Na Abdula Ali Maelezo-Zanzibar
Naibu Waziri wa Afya
Zanzibar Mhe. Mahmoud Thabit Kombo amesema Serikali haiwazarau Wakunga wa Jadi na
badala yake imeamua kuwapatia vibali maalumu ambavyo vitawahalalishia ufanyaji
wa kazi zao bila ya usumbufu ili kuokoa vifo vya akina mama wajawazito wakati
wa kujifungua.
Hayo ameyasema katika
ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja wakati
akijibu swali la mwakilishi wa kuteuliwa wa Nafasi Maalumu za Wanawake Mhe.
Panya Ali Abdalla.
Naibu Waziri huyo
amesema kuwa Wakunga hao watapewa vibali hivyo baada ya kupatiwa mafunzo
maalumu na kuhitimu vizuri katika ngazi ya uzalishaji (Ukunga) na kutanabahisha
kuwa Wakunga hao wana umuhimu mkubwa katika jamii kutokana na kazi yao hiyo
muhimu na hususan kwa akina mama wajawazito ambao wanatarajia kujifungua.
Amefafanua kuwa lengo
la Serikali la kuwapa mafunzo wakunga hao ni kupunguza vifo vya akina mama wajawazito ambao husumbuka
kwa kutembea masafa marefu kutafuta huduma ya kujifungua na anaamini kuwa
kutokana na elimu watakayopewa wakunga hao watasaidia kina mama hao kujifungua
salama bila ya kusumbuka kwa kutembea masafa marefu.
“Mara nyingi vifo hivi
huchangiwa na kuchelewa kwa mama mjamzito kufika katika Kituo cha huduma kitu
ambacho kinapelekea kukosa huduma ya haraka”, alieleza Naibu Wazir Thabit Kombo.
Naibu Wazir Thabit
Kombo ametanabahisha kuwa suala la kupunguza vifo vya kina mama vinavyotokana
na Uzazi ni moja kati ya maeneo yanayopewa kipaumbele katika Sekta ya Afya na
ili kupunguza tatizo hilo serikali inahitaji mashirikiano ya pamoja kati ya Wizara
ya Afya, Jamii na Sekta nyengine.
Amesema jamii ina
wajibu mkubwa katika kukabiliana na tatizo hilo kwa kufanya maamuzi ya haraka
wakati mama mjamzito anapohisi dalili za kutaka kujifungua ili kuokoa uhai wa
mama huyo na mtoto, kwani vifo vya uzazi hushuka na kupanda kati ya Mwaka hadi Mwaka,
takwimu za vifo zinaonesha kuwa Mwaka 2011 vifo 77 vilitokea na kushuka hadi
vifo 62 Mwaka 2012 na baadae kupanda tena Mwaka 2013 ambapo vifo 103
viliripotiwa kutokea na vifo 80 kwa Mwaka 2014.
Amesema kutokana na
vifo hivyo Wizara yake imechukua hatua mbalimbali katika kuhakikisha tatizo
hilo linapungua kadri itakavyowezekana, ikiwemo kupeleka huduma ya kujifungua
karibu na wananchi, kuongeza wahudumu wa afya ya uzazi katika vituo vinavyotoa
huduma hiyo, kuandaa mpango maalumu wa upatikanaji wa dawa na vifaa vya akina
mama na watoto.
Akielezea hatua
nyengine Mhe. Thabit Kombo amesema Serikali imeanzisha mpango wa kusomesha
masomo ya juu yanayohusu kina mama na watoto (Obstetrics and Gynaecology, Peadiatrics
and Child Health Care, Neonatology), kuendelea kutoa elimu kwa akina mama juu
ya umuhimu wa kuhudhuria katika vituo vya afya mapema ili kugundua matatizo kwa
wakati na kuyafanyia kazi kwa wakati unaostahiki, na kuendelea kushirikiana na Wakunga
wa Jadi ili kuwapeleka akina mama katika vituo vya afya na Hospitali kwa ajili
ya kujifungua.
Amefafanua kuwa
sambamba na jitihada hizo wizara yake imepanga mpango maalumu wa kujadili kila
kifo kinachotokea (Maternal Death Audit) ili kujua sababu ya kifo cha mama huyo
na kuweza kujipanga ili kifo kama hicho kisitokee tena pale inapowezekana.
No comments:
Post a Comment