Habari za Punde

Hotuba ya mhe Waziri Ramadhan A Shaaban kwenye kongamano la mwisho la mradi wa SMOLE II

HOTUBA YA MHE. RAMADHAN A. SHAABAN KATIKA KONGAMANO LA MWISHO LA MRADI WA SMOLE II KATIKA UKUMBI WA SALAMA, HOTELI YA BWAWANI
21 MEI 2015

Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
Mhe. Balozi wa Finland nchini Tanzania, Bibi Sinikka Antila
Waheshimiwa Wawakilishi wa Kibalozi
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa
Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya
Ndugu Makatibu Wakuu
Ndugu Wageni Waalikwa
Mabibi na Mabwana

Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutajaalia afya njema na kutupa fursa ya kukutana hapa leo. Pili nachukua fursa hii kukushukuruni kwa kuweza kuacha shughuli zenu na kushirikiana nasi katika hafla hii muhimu ya mashirikiano baina ya Finland na Zanzibar. Nachukua fursa hii pia kuwashukuru waandaaji wa hafla hii kwa kunialika kuwa ni mgeni rasmi. Nasema Ahsante sana.

Ndugu Wananchi,
Sina budi kuishukuru Serikali ya Finland na watu wake kwa msaada mkubwa wa kimaendeleo uliokuwa unaipa Zanzibar katika nyanja mbali mbali. Finland imeisaidia Zanzibar katika sekta ya maji, sekta ya misitu na sekta ya ardhi na mazingira kwa muda mrefu tangu kwenye miaka 1980. Kwa hili namuomba Mhe. Balozi, awasilishe shukurani zetu za dhati kwa Serikali ya Finland na watu kwa jinsi wanavyotuunga mkono katika jitihada zetu za kuleta maendeleo kwa watu wa Zanzibar.

Mhe Balozi wa Finland
Nikiwa kama Waziri wa Ardhi nautambua mchango wako mkubwa katika kuisaidia Zanzibar kupiga hatua za mara kwa mara. Mapema mwaka 2014 ulisaidia kumleta nchini Waziri Mkuu wa Finland ambaye pia alifika kuangalia shughuli za usimamizi wa ardhi na mazingira. Aidha mwaka huu, mwezi wa Februari, ulishiriki katika uzinduzi wa ZALIS katika Jengo la Ardhi. Hii ni ishara tosha ya jinsi unayoithamini Zanzibar na watu wake.

Ndugu Wananchi,
Leo ni siku nzuri lakini ni siku ya huzuni. Ni siku ya huzuni kwa sababu tunaagana na kipenzi chetu tuliyekuwa naye kwa muda mrefu. Tumekutana hapa kwenye kongamano hili kwa nia ya kuufunga rasmi mradi wa SMOLE II. Mradi huu ulianza mwaka 2010 ambapo mchango wa Zanzibar ni Shilingi million 828 za Kitanzania na mchango wa Finland ni Euro million 9 ambazo ni karibu sawa na bilioni 20.


Mradi huu ingawa si mkubwa lakini haukuwa rahisi kiutekelezaji kwani ulihusisha Idara tano za serikali Idara ya Misitu na Maliasili Zisizorejesheka, Idara ya Mazingira, Idara ya Ardhi na Usajili, Idara ya Mipango Miji na Vijiji na Idara ya Upimaji na Ramani.  SMOLE II katika utekelezaji wake ilisimamiwa na Wizara nne tofauti Wizara ya Fedha, Wizara ya Ardhi, Wizara ya Kilimo na Afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais.

Muundo huu peke yake ulikuwa na changamoto kubwa mbali na lengo kuu la mradi la kupunguza umaskini kupitia usimamizi endelevu wa ardhi na mazingira. Hata hivyo mtakubaliana nami kuwa Idara zilizotekeleza Mradi wa SMOLE II zimefanya kazi kubwa tena kwa ufanisi. Mliopo hapa leo mmeona mafanikio ya Idara hiyo.


Ndugu Wananchi
Naomba nichukue fursa hii nami kuelezea machache baadhi ya mafanikio hayo kwa upande wangu. Naelewa kuwa sasa Wizara yangu ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati imefanikiwa kutayarisha rasimu ya Sera ya Taifa ya Ardhi ambayo imo mbioni kuwasilishwa serikalini. Aidha Mradi wa SMOLE II umefanikisha Marekebisho ya Sheria ya Usajili wa Ardhi, imesaidia utayarishaji wa Sheria ya Kamisheni ya Ardhi na pia kuchangia katika utayarishaji wa Sheria ya Uthamini. Huu si mchango mdogo katika usimamizi endelevu wa ardhi. Mama Balozi nasema Ahsante sana

Vile vile kwa upande wa Idara ya Mazingira na Idara ya Misitu na Maliasili Zisizorejesheka, Mradi wa SMOLE II umesaidia kuzifanyia marekebisho Sheria kuu za Idara hizo pamoja na kusaidia mapitio na marekebisho ya Sera za Misitu na Mazingira. Sambamba na hayo naelewa kuwa Idara zote tano hivi sasa zina Mipango Mikakati yake iliyotayarishwa kwa mashirikiano na Mradi wa SMOLE II. Kwa maoni yangu lengo la kuzijenga uwezo wa kitaasisi idara hizi tano limefanikiwa hasa. Kwa hili sina budi kuwapongeza viongozi na watendaji wa Idara hizi tano kwa utendaji wao mzuri.

Mheshimiwa Balozi
Pamoja na kwamba tupo hapa leo kuagana na kuufunga mradi wa SMOLE II lakini sina budi nikiri kuwa kuna baadhi ya maeneo hatukuwa kufikia malengo yetu. Maeneo hayo ni maeneo ya Usajili wa Ardhi na Uwekaji wa Taarifa za Ardhi chini ya mfumo wa ZALIS.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia MKUZA II mwaka 2010 uliweka lengo la kusajili asilimia 50 ya Ardhi ya Zanzibar ifikapo mwaka 2015. Kwa bahati mbaya sana zoezi la usajili wa ardhi kutokana na sababu za kitaalamu na kisheria lilichelewa kuanza hadi mwaka 2013. Hadi wakati huu ni vikataa karibu 5,000 ndiyo vimeweza kusajiliwa. Hata hivyo, pamoja na matokeo hayo, napenda kukuhakikishia kuwa zoezi hili halitasimama na tutaendelea nalo kwani lengo kuu hasa ni kusajili  ardhi yote kwa asilimia 100.

Aidha lengo la kuanzisha mfumo wa kuweka taarifa za ardhi yaani ZALIS nalo lilichelewa kuanza hadi mwaka 2014. Uwekaji wa miundo mbinu ya mfumo wa ZALIS umekamilika na utayarishaji wa programu za kukusanyia taarifa hizo za ardhi unaendelea. Hapa napenda kukuhakikishia kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea na shughuli hii ya kutayarisha mfumo kamili wa uwekaji wa kumbukumbu zote za ardhi ili uwe ni kichocheo cha usimamizi endelevu wa ardhi na ukuaji wa uchumi.

Mheshimiwa Balozi
Let me say this in English for clarity, the Goverment of Zanzibar is committed to support the land registration process in Zanzibar as well as support the development of ZALIS. However, thorough you, we request Government of Finlad to renew their support in the areas of Systematic Land Registration and Development of ZALIS. These areas were implemented very late in the SMOLE II support.

Ndugu Watendaji
Mradi wa SMOLE II umetusaidia kutupatia ala mbali mbali za usimamizi na uendeleshaji w sekta zetu. Sasa ninachoweza kukunasihini kuwa wakati umefika wa kuonekana kuwa ala hizo za usimamizi kwa maaana ya sera, sheria, mipango mikakati inatekelezwa katika usimamizi endelevu wa ardhi.

Ndugu Wananchi na Wageni Waalikwa
Baada ya maelezo hayo mafupi, kwa niaba yangu binafsi na Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati naomba kutangaza kuwa Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Ardhi na Mazingira wa Awamu ya Pili umefungwa rasmi.

Ahsanteni  kwa kunisikiliza.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.