Habari za Punde

Maalim Seif awahakikishia vijana ajira pindipo akipata ridhaa ya kuchaguliwa kuwaongoza

Na Khamis Haji , OMKR

Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi CUF, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad amesema wananchi wakimchaguwa kushika wadhifa huo atahakikisha vijana kote Zanzibar wanapata ajira za kutosha na za heshima zitakazo wawezesha kuwa na maisha mazuri.

Akihutubia mkutano wa hadhara wa kampeni katika jimbo la Kijini, Wilaya ya Kaskazini ‘A’ amesema uhaba wa ajira kwa vijana wa Zanzibar hivi sasa, ni tatizo kubwa ambalo atalipa kipaumbele katika kulitatua, kwa mujibu wa Ilani bora ya Uchaguzi ya CUF.

Amesema vijana wapatao 300, 000 wa Zanzibar hawana ajira, jambo ambalo linahitaji mipango na mikakati madhubuti, ikiwemo kuwavutia wawekezaji vitegauchumi wenye miradi mkubwa itakayoweza kutoa ajira nyingi.

Amesema mipango mingine atakayosimamia kumaliza tatizo hilo ni kufufua na kuanzisha miundo mbinu ya kiuchumi, ikiwemo bandari na viwanja vya ndege na kuimarisha sekta za uvuvi, kilimo, biashara na ujasiriamali.

Maalim Seif amesema Serikali iliyopo madarakani chini ya CCM haijaonesha uwezao mkubwa kukabiliana na changamoto ya uhaba wa ajira kwa wananchi, na sasa wananchi wanapaswa kumchagua yeye ili aweze kuongoza kwa kutumia Ilani ya CUF.

Naye, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Janet Fusi aliyekaribishwa kuzungumza katika mkutano huo amewataka wananchi katika jimbo la Kijini na Zanzibar kote kumchagua Maalim Seif ili aweze kuharakisha maendeleo yao.

Amesema, Maalim Seif ana uwezo mkubwa wa kutatua kero za wananchi na kuwaletea maendeleo na iwapo watamchagua baada ya miaka isiyozidi miwili eneo hilo la Kijini litakuwa na maendeleo makubwa na wananchi wake wataishi maisha mazuri.    

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.