Habari za Punde

Dk Shein Amesisitiza Kauli Yake ya Kuwataka Viongozi na Watendaji Sekta ya Umma Kuacha Kufanya Kazi kwa Mazoea.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                                     2.2.2017
RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza kauli yake ya kuwataka viongozi na watendaji katika sekta ya umma kuacha kufanya kazi kwa mazoea huku akieleza azma ya Serikali ya kuwaongeza mshahara wafanyakazi wa kima cha chini ifikapo Aprili mwaka huu kuwa iko pale pale.

Dk. Shein aliyasema hayo huko katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani, MnaziMmoja Mjini Zanzibar wakati akifunga Semina ya siku moja kwa Viongozi na Watendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Takwimu na Matumizi yake.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisisitiza haja kwa kila kiongozi kuhakikisha anasimamia vyema kazi zake pamoja na kuwasimamia anaowaongoza katika sehemu yake ya kazi pamoja na kufanya kazi kwa bidii na kuachana na kufanya kazi kwa mazoea.

Alisema kuwa ni jukumu la kila kiongozi kubadilika katika utendaji wake wa kazi na kuwataka wajitahidi kufanya hivyo licha ya kuwa itachukua muda lakini aliwasisitiza kuwa si busara kuendelea kufanya kazi kwa mazoea.

Dk. Shein alisema kuwa moja kati ya tamko la Ilani ya Chama cha ASP katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1963 ilikuwa ni kuwapa nafasi Waafrika wa Zanzibar kuongoza nchi yao na baada ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 chini ya uongozi wa Mzee Abeid Amani Karume hilo lilifanikiwa kwa kuanzia Wizara ya Afya na kuendelea kwa Wizara nyengine ambapo wananchi wa Zanzibar walipata fursa ya kufanya kazi.

Kutokana na mafanikio hayo, Dk. Shein alieleza kuwa ndani ya miaka 53 wananchi wa Zanzibar wamekuwa wakijiongoza wenyewe, hivyo ni vyema kwa kila mmoja ajisimamie mwenyewe sambamba na kuwasimamia walio chini yake ambapo katika suala la usimamizi limekuwa halifanywi vizuri hivyo, kuna kila sababu ya kulitilia mkazo jambo hilo.

“Tufanye kazi kwani hakuna wa kutusaidia wahisani watatusaidia pale tu tutakapohitaji msaada wao lakini suala la kufanya kazi ni letu wenyewe, hivyo tufanye kazi wala tusifanye kazi kwa mazoea’,alisisitiza Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza kuwa suala la umuhimu wa takwimu na matumizi yake ni jambo kubwa na kuanzia sasa Serikali itaweka mkazo mkubwa zaidi kwenye takwimu kutokana na muhimu wake katika maendeleo ya nchi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar imepiga hatua kubwa katika ukusanyaji wa mapato yake kwani tokea mwaka 2010 wakati alipoingia madarakani mapato yameongezeka kwa kiasi kikubwa takriban mara nne hivyo, hakuna kisingizio kwani Serikali iko vizuri na cha muhimu ni kufanya kazi.

Alisisitiza kuwa Serikali iko vizuri na tofauti na baadhi ya watu wanavyoizungumzia ambao hawana hoja za msingi na kueleza kuwa ahadi zote za Serikali zitatekelezwa kwa asilimia mia ikiwemo ya kuwaongezea mshahara wafanyakazi wa kima cha chini ifikapo Aprili mwaka huu sambamba na vikosi vya SMZ navyo kulingana na vikosi vyengine kimaslahi.

Nae Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd alisisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano katika utoaji wa takwimu na kuzitaka taasisi za umma na zile binafsi kushirikiana vyema na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali.

Balozi Seif alisema kuwa takwimu zina umuhimu mkubwa katika maendeleo ya nchi pamoja na wananchi wake na zimekuwa zikisaidia kwa kiasi kikubwa katika kufanya maamuzi, kuwahudumia wananchi pamoja na kuzisaidia Wizara katika kutekeleza mipango yake.

Waziri wa Fedha na Mipango Dk. Khalid Salum Mohammed nae alitumia fursa hiyo kueleza kuwa Wizara yake kupitia Ofisi ya Mtakwimu Mkuu itahakikisha kuwa Sheria ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali inatekelezwa vizuri na kupanga mpango madhubuti wa utekelezaji huku akiwataka viongozi kuwa wasimamizi wa utoaji wa takwimu sahihi.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Abdulhamid Yahya Mzee aliitaka Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali kuitumia vyema Sheria yake Namba 9 ya mwaka 2007 ambayo inaipa Ofisi hiyo mamlaka ya kuratibu na kusimamia masuala yote ya kitakwimu ambayo itatatua vyema changamoto zilizopo.

Nao Washiriki wa Semina hiyo wakitoa michango yao mbali mbali walisisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano baina ya taasisi zao na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ili kufikia lengo lililokusudiwa pamoja na kueleza umuhimu mkubwa wa kuwepo takwimu sahihi kwa maendeleo ya nchi.

Sambamba na hayo, Washiriki hao walieleza haja na umuhimu wa kuwajibika na kufanya kazi kwa bidii sambamba na kufuata na kuyafanyia kazi maagizo yote yanayotolewa na Rais wa Zanzibar katika kutekeleza wajibu wao wa kazi.

Pia, washiriki hao walieleza kuwa juhudi za makusudi zimekuwa zikichukuliwa na taasisi zao katika ukusanyaji wa takwimu na kufanyika kwa Semina hiyo itazidi kuwa chachu katika utekelezaji wa majukumu yao.

Hatimae Semina hiyo ilikuja na maazimio ambayo yalisomwa mbele ya washiriki wote kufuatia mada tano silizowasilishwa na wasilishaji mbali mbali kutoka Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali zenye maudhui tofauti ikiwemo mada ya Muhtasari wa majukumu ya Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali katika upatikanaji wa takwimu na matumizi yake.

Mada nyengine ilikuwa ni Umuhimu wa takwimu, hatua za uzalishaji na matumizi yake, Takwimu za sekta ya kilimo, Takwimu za sekta ya viwanda na Takwimu za sekta ya huduma.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.