Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa
Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Bw. Bernard Konga (wa pili kutoka kushoto) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo
pichani) kuhusu ongezeko la usajili wa
vituo vya kutolea huduma kwa wanachama wa Mfuko. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa
Uhai wa Mfuko Bw. Baraka Maduhu.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa
Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Bw. Bernard Konga (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo
pichani) kuhusu ushiriki wa Mfuko katika
kupunguza magonjwa yasiyoambukiza Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Masoko na
Utafiti Bi. Angela Mziray.
Baadhi ya waandishi wa habari
wakifuatilia maelezo ya Kaimu Mkurugenzi wa NHIF Bw. Bernard Konga (Picha na Frank Mvungi-Maelezo)
Na Grace
Michael
MFUKO wa
Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umefanikiwa kufikia makundi mbalimbali wakiwemo Wabunge wa
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
Akizungumza
na waandishi wa habari leo Jijijini Dar es salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa
NHIF, Bw. Bernard Konga amesema kuwa mafanikio haya yamefikiwa chini ya
Serikali ya Awamu ya Tano ambayo imejipanga kuhakikisha zaidi ya asimilia 85 ya
Watanzania wanakuwa kwenye Mfumo wa Bima ya Afya ifikapo mwaka 2020.
“Sisi kama
Mfuko tunajivunia sana kufikia makundi mengi ya wananchi na kuyahudumia hususan
kundi la waheshimiwa wabunge ambao awali hawakuwemo lakini pia kundi la watoto
ambalo nalo ni muhimu sana,” alisema Bw. Konga.
Alisema kuwa
kitendo cha Wabunge kuwa ndani ya huduma za Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya
utasaidia kwa kiasi kikubwa kwa kuwa wao ndio wawakilishi wa wananchi hivyo
watasaidia kuwahamasisha wananchi kujiunga na Mfuko.
Bw. Konga
alieleza kuwa pamoja na kuwepo kwa ongezeko la wanachama, Mfuko pia umeongeza
usajili wa vituo vipya 92 na kufanya idadi ya vituo vinavyohudumia wanachama
kuwa ni 6,998 hivyo kuwezesha kuwa na mtandao mpana wa huduma kwa wanachama wa
NHIF.
Alitumia
fursa hiyo pia kusema kuwa Mfuko umeshiriki kwa kiasi kikubwa kupunguza
magonjwa hususan magonjwa yasiyoambukiza kutokana na kujikita katika utoaji wa
elimu kwa wananchi ya namna ya kujikinga na magonjwa hayo lakini pia kuendesha
zoezi la upimaji wa afyua bure katika maeneo mbalimbali vijijini.
“Tunao
mpango wa elimu ya kata kwa kata ambapo kwa mwaka 2016 jumla ya kata 560
zilifikiwa na mpango huo hivyo sisi kama Mfuko tumetekeleza jukumu hili na
tunaendelea kulifanya kupitia ofisi zetu za mikoani,” alisema.
Akizungumzia
suala la uboreshaji wa miundombinu ya afya pamoja na ujenzi wa hospitali, Bw.
Konga alisema kuwa, Mfuko umewekeza katika Vituo vya Kisasa vya uchunguzi wa
magonjwa vilivyoko Dodoma na kutokana na uwekezaji huu umekwenda sambamba na
mkakati wa Serikali wa Dodoma kuwa Makao Makuu ya nchi.
Alisema kuwa
ujenzi wa Hospitali kubwa iliyopo Chuo Kikuu cha Dodoma inayojulikana kama
Benjamin Mkapa imelenga kusaidia Serikali hasa katika kuondokana na gharama za
kusafirisha wagonjwa nje ya nchi hivyo uwekezaji huo unayo manufaa makubwa kwa
Watanzania kwa ujumla.
Aliwahakikishia
wanachama wa Mfuko kuwa Mfuko uko imara na utawahudumia kwa kiwango
kinachotakiwa kulingana na dhamana kubwa iliyopewa ya kutoa huduma za matibabu
kwa wanachama wake.
“Mfuko uko
imara kabisa, wanachama wajue hilo na sisi tunayo dhamana ya kulinda uhai wa
Mfuko hivyo rai yetu ni kwa kila mwanachama ama Mtanzania kulinda huduma za
Mfuko ili ziweze kutoka kwa walengwa na hatimaye kutimiza lengo lake.
No comments:
Post a Comment