Na Salum Vuai
JUMUIYA ya Wewekezaji wa Sekta ya Utalii Zanzibar
(ZATI), imeeleza kuridhishwa na namna Serikali ya Muungano na ile ya Mapinduzi
Zanzibar, zinavyochukua hatua kuhakikisha sekta hiyo inaimarika zaidi na
kuchangia pato la taifa.
Akizungumza katika hafla maalumu ya chakula cha
usiku iliyojumuisha wanachama wa ZATI kwenye hoteli ya Zanzibar Beach Resort
Mazizini, Mkurugenzi Mtendaji wa jumuiya hiyo Pamela Matthew, alisema
ushirikiano wa serikali unachangia sana kuongezeka kwa watalii wanaokuja
nchini.
Pamela alikumbusha ujumbe wa Rais wa Tanzania
Dk. Jakaya Kikwete alioutoa kwenye 'Swahili International Travel Expo' jijini
Dar es Salaam mapema mwezi huu, ambapo Rais alisema, jitihada ziongezewe
maradufu kuwezesha mazingira ya sekta binafsi na wadau wengine kuchangia zaidi
ukuaji wa utalii.
Akimnukuu Rais Kikwete, Mkurugenzi huyo alisema
iko haja ya kufanya kazi ya ziada na nzuri kulingana na hali ya uwekezaji
kwenye sekta ya utalii, utoaji viza, kuweka uwiano wa kodi na ada, kuweka bei
za ushindani na kuimarisha huduma kwa watalii ili wafurahie ziara zao na kujua
thamani ya fedha zao.
Pamoja na mambo mengine, Pamela alisema suala la
usalama katika sekta ya utalii litabaki kuwa ajenda kuu.
Alieleza shukurani zake kuwa, serikali
kujidhatiti katika kuimarisha sekta ya utalii, na kwamba agizo lake la kutaka
wadau wabebe dhamana na kufanya kazi kwa pamoja kuelekea lengo la
utalii kwa
wote, linatekelezwa.
"Ujumbe huu wa Mhe. Rais, unaendana na
mikakati ya jumuiya yetu, ambapo uongozi na wanachama wetu wote wanafanya kazi
kubwa kuhakikisha utalii unaleta tija kwa umma wa Zanzibar na
Tanzania kwa
jumla," alieleza.
Alifahamisha kuwa, takwimu zinaonesha kuwa idadi
ya watalii wa moja kwa moja waliofika Zanzibar mwaka 2013, ilifikia
181,000
kiwango ambacho ni kikubwa.
Aidha alisema inakadiriwa kuwa wageni wengine
250,000 waliingia visiwani humu kutokea Tanzania Bara wakiwa katika mapumziko,
ambapo kwa ujumla idadi hiyo inafanya watalii
waliofika mwaka jana kufikia
400,000.
Pamela alisema idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka
maradufu kadiri sekta hiyo inavyozidi kuimarika.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ZATI Abdulsamad
Said, alisema jumuiya hiyo imepata faraja kubwa kutokana na jitihada za jeshi
la polisi kudhibiti wimbi la vitendo vya kihalifu dhidi ya
watalii.
Alisema kuongeza nguvu za ziada kwa polisi jamii
katika ukanda wa utalii, sambamba na jeshi lenyewe, kumesaidia sana kuuweka
ukanda huo katika hali ya usalama.
Kutokana na mafanikio hayo, ZATI imelitunuku
jeshi la Polisi
Tanzania cheti kwa kutambua ushirikiano na mchango linaotoa
katika kulinda usalama wa hoteli na watalii.
Cheti hicho kilipokelewa na Kamishna wa polisi
Zanzibar Hamdan Omar Makame kwa niaba ya jeshi hilo.
Cheti kama hicho pia, kilitolewa kwa Mamlaka ya
Uwekezaji na Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) na kupokelewa na Mkurugenzi Mtendaji
wake, Salum Nassor.
Mapema, Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania,
Egon Kochanke, aliyealikwa katika hafla hiyo aliisifu Zanzibar kupitia Kamsheni
ya Utalii, jinsi inavyojitangaza kimataifa na kuwavutia watalii wengi kutoka
nchi za nje ikiwemo Ujerumani.
Alisema kwa kutumia maonesho ya kimataifa ya
utalii yanayofanyika kila mwaka jijini Berlin, visiwa vya Zanzibar vimezidi
kung'ara kutokana na kutangaza vivutio vingi maeneo ya kihistoria yaliyopo
nchini.
Balozi huyo alisema, kutokana na sifa hizo, ndio
maana nchi yake inashika nafasi ya pili kwa kuleta watalii wengi hapa nchini,
ikitanguliwa na Italia.
Balozi Kochanke aliahidi kusaidia juhudi hizo
kwa kuzidi kuitangaza Zanzibar nchini kwake, ili kuvutia watalii zaidi na hivyo
kuimarisha juu uchumi wa nchi hii.
No comments:
Post a Comment