Habari za Punde

SMZ yasikitishwa na kulaani matukio ya uchomwaji moto

Na Haji Nassor, Pemba

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar imesikitishwa na kulaani vikali, matukio zaidi ya manane ya uchomaji nyumba za wananchi, matawi ya vyama pamoja na majengo ya serikali yaliojitokeza kisiwani Pemba, usiku wa kuamkia Machi 12 mwaka huu.

Akitoa taarifa ya Serikali waziri wa nchi afisi ya Makamu wa pili Zanzibar Mhe: Mohamed Aboud Mohamed mjini Chakechake, alisema serikalili hairidhishwi hata kidogo na matendo hayo.

Alisema serikali kila siku imekuwa ikipiga kelele kwa wananchi kuendelea kuishi kwa amani na utulivu, ikiamini kuwa ndio msingi wa kufikia maendeleo ya kweli.

Waziri Aboud alisema suala la siasa kuitia moyoni hadi kupelekea kutiliana moto, sio jambo jema na wala sio malengo ya kuwepo kwa mfumo wa vyama vingi nchini.

Alieleza kuwa, suala la uchomaji moto, haliashirii mwisho mwema miongoni mwa wananchi, na ndio maana amewataka wananchi waliokumbwa na matukio hayo, kuwa wastahamilivu na serikali inaendelea kuwatafuta wahusika, ili wafikishwe mbele ya vyombo vya sheria.

“Serikali kwa kupitia Jeshi la Polis, linaendelea na uchunguzi wa hali ya juu, ili kuwapa wahusika na kisha sheria ichukuwe nafasi yake, maana matendo haya sio ya kuyavumilia’’, alifafanua.

Alibainisha kuwa kuanzia kipindi cha mwezi Febuari mwaka huu, kumeanza kujitokeza tena matukio mbali mbali ya kuashiria uvunjifu wa amani yakiowemo hayo ya utiwaji  wa moto.

Alisema tayari jumla ya nyumba nane za wananchi zimeshateketezwa kwa moto, ikiwa ni pomoja na shehia ya Kangagani nyumba mbili, Mihogoni, Tondooni moja moja.


Nyumba nyengine ambazo zimeshateketezwa kwa moto na watu wasiofahamika ni shehia ya Msuka, Makangale na Tumbe kukiwa na nyumba moja moja, Maskani ya CCM Junguni, tawi la CCM Tibirinzi, na kituo cha afya Kiuyu.

Kuhusu hasara ambayo imepatikana kutokana na matukio hayo manane ambayo yaliripotiwa juzi, kutoka Idara ya maafa, alisema, ni wastani wa shilingi milioni 200 (shilingi milioni mia mbili), ambapo serikali baadae itawafidia wananchi hao.

Katika hatua nyengine waziri huyo wa afisi ya makamu wa pili wa rais Zanzibar, Mohamed Aboud Mohamed, aliwataka wananchi wenye sifa za kupiga kura kwenye uchaguzi wa marudio, kujitokeza kwa wingi bila ya woga.

“Keshokutwa tunakabiliwa na uchaguzi, wala wananchi wasiwe na hofu waende kwenye vituo walivyopangiwa na serikali itaimarisha ulinzi kama kawaida’’,alifafanua.

Hata hivyo waziri Aboud amerejea kauli yake, kuwa serikali haitosita kuwanyang’anya leseni wafanyabiashara yoyote atakaebainika kuendesha mgomo wa utoaji huduma.

“Serikali inarudia kila siku tamko lake, kwamba itawanyng’anywa lesini wafanyabiasha hata akiwa chama gani, kama atatoa huduma kwa njia ya ubaguzi’’,alisisitiza.


Usiku wa kuamkia juzi Machi 12 hasa mkoa wa kaskazini Pemba kuliripotiwa matukio ya uchomaji moto nyumba za wananchi, matawi ya CCM, na kituo cha Afya cha Kiuyu na watu wasiofahamika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.