Habari za Punde

Dk Shein Akutana na Mhe Wang Jiaru Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Baraza la Ushauri

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Mhe,Wang Jiarui  Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Baraza la Ushauri wa Kisiasa la Watu wa China pia Waziri wa Idara ya Kimataifa wa kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China alipofika Ikulu Mjini Zanzibar akiwa na ujumbe wake leo,[Picha na Ikulu.]
  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                                                                            27.3.2015
---
SERIKALI ya Jamhuri ya Watu wa China imeahidi kuendelea kuiUnga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi yake ya maendeleo sambamba na kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu  ulioasisiwa na viongozi wake wakuu.

Makamo Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Baraza la Ushauri wa Kisiasa la Watu wa China ambae pia, ni Waziri wa Idara ya Kitaifa wa Kamati Kuu ya Chama Cha Kikomunisti cha China Mhe. Wang Jiarui, aliyasema hayo leo huko Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwekitiwa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Wang Jiarui, alimueleza Dk. Shein kuwa China inathamini uhusiano na ushirikiano huo wa muda mrefu kati yake na Tanzania ikiwemo Zanzibar hatua ambayo imeweza kuleta maendeleo makubwa kwa pande zote mbili.

Mhe. Jiarui alisisitiza kuwa China itaendeleza yale yote yalioasisiwa na viongozi hao na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika miradi yake mbali mbali kwani inatambua juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein.

Aidha, Waziri huyo wa Idara ya Kitaifa wa Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China, alimueleza Dk. Shein kuwa mafanikio yaliopatikana nchini mwake na kumueleza kuwa hatua hiyo imefikiwa kutokana na msimamo madhumuti sambamba na mikakati iliyowekwa chini ya chama cha Kikomunisti cha nchi hiyo.


Alisema kuwa viongozi wa China na Tanzania wamekuwa na uhusiano na ushirikiano mwema katika kuendeleza maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii hatua ambayo hupelekea viongozi wa pande zote mbili kufanya ziara kwa ajili ya kupanua wigo wa maendeleo.

Kiongozi huyo pia, alisisitiza haja ya kuimarishwa kwa uhusiano na ushirikiano wa kibiashara kati ya China na Tanzania ikiwemo Zanzibar kwa kutambua kuwa hivi sasa nchi hiyo imepiga hatua kubwa kiuchumi ikiwa inashika nafasi ya pili duniani.

Pamoja na hayo, kiongozi huyo alisisitiza haja ya kuwajengea misingi imara vijana kwa kutambua mchango wao mkubwa katika kuziletea nchi zao maendeleo katika sekta zote muhimu.

Alisema akuwa vijana ndio nguvu kazi ya Taifa hivyo kuna kila sababu kuwapa kipaumbele katika kuhakikisha wanajenga nchi yao na kueleza kuwa vijana ndio waliosimama kidete wakati  wa kudai huru kwa upande wa China na Tanzania hivyo kuna kila sababu ya kuwaunga mkono katika juhudi zao za kimaendeleo.

Alisisitiza kuwa China imeweza kushirikiana vyema na nchi za Afrika katika kuimarisha sekta za maendeleo na uchumi na kuahidi kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo kwa nchi hizo ikiwemo Tanzania.

Sambamba na hayo, Kiongozi huyo alieleza kuvutiwa kwake na visiwa vya Zanzibar kutokana na maumbile yake kiutalii na kueleza azma ya watalii kutoka nchi hiyo kuendelea kuja kuitembelea Zanzibar.

Aidha, Makamu Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Kitaifa ya Baraza la Ushauri wa Kisiasa la Watu wa China alisema kuwa  chama hicho kina historia kubwa na ya muda mrefu kati yake na Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kueleza kuwa uongozi wa chama hicho utaendeleza uhusiano na ushirikiano huo kama ulivyoasisiwa na viongozi wake wakuu.

Nae Dk. Shein kwa upande wake alitoa pongezi kwa kiongozi huyo kwa kufanya ziara yake hapa Zanzibar hatua ambayo inaonesha jinsi China inavyothamini uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya pande mbili hizo na kuahdi kuwa Zanzibar nayo itauendeleza.

Dk. Shein alisema kuwa China ina historia kubwa katika juhudi za kuiunga mkono Zanzibar na ni miongoni mwa nchi za mwanzo zilizoyatambua Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 na kusisitiza kuwa  ni miaka 51 hivi sasa tokea China iwe na uhusiano na mashirikiano na Tanzania ikiwemo Zanzibar muda ambao umeweza kuleta mafanikio makubwa ya kimaendeleo, kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa China kutokana na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya afya kwa kuendelea kuleta madaktari kutoka nchini humo sambamba na juhudi zilizokuwa zikifanywa na nchi hiyo kwa kuleta wataalamu wa sekta mbali mbali.

Aidha, Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutekeleza malengo yake sambamba na mikakati yake ukiwemo Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA) ambao hivi sasa uko awamu ya pili sambamba na Dira ya 2020.

Alieleza kuwa juhudi zimekwua zikichukuliwa katika kuimarisha sekta za afya, elimu, kilimo, miundombinu, maji safi na salama na nyenginezo huku akigusia suala la kuimarisha sekta ya utalii ambayo imekuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa sambamba na ukuaji wa uchumi wa Zanzibar.

Dk. Shein,  pia, alieleza haja ya kuwepo kwa mashirikiano kati ya Manispaa za mji wa Beijing na Zanzibar hatua ambayo itaimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano wa viongozi na wananchi wa maeneo hayo sambamba na kuimarisha sekta ya utalii hapa Zanzibar.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa mara zote azma ya vyama vya siasa ni kuleta maendeleo hivyo kwa upande wa CCM hilo ndilo jambo ililolipa kipaumbele na tayari imefanikiwa kwa hilo kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara na kusisitiza kuwa CCM itaendeleza uhusiano na Chama Cha Kikomunisti cha China.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.