Habari za Punde

Tuwanyonyeshe watoto maziwa ya mama - Wito

Na  Khadija Khamis – Maelezo 

Mtaalamu wa kitengo cha lishe kutoka  Wizara ya Afya Zanzibar  Maryam Amir  amesema kunyonyesha mtoto  maziwa ya mama mara tu anapozaliwa  hadi kufikia miaka miwili humjenga  kukuwa  mwili  na  kiakili pamoja na kumuepushia utapiamlo na maradhi nyemelezi.

Aliyasema hayo leo  katika Shehia ya Muungano wakati akitoa elimu kwa  wananchi wa shehia hiyo katika siku ya kwanza ya wiki ya  unyonyeshaji wa maziwa ya mama kwa watoto wenye umri wa siku ziro hadi miaka miwili .

 Alisema kinga bora  kwa watoto ni maziwa ya mama katika kuwaepusha na maradhi mbali mbali iwapo wazazi watawanyonyesha watoto wao  kwa  mujibu inavyotakiwa .

“Kunyonyesha maziwa ya mama ni njia inayomsaidia mtoto kukua vizuri na kumuepushia   mzazi kupata ujauzito  katika  kipindi cha  miezi sita ya mwanzo,”alisema mtaalamu huyo .

Alifahamisha kuwa maziwa ya kifua  hupatikana muda wote na pahala popote na  ni safi na salama pia yanavirutubisho vya kutosha na joto linalohitajika kwa kumjenga  mtoto.

Aliongeza kuwa  maziwa ya mama hupunguza  vifo vya watoto kwa asilimia kubwa iwapo mtoto atanyonyeshwa maziwa pekee kwa miezi sita ya mwanzo

 Wiki ya unyonyeshaji huanzia wiki ya  kwanza ya mwezi wa nane kila mwaka  na tarehe nane huwa ni kilele cha siku hiyo na kaulimbiu ya   mwaka huu ni UNYONYESHAJI NA KAZI HAKIKISHA INAWEZEKANA .

Akizungumzia unyonyeshaji kwa akinamama wanaofanyakazi  ofisini, amewashauri  kukamua maziwa  katika chombo safi na kuyahifadhi katika jokofu na kupewa mtoto mara kwa mara kwani   yana uwezo  kukaa hadi   masaa manane bila kuharibika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.