Habari za Punde

Maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani Kitaifa Kufanyika Viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar- es -Salaam

Mkuu wa wilaya ya Ilala Bw. Raymond Mushi akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam kuhusu maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani mwaka 2015 alipokutana na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam. Maadhimisho ya mwaka huu yanalenga kuwakumbusha na kuwaelimisha wananchi juu ya athari za Malaria na mbinu za kukabiliana na ugonjwa huo.(Picha na Aron Msingwa

Na. Mwandishi Wetu – Dar es salaam.
Tanzania itaungana na mataifa mengine kuadhimisha Siku ya Malaria duniani Aprili 25 mwaka huu ili kutathmini mafanikio ya utekelezaji wa mikakati  mbalimbali ya kupambana na ugonjwa huo hapa nchini.

Mkuu wa wilaya ya Ilala Bw. Raymond Mushi akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam kuhusu maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani mwaka 2015, leo jijini Dar es salaam amesema maadhimisho ya mwaka huu yanalenga kuwakumbusha na kuwaelimisha wananchi juu ya athari za ugonjwa wa Malaria na mbinu za kukabiliana na ugonjwa huo.

Amesema maadhimisho hayo kitaifa yatafanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja jijini Dar es salaam chini ya kauli mbiu isemayo Wekeza kwa Maisha ya Baadaye, Tokomeza Malaria huku msisitizo mkubwa ukilenga kuikumbusha na kuielimisha jamii kuepuka athari na madhara yanayotokana  na ugonjwa huo.

Bw. Mushi amesema maadhimisho ya mwaka huu  yamelenga kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa kutambua dalili za malaria na kuwahi kwenye vituo vya kutolea huduma pindi wasikiapo dalili za ugonjwa huo ili waweze kupima afya zao  na kupatiwa matibabu.

“Ugonjwa wa malaria kwa muda mrefu umekuwa na athari kwa nguvu kazi ya taifa na utekelezaji wa mikakati mbalimbali, hivyo ni wajibu wetu kushirikiana kuwaelimisha wananchi kuwahi katika vituo vya afya pindi wasikiapo dalili za malaria” Amesema.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Uhamasishaji Mpango wa Udhibiti wa Maambukizi ya Malaria Dkt. Linda Nakara akizungumza kuhusu maadhimisho hayo amesema kuwa maadhimisho ya mwaka huu yataambatana na wadau mbalimbali wa huduma za afya kufanya maonyesho ya huduma wanazotoa kwa jamii.
Ameongeza kuwa wadau hao pia wataendesha shughuli za uchunguzi wa vimelea vya malaria kwa kutumia vipimo vinavyotoa majibu kwa haraka (MRDT) na matibabu ya ugonjwa wa malaria kwa wale watakaogundulika kuwa na malaria.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.