CHUO KIKUU CHA TAIFA (SUZA)
Sanduku la Posta 146, Zanzibar -
Tanzania
Simu: + 255 24
2230724/2233337/2234063 Nukushi: + 255
24 2233337
Chuo
Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kimetiliana saini mkataba wa makubaliano juu
ya mashirikiano na Chuo Kikuu cha Komoro mjini Moroni katika hafla maalum iliyofanyika
tarehe 19 Januari, 2016 na kuhudhuriwa
na uongozi wote wa Chuo Kikuu cha Komoro, Balozi wa Komoro nchini Tanzania Dkt.
Ahmada El Badaoui Mohamed na Mwakilishi wa Balozi wa Tanzania nchini Komoro, Bw
Mudrik Ramadhan Soragha.
Makubaliano
kati ya vyuo hivi ni moja ya matokeo ya ziara ya nchini Komoro ya Mheshimiwa
Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
aliyoifanya hivi karibuni.
Profesa Idris Rai, Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) na Dkt Said Bourhani, Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Komoro wakisaini Mkataba wa makubaliano ya mashirikiano baina ya vyuo
vyao.
Katika
hotuba yake kwenye hafla hiyo, Profesa Idris Rai, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha
Taifa cha Zanzibar aliwaeleza wahudhuriaji kwamba ametembea nchi nyingi duniani
lakini Komoro ni nchi ya kwanza ambayo amekuwa akijisikia kama kwamba yuko
nyumbani tokea alipoingia nchini humo. Alisema kwamba kuna uwiano mkubwa sana
baina ya watu wa Zanzibar na watu wa visiwa vya Komoro katika kila nyanja za
maisha.
Makamu
Mkuu huyo wa SUZA aliwaeleza wana Chuo hao kwamba makubaliano baina ya vyuo
hivyo viwili ni tofauti kabisa na mashirikiano ambayo SUZA imekuwa ikiweka
saini na vyuo vingine mbali mbali kwani hayo yanahusisha vyuo vya nchi ndugu ambazo
zinashabihiana kihistoria, kimazingira, kidini na kiutamaduni. Aliwahakikishia
wanachuo waliohudhuria hafla hiyo kwamba SUZA kwa upande wake itahakikisha
mashirikiano ya makubaliano yaliyofikiwa yanapewa kipaumbele na yanatekelezwa
kama yatakavyopangwa.
Mkataba
huo wa mashirikiano umeainisha mambo ya mashirikiano kama ifuatavyo:
-
kusaidiana kuendesha mafunzo ya lugha za Kiswahili na Kiingereza kwa
upande wa Komoro na lugha ya Kifaransa katika ngazi ya Shahada kwa upande wa
SUZA.
-
Kufanya tafiti za pamoja kwenye maeneo ya sayansi jamii na historia,
tamaduni, lugha, dini kwa upande mmoja na masuala ya mazingira, rasilimali
asilia na bahari kwa upande mwingine.
-
Kubadilishana walimu na wanafunzi baina ya SUZA na Chuo Kikuu cha
Komoro.
-
Kusaidiana kujenga uwezo wa wanataaluma wa vyuo viwili hivi kwa maeneo
ambayo Chuo kimoja kina uwezo zaidi.
-
Kuandaa mapendekezo ya kuazisha taasisi ya pamoja inayohusu masomo ya
Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Komoro.
Ilibainika
kwamba moja ya kikwazo kikubwa cha utekelezaji wa mashirikiano haya kitakuwa ni
lugha ambapo lugha kuu ya taaluma inayotumika katika Chuo Kikuu cha Komoro ni
Kifaransa wakati lugha inayotumika SUZA ni Kiingereza na Kiswahili. Mafunzo ya
lugha katika makubaliano haya yataweza kuondosha kikwazo hicho hivyo
kuwawezesha wanafunzi na wafanyakazi wa vyuo hivi kutembeleana kwa masomo na
kushirikiana katika kufanya tafiti za pamoja.
Kwa
upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Komoro, Dkt Said Bourhani aliwaambia
wanachuo wa Chuo Kikuu cha Komoro kwamba utekelezaji wa mashirikiano haya ni
tofauti na mashirikiano na vyuo vingi kwani safari ya Tanzania, Zanzibar kutoka
Moroni ni fupi na rahisi. Pia aliwashukuru marais wa Zanzibar na Komoro kwa
kufikiria na kutaka Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) na Chuo Kikuu cha
Komoro kuanzisha mashirikiano haya.
Chuo
Kikuu cha Komoro na SUZA ni vyuo vichanga lakini vimekuwa kwa kasi kubwa katika
miaka ya karibuni. Wakati Chuo Kikuu cha Komoro kilianzishwa mwaka 2003 na
kikiwa ni Chuo Kikuu pekee nchini Komoro kikiwa na wanafunzi karibu 9,500
katika masomo ya fani mbali mbali, Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar
kilianzishwa mwaka 2001 na sasa kina wanafunzi karibu 4,000 waliojiunga na
masomo kwenye karibu fani 40 katika ngazi za cheti hadi shahada ya uzamivu.
Mara
tu baada ya ziara yake nchini Komoro, imekuwa ni hamu kubwa ya Dkt. Ali Mohamed
Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuona Chuo Kikuu
cha Taifa cha Zanzibar kinashirikiana kwa karibu sana na Chuo Kikuu cha Komoro.
No comments:
Post a Comment