Habari za Punde

Na Mwandishi Wetu Pemba.
Viongozi wa CCM Zanzibar wamewataka wananchi na wanaCCM kumpigia kura Dk. Ali Mohamed Shein ili aendelee kuiongoza Zanzibar miaka mitano ijayo kwani ahadi zake zinatekelezeka na tayari ameshafanya mambo mengi ya kimaendeleo Unguja na Pemba.

Hayo waliyaeleza leo huko katika mkutano wa Kampeni ya uchaguzi wa CCM uliofanyika Makombeni, Mkoa wa Kusini Pemba uliohudhuriwa na maelfu ya wanaCCM na wananchi ambapo mgeni rasmi alikuwa mgombea nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohamed Shein.

Viongozi hao wa CCM walipata fursa ya kusalimiana na wananchi pamoja na WanaCCM waliohudhuria katika mkutano huo waliwaeleza haja ya kumchagua tena Dk. Shein kutokana na uadilifu wake na utekelezaji wa ahadi zake.

Nae Omar Yussuf Mzee, ambaye ni Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, alisema kuwa ipo haja ya kushindana kwa Sera, kwani Dk. Shein anapofanya na anapoahidi jambo anakuwa ameshafanya hesabu.

Waziri Yussuf alishangazwa na CUF kusema kuwa wakipata madaraka watatoa mshara wa Shilingi laki nne na kuuliza fedha hizo watazipata wapi kwani tayari Dk. Shein ameshaeleza kuwa yeye atatoa kima cha chini kwa mwaka wa kwanza kitakuwa laki tatu kwani anajua fedha zilizopo.

Alisema kuwa tayari CCM imeshashinda na kuwataka wanaCCM kudumisha amani kwani vyama vya upinzani wanataka kuivunja ili uchaguzi usifanyike na kusema kuwa meli itakapokuwa tayari itawachukuwa bure wanachama wa CCM kwenda Unguja kushuhudia Dk. Shein anavyoapishwa.


Waziri wa Maji,Ardhi na Nishati Ramadhan Abdalla Shaaban alisema kuwa mgombea nafasi ya urais kupitia chama cha CUF anawadharau wananchi kwa sababu amekuwa akiwadanganya kwa kiasi kikubwa hasa kwa suala la mafuta.

Alisema kuwa suala la mafuta limeanza kushughulikiwa kwa muda mrefu kwani Dk. Shein baada ya kuingia madarakani ameanza kulishughulikia suala hilo kwani kupata mafuta inachukua muda mrefu ambapo kwa teknolojia ya sasa hufika hadi miaka mitano.

Alisisitiza kuwa tayari Dk. Shein ameshatekeleza Sera na tayari Sheria iko tayari na lililobaki ni kujadiliwa na kusema kuwa huwezi kuchimba mafuta bila ya kuwa na sheria.

Alisema kuwa katika katiba iliyopendekezwa tayari suala la mafuta lilikuwa limeshatolewa lakini hata hivyo tayari sheria ya kutoa ruhusa imeshatolewa baada ya juhudi za Dk. Shein na Rais Jakaya Mrisho Kikwete.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai, alitoa pongezi kwa wanaCCM wa Pemba kwa kuendelea kukiunga mkono Chama Cha Mapinduzi na kusema kuwa CCM inaendesha kampeni kwa kistaarabu bila ya kumtukana mtu wala kugombana na mtu na kuvitaka vyama vya upinzani navyo kufanya hivyo.

Bi Zainab Omar Mohammed ambaye ni Waziri wa Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana , Wanawake na Watoto alieleza kuwa Serikali ina mpango wa kuanzisha Benki ya Wanawake.

Alisema kuwa  wanawake na vijana wamekuwa wakipewa mikopo bila ya riba yoyote na kueleza kuwa CCM haitaki kukopiwa Sera zake huku akieleza haja ya kumpongeza rais kwa kuanzisha Mfuko wa Uwezeshaji.

Alisema kuwa Wilaya zote za Pemba walipewa mikopo, wakulima wa mwani nao waliangaliwa ambapo Rais aliwagaiya mwenyewe wakulima wa zao hilo wa Pemba na Unguja na hivi sasa wanawake hawabebi tena mwani kwenye vichwa.

Alieleza kuwa vijana wamepewa green house ambazo zote hizo amezitoa Dk. Shein na kuwasifu wanaCCM kwa kutoyumba huku akisisitiza kuwa udhalilishaji sasa basi kwani hivi sasa Serikali imo katika kampeni ya kupambana na hali hiyo na atakaefanya hivyo sheria itafuata mkondo wake kwa kufungwa miaka 30.

Alisema kuwa kuna nyumba tatu za wazee ikiwemo ya Sebleni, Welezi na Limbani ambapo wazee wanalelewa na kupata milo mitatu ya uhakika pamoja na fedha za kujikimu huku watoto yatima nao wakiendelea kutunzwa.

Nae Mjumbe wa Kamati Kuu, Khadija Aboud aliipongeza Wadi ya Makombeni kwa kuhakikisha kila uchaguzi wadi hiyo inakuwa ya CCM na kuwataka wananchi na wanaCCM kuwachagua viongozi wa CCM

Alisema kuwa Dk. Shein ndie Rais anaefaa kutokana na kuleta maendeleo makubwa Zanzibar ndani ya miaka mitano iliyopita na  anafaa kupewa miaka mitano mengine huku akiwataka vijana kuichagua CCM.  

Nae Haji Mkema, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM aliwataka wananchi na wanaCCM kumpa kura zote Dk. Shein kutokana na kutekeleza sekta za maendeleo ikiwemo maji, umeme, barabara, afya sambamba na kudumisha amani na utulivu.

Alisema kuwa hulka na tabia yake ikiwa ni pamoja na kuwa na huruma ambapo tayari hivi karibuni ameshaiondosha michango ya skuli za msingi na Sekondari hapo baadae huku akiondosha malipo kwa wazazi pamoja na wazee.

Alimsifu Dk. Shein kwa kuimarisha uwanja wa Gombani, uwanja wa Amani na uwanja wa Maotsetung hivi karibuni utaanza matengenezo na hivi karibuni Fumba kutatengenezwa uwanja mwengine mpya wa michezo.

Skuli za Sekondari zimeimarika ikiwa ni pamoja na kuleta waalimu kutoka sehemu mbali mbali wakiwemo kutoka Nigeria, kuwepo kwa vyuo vikuu na kuanzishwa kipya huko Dole pamoja na kuimarisha vyuo vya amali ambapo hivi karibuni vyuo hivyo vitaengezwa katika maeneo ya Mtambwe na Makunduchi.

Mapema Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba Mberwa Hamad Mberwa, alisema kuwa ushindi wa CCM wa mwaka huu utakuwa mkubwa tena wa kishindo sambamba na kupata mafanikio mara tatu kuliko yale ya mwaka 2010.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.