Habari za Punde

Kaimu Katibu Mkuu UVCCM ashiriki mazishi ya Katibu wa UVCCM wilaya Ludewa Mkoa wa Njombe Ali Suleiman Nasir

Na Mwandishi Wetu.

Kaimu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Taifa (UVCCM) Shaka Hamdu Shaka (MNEC)  jana aliwaongoza   viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na jumuiya zake, wanachama na  wananchi mbali mbali wa Wilaya ya Masasi Mkoa wa Mtwara katika mazishi ya Katibu wa UVCCM wilaya Ludewa Mkoa wa Njombe Ali Suleiman  Nasir aliyezikwa  kijijini kwao   Masasi.

Marehemu amefariki dunia Juzi usiku nyumbani kwao Masasi baada ya kuugua kifua na pumu kwa zaidi ya wiki mbili ambako alikwenda  kwa mapumziko ya mwisho wa mwaka.

Akizungumza katika mazishi hayo Ndg: Kaimu Katibu Mkuu  Shaka alimtaja marehemu Ali Suleiman Nasir kama ni  kijana aliyekuwa mchapakakazi, aliyejituma kwa bidii, aliyekuwa tayari kukosolewa na kujirekebisha kila ilipobidi na hakuwa na nongwa.

"Tumempoteza mtendaji tuliyekuwa  tukimtegemea mno katika kupigania maslahi ya Chama Cha Mapinduzi na jumuiya yetu  mahali popote, huu ni msiba mzigo  uliogusa hisia zetu na kutuachia na  majonzi makubwa katika mioyo" Alisema kaimu Katibu Mkuu Shaka

Alimuelezea Marehemu  Nasir kuwa katika maisha yake kama mtendaji alikuwa tayari na mwepesi  kwa saa na wakati wowote kutii maelekezo toka  Makao  Makuu ikiwemo na kuridhia uhamisho toka mahali pamoja kwenda pengine kila ilipobidi na kusisitiza ingawaje pengo la Nasir linaweza kuzibika kwa vile ametii wito wa Mwenyezimungu lakini itachukua muda mwingi chama na jumuiya  kumpata mtu wa aina yake ambaye wakati wote alijali na kuthamini, kutimiza ahadi na maelekezo kwa ujasiri na ushupavu.

"Mwenzetu ameitwa na Mwenyezimngu ametangulia mbele ya haki, siku zake katika maisha ya dunia zimekwisha na hakuna mwenye uwezo wa kuzuia uamuzi wa Mwenyezimungu, marehemu alikuwa ni mtumishi wa CCM akitumikia jumuiya ya vijana hivyo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Ndugu Abdulrahman Omari Kinana  chama kinatoa pole kwenu nyote wafiwa na kuwaomba muwe na moyo wa subra, ustahamilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba, maombelezo na mtambue hili si lenu  peke yenu  sote tumeguswa na ndio maana tumekuja kuwakilisha, kuwafariji na kutoa mkono wa pole kwa niaba ya Chama Cha Mapinduzi na jumuiya ya Vijana" Alifahamisha Shaka*

Marehemu Ali Suleiman Nasir alizaliwa April 4 mwaka 1977 kijijini  kwao Masasi Mkoani Mtwara nakupata  elimu ya sekondari baadae chuo cha ufundi  aliteuliwa kuwa katibu wa UVCCM wilaya Tandahimba, baadae  alihamishiwa wilaya ya Nanyumbu Mkoani Mtwara, wilaya Lushoto mkoani Tanga, wilaya ya  Same mkoani kilimanjaro aidha katika maisha yake ya utumishi  ndani ya UVCCM aliwahi kuwa katibu  wilaya ya Uyui mkoa wa Tabora kabla ya kupelekwa Newala mkoani Mtwara na hadi mauti yanamfika alikuwa katibu wa vijana wilaya ya  Ludewa mkoa wa  Njombe.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.