Habari za Punde

Halmashauri ya Wilaya ya Magharibi Yatoa Siku Mbili Kuondoka kwa Wafanyabiashara Pembezoni mwa Barabara.

Na Takdir Ali - Maelezo Zanzibar. .
Serikali ya Wilaya Magharibi B imetoa muda wa siku mbili kwa wauza samaki pembezoni mwa soko kuu la Mwanakwerekwe kuondoka na atakaepuuza agizo hilo atachukuliwa hatua za kisheria.

Akizungumza na wauza samaki hao  Ofisini kwake Mwanakwerekwe, Mkuu wa wilaya  Magharibi B Silima Haji Haji amesema Serikali imekuwa ikichukuwa juhudi mbali mbali za kuwaelekeza sehemu zinazostahiki za kufanya biashara hiyo  lakini wamekuwa wakikaidi agizo hilo na kusababisha usumbufu kwa watumiaji wa Barabara.

Amesema kabla ya kutoa msimamo huo serikali ya Wilaya imekaa na wauza samaki hao mara kadhaa na kukubaliana kuondoka lakini  lakusikitisha wamekuwa wakiondoka kwa muda na baadae kurejea tena katika eneo hilo.

Amefafanua kuwa uuzaji wa samaki katika eneo la nje ya soko la Mwanakwerekwe kunasababisha uchafu kutokana na  matumbo ya samaki, vumba na kutapakaa Damu katika eneo hilo jambo ambalo limekuwa likiondosha haiba ya soko.


Aidha Mkuu  wa Wilaya ameutaka Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya Magharibi B kufuatilia  agizo hilo haraka iwezekanavyo ikiwemo kuwachukulia hatua wale  watakaokadi  agizo hilo.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Magharibi B Amour Ali Mussa amesema sababu  ya kuongezeka tatizo hilo ni  pamoja na kutokuwepo kuwepo mipango mizuri ya mji wa Zanzibar inayoonyesha mgawanyo mzuri wa masoko na mahitaji ya wateja.

Mkurugenzi Amour mesema wauza samaki hao wametakiwa kuhamia soko  la samaki Mikunguni lakini wamekuwa wakipinga kwa madai hakuna biashara na wamekukwa wakikosa wateja.

Amesema Halmashauri kwa kushirikiana na Wilaya inaandaa mipango maalum itakayoweza kutoa mvuto kwa wananchi wengi kuenda kufuata huduma katika soko hilo la Mikunguni.

Amesema wanafanya utaratibu wa kuweka kituo kikubwa cha daladala ili  wananchi wengi waweze kufika  na kuhamisha Mnada wa Samaki soko la Darajani na kuhamia katika soko hilo.

Mapema wafanyabiashara hao wa Samaki  wamesema hawapingi  kuhamia soko la Mikunguni  lakini kinachopelekea kubakia nje ya soko la Mwanakwerekwe  ni kukosa wateja na  kupata hasara katika biashara yao.

Wamesema hawana tatizo  kuondoka sehemu ili kutii amri ya Serikali lakini wameiomba kuandaliwa mazingira mazuri  yatakayowawezesha kufanyabiashara itakayo waongezea kipato chao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.