Habari za Punde

NHIF Kuwafikia Wananchi Asilimia 85 ya Watanzania Ifikipo 2020.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Bw. Bernard Konga (wa pili kutoka kushoto)  akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)  kuhusu ongezeko la usajili wa vituo vya kutolea huduma kwa wanachama wa Mfuko. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Uhai wa Mfuko Bw. Baraka Maduhu.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Bw. Bernard Konga (kushoto)  akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)  kuhusu ushiriki wa Mfuko katika kupunguza magonjwa yasiyoambukiza  Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Masoko na Utafiti Bi. Angela Mziray.
 Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia maelezo ya Kaimu Mkurugenzi wa NHIF Bw. Bernard Konga (Picha na Frank Mvungi-Maelezo)

Na Grace Michael
MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umefanikiwa  kufikia makundi mbalimbali wakiwemo Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jijijini Dar es salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bw. Bernard Konga amesema kuwa mafanikio haya yamefikiwa chini ya Serikali ya Awamu ya Tano ambayo imejipanga kuhakikisha zaidi ya asimilia 85 ya Watanzania wanakuwa kwenye Mfumo wa Bima ya Afya ifikapo mwaka 2020.

“Sisi kama Mfuko tunajivunia sana kufikia makundi mengi ya wananchi na kuyahudumia hususan kundi la waheshimiwa wabunge ambao awali hawakuwemo lakini pia kundi la watoto ambalo nalo ni muhimu sana,” alisema Bw. Konga.

Alisema kuwa kitendo cha Wabunge kuwa ndani ya huduma za Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya utasaidia kwa kiasi kikubwa kwa kuwa wao ndio wawakilishi wa wananchi hivyo watasaidia kuwahamasisha wananchi kujiunga na Mfuko.

Bw. Konga alieleza kuwa pamoja na kuwepo kwa ongezeko la wanachama, Mfuko pia umeongeza usajili wa vituo vipya 92 na kufanya idadi ya vituo vinavyohudumia wanachama kuwa ni 6,998 hivyo kuwezesha kuwa na mtandao mpana wa huduma kwa wanachama wa NHIF.

Alitumia fursa hiyo pia kusema kuwa Mfuko umeshiriki kwa kiasi kikubwa kupunguza magonjwa hususan magonjwa yasiyoambukiza kutokana na kujikita katika utoaji wa elimu kwa wananchi ya namna ya kujikinga na magonjwa hayo lakini pia kuendesha zoezi la upimaji wa afyua bure katika maeneo mbalimbali vijijini.

“Tunao mpango wa elimu ya kata kwa kata ambapo kwa mwaka 2016 jumla ya kata 560 zilifikiwa na mpango huo hivyo sisi kama Mfuko tumetekeleza jukumu hili na tunaendelea kulifanya kupitia ofisi zetu za mikoani,” alisema.

Akizungumzia suala la uboreshaji wa miundombinu ya afya pamoja na ujenzi wa hospitali, Bw. Konga alisema kuwa, Mfuko umewekeza katika Vituo vya Kisasa vya uchunguzi wa magonjwa vilivyoko Dodoma na kutokana na uwekezaji huu umekwenda sambamba na mkakati wa Serikali wa Dodoma kuwa Makao Makuu ya nchi.

Alisema kuwa ujenzi wa Hospitali kubwa iliyopo Chuo Kikuu cha Dodoma inayojulikana kama Benjamin Mkapa imelenga kusaidia Serikali hasa katika kuondokana na gharama za kusafirisha wagonjwa nje ya nchi hivyo uwekezaji huo unayo manufaa makubwa kwa Watanzania kwa ujumla.

Aliwahakikishia wanachama wa Mfuko kuwa Mfuko uko imara na utawahudumia kwa kiwango kinachotakiwa kulingana na dhamana kubwa iliyopewa ya kutoa huduma za matibabu kwa wanachama wake.


“Mfuko uko imara kabisa, wanachama wajue hilo na sisi tunayo dhamana ya kulinda uhai wa Mfuko hivyo rai yetu ni kwa kila mwanachama ama Mtanzania kulinda huduma za Mfuko ili ziweze kutoka kwa walengwa na hatimaye kutimiza lengo lake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.