Habari za Punde

Balozi Seif Azungumza na Waandishi na Kusema Sherehe za Mapinduzi Zipo Palepele 12Januari.


Na Othman Khamis OMPR.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba Maadhimisho ya Sherehe za kutimia Miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964  yatafanyika kama kawaida na kupangwa kuanza rasmi kesho jumapili ya Tarehe 3 Januri 2016.

Alisema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha kwamba katika muda wote wa maandamisho hayo kunakuwa na hali ya utulivu na usalama mkubwa katika maeneo yote ya Visiwa vya vya Unguja na Pemba.

Balozi Seif Ali Iddi ambae pia ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Maadhimisho ya Kitaifa Zanzibar alisema hayo wakati akitoa Taarifa rasmi ya ratiba ya maadhimisho ya sherehe za Miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar mbele ya Wana Habari hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.

Alisema suala la upande wa Upinzani kuzisusia sherehe za Mapinduzi   kwa kisingizio cha Rais aliyepo madarakani si halali ni muendelezo wa kuwapotosha Wananchi walio wengi nchini.

Balozi Seif alifafanua kuwa Rais wa sasa Dr. Ali Mohammed Shein ataendelea kuwa rais hadi yule atakayechaguliwa rasmi na kihalali na Wananchi ale kiapo kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar  ya mwaka 1984 kama ilivyokwishatolewa ufafanuzi na wanasheria walio wengi.

Alisema tukio hili la maadhimisho ya sherehe za Mapinduzi ya Zanzibar kutimia miaka 52 ni jambo la kujivunia kwa kila Mwananchi  wa Visiwa vya Unguja na Pemba mpenda maendeleo na anayeifahamu vyema Historia ya Zanzibar kabla na baada ya Mapinduzi.

Alieleza kwamba ipo miradi mingi na tofauti ya Wananchi ambayo Viongozi na hata baadhi ya  wanachama wa upande wa upinzani walishiriki kuibuni sasa inakuaje miradi hiyo waiachie wakati tayari imeshalengwa kuinufaisha jamii iliyowazunguuka.

“ Tuna kila sababu na ni haki yetu kusherehekea siku hii adhimu katika Maisha yetu. Hivyo tuambizane, tushajiishane na tushiriki katika matukio mbali mbali ya maadhimisho ya sherehe hizi kuanzia mwanzo hadi mwisho “. Alisema Balozi Seif.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  alieleza kwamba Miradi yote ya Maendeleo ipatayo 24 ambapo 16 ikiwa imekamilika na Minane inatarajiwa kuwekwa mawe ya msingi imehusishwa katika maadhimisho hayo itakayoanza Jumatatu ijayo.

Alisema madhimisho hayo yataanza rasmi kesho Jumapili  ikiwa ni siku maalum kwa kazi za usafishaji wa masingira katika maeneo mbali mbali Unguja na Pemba ukilenga zaidi katika sehemu za kutolea huduma za kijamii kama Hospitali, Vituo vya Afya pamoja na  masoko.

Mwenyekiti huyo wa Halmashauri ya Maadhimisho ya Kitaifa Zanzibar alifahamisha kwamba ingawa zoezi hilo hufanyika kila zinaponza sherehe za Mapinduzi lakini mwaka huu juhudi malum zinapaswa kuchukuliwa ili kuhakikisha maeneo yote yanakuwa katika hali ya usafi muda wote.

Alikumbusha kuwa hivi sasa Taifa linakabiliwa na tatizo la kuwepo kwa maradhi ya Kipindupindu, hivyo jamii  ina wajibu wa kutumia fursa hizi za maadhimisho ya sherehe za Mapinduzi kwa kuchukuwa hatua za kujikinga na kupambana na maradhi hayo ambayo kwa kiasi kikubwa husababishwa na mazingira machafu ya sehemu zinazotumika na jamii katika shughuli za kila siku.

Alisema kwa vile suala la usafi wa mazingira ni la lazima Viongozi Wakuu wa Kitaifa watahakikisha  wanaungana na Wananchi katika zoezi hilo kwenye maeneo watakayopangiwa.

Alieleza kwamba utaratibu maalum umeshaandaliwa kwa kila mamlaka za Mikoa, Wilaya, Baraza la Manispaa, Mabaraza ya Miji na Halmashauri za Wilaya katika kuratibu mfumo mzima wa kufanikisha zoezi hilo la usafi wa mazingira.  

Akigusia suala la hatma ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar  ambalo limekuwa agenda kubwa kwa baadhi ya watu wakiwemo hata wanasiasa nchini wakiendelea kupotosha Wananchi  Balozi Seif alisema Taarifa rasmi ya vikao vinavyowakutanisha Viongozi wa juu kulijadili suala hilo itatolewa rasmi mara baada ya kukamilika kwa mazungumzo hayo.

Hata hivyo Balozi Seif alitanabahisha kwamba  Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar {  ZEC } kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar  ya mwaka 1984 ndio yenye mamlaka ya kuendesha na kusimamia uchaguzi Mkuu wa Zanzibar.

Alisema kwa vile tume hiyo kupitia Mwenyekiti wake  haikuridhika na mazingira yaliyojichomoza wakati wa zoezi la kupiga kura na kulazimika kufuta Uchaguzi pamoja na matokeo yake yote Taasisi hiyo hiyo ndio yenye uwezo wa kuitisha uchaguzi mwengine kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar.

Akijibu baadhi ya maswali ya Waandishi wa Habari Balozi Seif alisema katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984 iko wazi na kutoa mamlaka kwa tume ya uchaguzi ya Zanzibar kupanga uchaguzi mwengine kufuatia kufutwa kwa ule wa mwezi oktoba mwaka 2015.

“ Kinachosubiriwa kwa sasa ni Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kutangaza Tarehe ya uchaguzi mwengine ambapo kujumu la kugharamia uchaguzi huo limo ndani ya mamlaka ya Serikali Kuu yenyewe “. Alisema Balozi Seif.
Kuhusu Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi ambao baadhi ya watu wamekuwa wakitoa tafsiri potofu, Balozi Seif aliwajibu wanahabari hao kwamba  Baraza la Wawakilishi lilivunjwa lakini Rais wa Zanzibar  bado anayo Mamlaka  ya kuliitisha iwapo kuna suala muhimu la Kitaifa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.