PRESS RELEASE
Zanzibar 11.07.2016
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesema kuwa Zanzibar inaweza kupiga hatua kubwa ya
kimaendeleo katika tasnia ya utengenezaji filamu na maagizo kutokana na
mandhari na historia yake katika fani hiyo sambamba na mikakati liyojiwekea.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo Ikulu mjini Zanzibar, wakati alipokuwa na mazungumzo na Mkongwe wa
Filamu za Kihindi Kunal Kapoor aliyefuatana na Msimamizi wa Ofisi ya Utalii ya
Zanzibar Mumbai, India Jilesh Babla ambapo mkongwe huyo yupo Zanzibar akiwa
mgeni rasmi wa Tamasha la Kimataifa la Filamu la Zanzibar (ZIFF) mwaka huu.
Katika mazungumzo hayo
Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar tayari imeshachukua
juhudi za makusudi katika kuhakikisha azma hiyo inafanikiwa ikiwa ni pamoja na
kufanya marekebisho sheria inayohusiana na mambo ya filamu ili kuendana na Sera
ambayo inasimamia tasnia hiyo.
Kutokana na hatua hizo
Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar inaweza kufanikiwa kuwa kituo cha uigizaji filamu
kwa makampuni makubwa duniani ambayo yatakuja kutengeneza filamu zao jambo
ambalo litaweza kuwainua wasanii wa filamu wa hapa nchini pamoja na kuinua pato
la Taifa.
Aidha, Dk. Shein
alieleza historia ya Zanzibar katika tasnia ya filamu na maigizo tokea mnamo
miaka 1940 ambapo Zanzibar iliweza kutumika kama kituo cha uigizaji wa filamu
mbali mbali kutoka kwa makampuni makubwa duniani pamoja na kuwa na majumba ya
sinema na majukwaa na kumbi za maigizo hali ambayo Zanzibar inakusudia kuirejesha
hivi sasa.
Kwa upande wa Ofisi ya
Utalii ya Zanzibar iliyopo Mumbai nchini India, Dk. Shein alieleza kuvutiwa
kwake na juhudi za makusudi zilizochukuliwa na Ofisi hiyo katika kuitangaza
Zanzibar na kupelekea kuongezeka kwa idadi ya Watalii kutoka India.
Dk. Shein alisema kuwa
mafanikio zaidi yanaweza kupatikana baada ya juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar za kukamilisha ujenzi wa jengo jipya la abiria katika uwanja wa ndege
wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.
Nae Mkongwe wa Filamu
za Kihindi kutoka nchini India Kunal Kapoor, alieleza kuvutiwa kwake na mandhari
pamoja na ukarimu wa Wazanzibari kwa wageni na hivyo kueleza haja kwa makampuni
mbali mbali duniani kuja kutengeza filamu zao hapa Zanzibar zikiwemo Kampuni
kutoka India.
Alisema kuwa katika
kipindi kifupi alichofika Zanzibar ameweza kuona vipaji mbali mbali vya wasanii
ambavyo iwapo vitaendelezwa na kukuzwa vinaweza kuendelea kuijengea sifa
Zanzibar katika tasnia ya filamu na maigizo.
Pamoja na hayo,
Mkongwe huyo wa Filamu za Kihindi na mtayarishaji mahiri na maarufu wa filamu kutoka Bollywood nchini India, alisema
kuwa yupo tayari kutoa ushirikiano wake na kuunga mkono juhudi za Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza tasnia hiyo ya filamu na maigizo hapa
Zanzibar.
Alieleza kuwa kutokana
na uzoefu mkubwa alionao katika tasnia hiyo anamatumaini makubwa kuwa iwapo
mashirikiano ya pamoja kati yake na Taasisi husika yataimarishwa Zanzibar
inaweza kupiga hatua kubwa ikiwa ni pamoja na kujenga majukwa na kumbi za
maigizo ya filamu za kisasa.
Sambamba na hayo,
Kapoor ambaye ni mwongozaji na mtayarishaji wa filamu mashuhuri nchini India,
alimuhakikishia Dk. Shein kuwa ana uwezo mkubwa wa kuyashajiisha makampuni
kutoka nchini India kuja kutengeneza filamu zao hapa Zanzibar ikiwemo Kampuni
ya Bollywood. “Uwezekano mkubwa upo wa kuzishawishi kampuni za India kuja
kufanya filamu hapa Zanzibar kutokana na mandhari yake nzuri inayovutia”,alisema
Kapoor.
Nae Msimamizi wa Ofisi
ya Utalii ya Zanzibar iliyopo mjini Mumbai nchini India, Jilesh Babla
alimueleza Dk. Shein mikakati iliyowekwa na Ofisi hiyo katika kuitangaza
Zanzibar kiutalii pamoja na mafanikio ambayo imeshaanza kuyapata.
Kunal Kapoor ambaye
anatoka katika familia ya waigizaji na watengeneza filamu maarufu nchini India,
alikuwa mgeni rasmi katika Tamasha la ZIFF mwaka huu hapa Zanzibar ambalo
hufanyika kila mwaka na kuhudhuriwa na wageni mashuhuri, wasanii na wanamuziki
na wadau mbali mbali wa kazi za sanaa duniani.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address:
2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment