Zanzibar aliuanza yeye na Rais Jakaya Mrisho Kikwete
tokea akiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutambua umuhimu
wake.

Aidha, Dk. Shein aliwataka Wanadiaspora kuendeleza misingi ya amani na utulivu kwani ni kawaida ya Wazanzibari wakiishi nchi za nje huwa hawabadilishi hulka wala desturi zao hatua ambayo imewajengea sifa kubwa. “Zanzibar inasifika sana kwa amani na utulivu”,alisema Dk. Shein

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar imeweza kupata mafanikio makubwa hasa katika sekta ya utalii ambayo hivi sasa imeweza kutangazwa zaidi katika vyombo vya habari mbali mbali duniani ikiwemo BBC kwa kutambua kuwa Zanzibar ni waasisi wa sekta hiyo na ina vivutio na sifa nyingi za utalii.

Mapema Mshauri wa Rais Ushirikiano wa Kimataifa, Uwekezaji na Uchumi Balozi Mohammed Ramia Abdiwawa alieleza kuwa nchi nyingi duniani zile zinazopokea Diaspora na zile zinazozalisha Diaspora zimepatambua umuhimu na mchango wa Diaspora katika maendeleo ya Kijamii na kiuchumi ambapo kwa upnde wa Zanzibar tayari faida imeshaanza kupatikana hususan katika sekta ya afya na Elimu.

Alieleza kuwa Ofisi inayoshughulikia masuala ya Diaspora imekuwa ikifanya juhudi kubwa ya
kuwa karibu na Diaspora na wengi wao tayari wameshuhudia kwa macho yao juhudi hizo na kadiri siku zinavyokwenda mbele mashirikiano baina ya ofisi hiyo yamekuwa yakiongezeka.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Wanadiaspora Bi Hafsa Hassan Bamba walitoa shukrani zao kwa mwaliko huo na kutoa pongezi kwa jitihada zinazoendelea kuchukuliwa na Mheshimiwa Rais ya kuwashirikisha kikamilifu katika harakati za maendeleo ya nchi yao.

‘Sisi Wanadiaspora hatuna cha kukulipa kwa jitihada za maendeleo ya nchi yetu. Bila shaka Mwenyezi Mungu ndiye atakaekulipa kwa jitihada hizi na tunaomba dua akuzidishie mapenzi uliyonayo ya kuwa karibu nasi kwa kila uchao” alisema Bamba.

Wanadispora hao, waliahidi kuwa Mabalozi na Mawakala kwa kuitangaza Zanzibar katika sekta zote za maendeleo na kijamii na kuiomba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuoneza juhudi katika kukamilisha mchakato wa kuandaa Sera na Diapora kwa lengo la kuimarisha maendeleo na maslahi ya Wazanzibari waishio nchi za nje.

Katika hafla hiyo kikundi cha taarabu cha JKU kiliweza kutoa burudani safi kwa waalikwa wote pamoja na viongozi ambapo Dk. Shein katika nasaha zake alikipongeza kikundi hicho kwa kutoa burudani safi ikiwa ni pamoja na kutoa burudani ya nyimbo za asili zilizoibwa na waimbaji mahiri wa taarabu asilia hapa nchini.

Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.