Na Takdir Ali - Maelezo Zanzibar. .
Serikali ya Wilaya Magharibi B imetoa muda wa siku mbili kwa wauza samaki pembezoni mwa soko kuu la Mwanakwerekwe kuondoka na atakaepuuza agizo hilo atachukuliwa hatua za kisheria.
Akizungumza na wauza samaki hao Ofisini kwake Mwanakwerekwe, Mkuu wa wilaya Magharibi B Silima Haji Haji amesema Serikali imekuwa ikichukuwa juhudi mbali mbali za kuwaelekeza sehemu zinazostahiki za kufanya biashara hiyo lakini wamekuwa wakikaidi agizo hilo na kusababisha usumbufu kwa watumiaji wa Barabara.
Amesema kabla ya kutoa msimamo huo serikali ya Wilaya imekaa na wauza samaki hao mara kadhaa na kukubaliana kuondoka lakini lakusikitisha wamekuwa wakiondoka kwa muda na baadae kurejea tena katika eneo hilo.
Amefafanua kuwa uuzaji wa samaki katika eneo la nje ya soko la Mwanakwerekwe kunasababisha uchafu kutokana na matumbo ya samaki, vumba na kutapakaa Damu katika eneo hilo jambo ambalo limekuwa likiondosha haiba ya soko.
Aidha Mkuu wa Wilaya ameutaka Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya Magharibi B kufuatilia agizo hilo haraka iwezekanavyo ikiwemo kuwachukulia hatua wale watakaokadi agizo hilo.
Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Magharibi B Amour Ali Mussa amesema sababu ya kuongezeka tatizo hilo ni pamoja na kutokuwepo kuwepo mipango mizuri ya mji wa Zanzibar inayoonyesha mgawanyo mzuri wa masoko na mahitaji ya wateja.
Mkurugenzi Amour mesema wauza samaki hao wametakiwa kuhamia soko la samaki Mikunguni lakini wamekuwa wakipinga kwa madai hakuna biashara na wamekukwa wakikosa wateja.
Amesema Halmashauri kwa kushirikiana na Wilaya inaandaa mipango maalum itakayoweza kutoa mvuto kwa wananchi wengi kuenda kufuata huduma katika soko hilo la Mikunguni.
Amesema wanafanya utaratibu wa kuweka kituo kikubwa cha daladala ili wananchi wengi waweze kufika na kuhamisha Mnada wa Samaki soko la Darajani na kuhamia katika soko hilo.
Mapema wafanyabiashara hao wa Samaki wamesema hawapingi kuhamia soko la Mikunguni lakini kinachopelekea kubakia nje ya soko la Mwanakwerekwe ni kukosa wateja na kupata hasara katika biashara yao.
Wamesema hawana tatizo kuondoka sehemu ili kutii amri ya Serikali lakini wameiomba kuandaliwa mazingira mazuri yatakayowawezesha kufanyabiashara itakayo waongezea kipato chao.
No comments:
Post a Comment