Habari za Punde

Kutoka Baraza la wawakilishi: Trilioni 3 zahitajika kuyageuza maeneo ya kihistoria kuwa vivutio kwa watalii


Na Abdula Ali   Maelezo-Zanzibar                                             29/01/2015

Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Zanzibar Mhe. Said Ali Mbarouk amesema zaidi ya shilingi trilioni tatu zinahitajika ili kuyafanya maeneo ya kihistoria kuwa ni kivutio kikubwa kwa watalii nchini.

Hayo ameyaeleza katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja wakati akijibu swali la mwakilishi wa Jimbo la Wawi Mhe. Saleh Nassor Juma.

Amesema hadi sasa Zanzibar ina maeneo ya kihistoria yapatayo 85 Unguja na Pemba, ambayo yatakuwa ni kivutio kikubwa cha Watalii na kuinua Uchumi wa  Nchi ikiwa yatatunzwa, kuhifadhiwa na kutangazwa nje ya nchi.

Ametanabahisha kuwa kwa sasa Serikali inayashughulikia zaidi maeneo ya Ras Mkumbuu, Chwaka, Tumbe na Jambangome ambayo hayako katika uhifadhi mzuri na yameandaliwa mpango maalumu wa kuyashughulikia kwa kuwa kuna maeneo mengi ya kihistoria yanayohitaji kuhifadhiwa.

Amesema kuwa kwa mujibu wa mpango wa Maabara ya Utalii, Ras Mkumbuu imewekwa katika mpango wa mwaka wa fedha wa kujengwa ukuta wa kuzuia maji ya bahari yasiingie katika eneo hilo ili kuifanya Ras hiyo kubakia katika muonekano wake wa sasa na mandhari yaliyo mazuri yenye kuwavutia watalii .


Waziri Mbarouk amefafanua kuwa kuna maeneo mengi yaliyohifadhiwa katika kipindi cha hivi karibuni miongoni mwa maeneo hayo ni Kijichi, Kwa Bikhole, Maeneo ya Mahandaki yaliyotumika katika Vita vya Pili vya Dunia, Eneo la Pango la Watumwa na Mnara vyote vilivyoko Mangapwani Mkoa wa Kaskazini Unguja ambapo ujenzi wa Makumbusho kwenye Pango la Kumbi tayari umeshamalizika.

Waziri Mbarouk amesema ipo haja kwa Serikali kushirikiana na Kamati za Vijiji husika ili kuweza kuyahifadhi maeneo ya kihistoria kwa ajili ya vizazi vijavyo pamoja na kuzitaka kamati hizo za Vijiji kukarabati sehemu hizo pale wanapoona kuna maharibiko yamejitokeza.

Aidha Waziri Mbarouk amesema Serikali imekuwa ikichukua tahadhari kubwa kuona Kazi za Sanaa zikiwemo za Filamu na Muziki haziendi kinyume na Mila, Silka na Utamaduni wa Mzanzibari na badala yake ziwe ni zenye kutoa mafunzo pamoja na kuelimisha jamii.

Amesema katika kuhakikisha hayo Wizara yake inazingatia utekelezwaji wa Sheria Namba 1 ya Mwaka 2009 ya Bodi ya Sensa, Sheria hiyo iliundwa kwa lengo la kuhakikisha kazi zote za Sanaa na Utamaduni zinahakikiwa, ili kuhakikisha mafunzo yanayopatikana katika Sanaa hizo yanaenziwa, kulindwa, kukuzwa na kuendeleza Mila, Silka na Utamaduni wa Mzanzibari.

Amefafanua kwamba kwa kiwango kikubwa kazi hiyo imefanyika na hivi sasa Bodi ya Sensa ya Zanzibar inafanya kazi na Bodi ya Sensa ya Tanzania Bara katika kutekeleza jukumu la kuzuia uoneshwaji wa kazi za Sanaa zinazokwenda kinyume na Maadili ya Nchi yakiwemo Mavazi ya Wasanii yasiyokuwa na Stara na yanayokwenda kinyume na Utamaduni wa Mtanzania.

Waziri Mbarouk amewataka wasanii wa Filamu pamoja na Muziki kuwacha kuiga utamaduni wa Kimagharibi kwa kutoa kazi za sana ambazo zinahamasisha Ngono na kupelekea kumong’onyoka kwa Maadili ya Mtanzania.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.