Habari za Punde

Wazanzibari 500,000 kupata vitambulisho


Na Rahma Suleiman

Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) imeanza kutoa vitambulisho vya taifa kwa wananchi  wa Zanzibar ambapo zaidi ya vitambulisho 500,000 vinatarajiwa kutolewa.

Mkurugenzi wa Nida Zanzibar, Vuai  Mussa Suleiman, alisema katika zoezi hilo wamejipanga vizuri ili kudhibiti maafa yasitokee kama yaliotokea wakati wa uandikishwaji wa zoezi hilo lililosababisha kifo na majeruhi.

Alisema kwa hatua za awali ugawaji huo umeanzia Mkoa wa Kaskazini Unguja na kuwataka  wananchi wanapokwenda kuchukuwa vitambulisho vyao katika vituo walivyopangiwa wachukue stakabadhi  au vielelezo walivyopewa wakati wa uandikishwaji.

Alisema kama stakabadhi zao zimepotea, wanatakiwa kuchukua vitambulisho vingine ambavyo walivitumia wakati wa kujiandikisha.

Kwa mujibu wa Vuai, tayari vitambulisho 20,741 vimeshachapishwa na kutolewa kwa watumishi wa serikali wapatao 17,571.

Alisema idadi hiyo haijafikia lengo lililokusudia kutokana na baadhi ya vitambulisho kutokamilishwa kwani vinafanyiwa uchunguzi wa mwisho na vingine bado havijachapishwa.

Alisema tangu Oktoba 2012 wametambua na kuwasajili wananchi 682,202, lakini waliosajiliwa ni 561,530 (asilimia 82.31).

Alisema changamoto zilizopo katika zoezi hilo ni baadhi ya wananchi wameshapoteza vitambulisho walivyopatiwa kutokana na kutovitunza vizuri, wananchi kutopeleka vielelezo muhimu katika uandikishwaji na baadhi yao kuhusisha zoezi la utambuzi na usajili na masuala ya kisiasa.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.