Habari za Punde

Dk Shein: Kufanikiwa kwa udhibiti na ukaguzi wa fedha ni silaha ya maendeleo

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                           28.10.2014
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa kufanikiwa kwa udhibiti na ukaguzi mzuri wa fedha za serikali ndio silaha kubwa  ya maendeleo ya nchi.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungumzo na aliyekuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Tanzania, Bwana Ludovick Utoh aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kusalimiana na Rais pamoja na kumuaga rasmi baada ya kumaliza muda wake wa kazi.

Katika maelezo yake Dk. Shein alimueleza Bwana Utoh kuwa mafanikio makubwa yameweza kupatikana katika Serikali zote mbili ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutokana na usimamizi mzuri wa fedha za umma.

Dk. Shein alisema kuwa fedha ndio jambo kubwa katika kuendesha serikali, hivyo iwapo usimamizi na udhibiti wake utafanyika vizuri, mafanikio pamoja na maendeleo endelevu yanaweza kupatikana kwa ufanisi mkubwa.

Aidha, Dk. Shein alimpongeza Bwana Utoh kwa utendaji kazi wake mzuri katika kipindi chake chote cha kazi ndani ya miaka minane aliyoitumikia afisi hiyo sambamba na kuonesha mashirikiano mazuri kati ya afisi yake na  afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Zanzibar.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisifu mabadiliko makubwa yaliyopatikana chini ya uongozi wa Bwana Utoh katika afisi hiyo kwani alianza kazi vizuri sambamba na mikakati aliyoiweka katika kufikia malengo yaliokusudiwa na serikali hatua ambayo matunda yake yameonekana. “Hakuna atakaesahau juhudi zako”alisema Dk. Shein.

Nae  Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Tanzania Mstaafu Bwana Ludovick Utoh  alitoa shukurani zake kwa Dk. Shein na kumpongeza kwa kumpa mashirikiano mazuri tokea akiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hadi hivi leo akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

“Nashukuru kwa mashirikiano yako mazuri uliyonipa Mhe. Rais,  katika muda wangu wote wa kazi katika afisi hii, tokea siku ile niliyoapishwa hadi kustaafu kwangu, nashukuru sana... kwani fedha ya umma zinahitaji usimamizi mzuri...fedha za umma sio shamba la mtu”alisema Bwana Utoh.

Aidha, Bwana Utoh alimpongeza Dk. Shein kwa kuiimarisha vyema afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hatua ambayo imeipelekea Zanzibar kuendelea kupata maendeleo makubwa.

Bwana Utoh alisisitiza kuwa katika suala zima la udhibiti, ukaguzi na usimamizi wa fedha za umma, uwajibikaji ndio jambo la msingi kwani bila ya uwajibikaji fedha za umma hazifikii malengo yaliokusudiwa huku akimwagia sifa Dk. Shein kwa kufanikiwa kulisimamia hilo katika uongozi wake.

Bwana Utoh alisema kuwa mafanikio makubwa yameweza kupatikana hasa katika uimarishaji wa Serikali za Mitaa, usimamizi na udhibiti wa fedha za umma sambamba na ujenzi wa majengo kwa ajili ya shughuli za afisi hiyo katika maeneo mbali mbali Tanzania Bara.

Alieleza kuwa katika kipindi chote cha uongozi wake, mashirikiano makubwa yameweza kupatikana kati ya afisi hiyo na ile ya Zanzibar na kutoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa ujenzi wa jengo la kisasa la afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali hapa Unguja sambamba na ujenzi wa afisi kama hiyo huko kisiwani Pemba.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.