Na Khamis Haji, OMKR
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti
wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, ametoa wito kwa waganga wa
tiba asili nchini, kuzingatia maadili na taratibu za kazi zao na kuepusha
madhara yanayoweza kuwakumba wananchi wanaowapa huduma.
Aliyasema hayo jana katika
hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar,
Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, wakati wa maadhimisho ya siku ya waganga wa asili
barani Afrika, yaliyofanyika bustani ya Victoria, Mnazi mmoja mjini Zanzibar.
Alisema tiba asili na tiba mbadala
inategemewa na wananchi wengi barani
Afrika na duniani kote, ambapo kwa Tanzania asilimia 60 ya wananchi wake
imethibitishwa hupata tiba hiyo.
Alisema kutokana na haja
iliyopo, waganga wa tiba asili hawana budi kufuata taratibu zilizowekwa na
Baraza la Tiba Asilia katika kuhakikisha hawasababishi athari kwa wateja
wanaofika kupata huduma wanazozitoa.
Alisema fani ya tiba asili
itapata mafanikio na kunufaisha wananchi ipasavyo, iwapo waganga hao
watashirikiana na waganga wa kisasa kuhakikisha matibabu yao yanathibitishwa
kitaalamu na yana ubora unaohitajika.
Alisema serikali inathamini
mchango unaotolewa na waganga hao na itahakikisha mamlaka zinazohusika na
matibabu wanayoyatoa, zinapewa msukumo na kuwezeshwa kutekeleza
majukumu yao
kwa ufanisi zaidi.
Katika hafla hiyo, Rais wa taasisi
ya tiba asili na tiba mbadala ya Afrika Mashariki, Kamuntu Matoke, aliahidi
kuwa wataendelea kusimamia maadili na kuhimiza utunzaji wa miti asili ambayo
imekuwa ikitegemewa na wananchi wengi kwa matibabu.
Hata hivyo, alisema ili waweze
kutekeleza majukumu hayo kwa ufanisi na kufikia matarajio ya wateja wao, nchi
za Afrika
Mshariki zikiwemo Tanzania, Kenya na Uganda hazina budi kuwa na sera
na sheria za tiba asili zenye lengo moja.
Mapema Mwenyekiti wa Baraza la
Tiba Asili Zanzibar, Dk. Mayasa Salum, alisema wanachukua juhudi kubwa kuhakikisha watu wote
wanaofanya kazi za tiba asili na mbadala, wanasajiliwa na kupewa mafunzo ya
kazi hizo.
Alisema hadi sasa Zanzibar kuna
waganga asili 193 waliosajiliwa rasmi na wamekuwa wakinufaika na mafunzo mbali
mbali yanayohusu utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
No comments:
Post a Comment