Habari za Punde

Kutoka Baraza la wawakilishi: Serikali haina utaratibu wa kutoa mikopo kwa wakulima

Na Miza Othman -Maelezo Zanzibar       30/01/2015.
 
Serikali  ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema Wizara ya Kilimo na Maliasili haina utaratibu wa kutoa  mikopo  kwa wakulima  ikiwemo wafugaji wa nyuki bali  suala la kuwawezesha wananchi ikiwemo mikopo ni la Wizara  ya  Uwezeshaji, Ustawi  wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto.
 
Naibu Waziri wa Kilimo na Maliasili Mtumwa Kheir Mbaraka ameyasema hayo katika kikao cha Baraza la Wawakilishi wakati  akijibu suali la Mh.Saleh Nassor Juma Mwakilishi wa Jimbo la Wawi  alietaka mpango wa Serikali kupitia taasisi za fedha kutoa mikopo yenye masharti nafuu  ili wafugaji waweze kufuga nyuki kitaalamu.
 
Amesema Wizara yake inajukumu la kuwashajihisha na kuwahamasisha wananchi katika ufugaji wa nyuki na kujiunga katika vikundi kwa lengo la kujikwamua na umaskini.
 
Ameongeza kuwa  Wizara yake inatoa mizinga  ya nyuki na mafunzo ya mbinu bora za ufugaji  kwa wale wanaojishughulisha na kazi hiyo kama inavyofanya kwa  wanaushirika wa Tujiendeleze wa Jimbo la Wawi Chake chake Pemba.
 
“Kinachofanyika ni jitihada za kupunguza umaskini na kuwaongezea kipato wananchi kwa kupitia shughuli zao”,  Naibu Waziri Mtumwa Kheir amesema.

Alielezea kuwa  wafugaji wa nyuki wanaweza kupata mikopo binafsi kwa vikundi vya kukopa na kuweka ikiwemo vikoba au kupitia taasisi za fedha zinazotambuliwa na Serikali kitu muhimu ni kutimiza   vigezo na masharti ya taasisi hizo.
 
Pia amesema nia na lengo la Wizara hiyo ni kuvitembelea vikundi vyote  vya wafugaji wa vyuki  ili kuwapa mafunzo yaliyo bora katika kuendeleza ufugaji  wao.
 
Wizara ya Uwezeshaji Ustawi wa Jamii, Vijana,  Wanawake na Watoto kupitia program mbali mbali hutoa mafunzo ya kusarifu mazao kwa njia mabli mbali  kwa vikundi vya  akina mama na makundi mengine katika jamii                           
                                                               Mwisho
IMETOLEWA NA IDARA YA HABARI MAELEZO ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.