Habari za Punde

Majaribio BVR Novemba

Na Fatuma Kitima, Dar es Salaam
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema zoezi la majaribio la uimarishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura, linatarajia kuanza katikati ya Novemba mwaka huu.

Zoezi hilo litafanyika kwa kutumia mfumo mpya wa biometric voter registration (BVR) katika majimbo matatu ya uchaguzi ambayo ni Kawe manispaa ya Kinondoni, Kilombero, halimashauri ya mji wa Kilombero na Mlele, halimashauri ya 

Mlele, ambapo vituo vya uandikishaji vimewekwa katika kata zilizomo kwenye majimbo husika.

Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mkuu (mstaafu) wa Zanzibar, Hamid   Mahamoud, alisema hayo wakati  akisoma taarifa kuhusu kuanza kwa shughuli za uimarishaji wa daftari hilo katika  mkutano na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dares Salaam.

“Tume tayari imekwishapokea baadhi ya vifaa muhimu vya uandikishaji zikiwemo fomu za undikishaji, hivyo kinachosubiriwa ni kupokea BVR 250 zinazotarajiwa kufika wakati wowote kuanzia leo. Zoezi la uandikishaji litakapoanza, vituo vitafunguliwa kuanzia saa 2:00 asubuhi na kufungwa saa 12:00 jioni, vyama vya siasa vinaruhusiwa kuweka mawakala wao katika kituo ili kushuhudia jinsi uandikishaji utakavyofanyika,” alisema.

Alisema baada ya zoezi hilo kukamilika, litaendelea katika maeneo mengine ya nchi.

“Tunatarajia uimarishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura utafanyika kwa wakati mmoja katika mikoa yote nchini isipokuwa mkoa wa Dares Salaam na Zanzibar. Uandikishaji katika mikoa ya Dares Salaam na Zanzibar utafanyika baada ya uandikishaji katika mikoa yote kukamilika. Muda wa uandikishaji  utakuwa ni siku saba katika kila kituo,” alisema.


Alisema uandikishaji katika mikoa yote utaanza Januari, mwakani hadi katikati ya   Februari wakati mikoa ya Dar es Salaam na Zanzibar utafanyika mwishoni mwa mwezi Februari.

Alisema uandikishaji huo utafanyika kwa awamu nne kwenye kila halimashauri ili kutoa fursa ya kuhamisha vifaa vya uandikishaji   kutoka eneo moja kwenda jingine.

Alisema wapiga kura wa zamani yaani wale ambao walikuwa wamejiandikisha katika daftari la zamani, watatakiwa kwenda katika vituo vya kujiandikisha vilivyoko karibu na maeneo wanayoishi kuchukuliwa taarifa zao hasa alama za vidole, picha na saini zao kuingizwa katika mfumo BVR na kupewa vitambulisho.

Alisema wenye kadi za kupiga kura za zamani watatakiwa kwenda na kadi zao katika kituo cha kujiandikisha ili kurahisisha zoezi la kuhamisha taarifa zao.

Kwa wapiga kura waliopoteza kadi au wale ambao kadi zao zimeharibika watatakiwa kwenda kituoni ili kujiandikisha na kupewa kadi mpya.

Alisema wapiga kura wenye vitambulisho vya taifa kutoka Dares Salaam na Zanzibar wanatakiwa kwenda na vitambulisho vyao ambavyo vitasomwa na vifaa maalum ili kupunguza muda utakaotumika kuhamisha taarifa zao.

Alisema uimarishaji huo unahusu pia kuandikisha wapiga kura wapya waliotimiza umri wa miaka 18 au zaidi na wale ambao ifikapo siku ya upigaji kura ya maoni na uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 watakuwa wametimiza miaka 18.

Alisema jumla ya watu milioni 23.09 wenye umri wa miaka 18 na zaidi wanatarajiwa kuandikishwa.

Alitahadharishwa kwamba mpiga kura atakaesajiliwa kwenye buku hilo ndie atakaeruhusiwa kupiga kura.

Naye Mkurugenzi wa uchaguzi, Julias Malaba, alisema shilingi bilioni 15 zimetolewa kwa ajili ya zoezi hilo.

Daftari hilo linatarajiwa kukamilika  Aprili 14 mwakani na litawekwa  wazi   kwa muda wa siku tano katika maeneo yanayohusika  ili kumwezesha kila mtu aliyejiandikisha  aende  kukagua taarifa zake.


Akizungumzia mfumo wa BVR, alisema unasaidia kupunguza ujiandikisha mara mbili na kuwa na taarifa sahihi. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.