Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk. Shein Akutana na Balozi wa Singapore Ikulu Zanzibar na Mabalozi wa Tanzania Nchi za Nje.


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                          03.03.2017
---
SINGAROPE imeahidi kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza sekta za maendeleo hasa katika sekta ya utalii, pamoja na vipaumbele vyengine vilivyowekwa na Serikali ili Zanzibar izidi kuimarika kiuchumi.

Balozi wa Singapore nchini Tanzania  Tan Puay Hiang aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungunmzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake, Balozi Hiang alimueleza Dk. Shein  kuwa Singapore inathamini sana juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo hivyo kuna kila sababu ya kuendelea kuziunga mkono hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar inalingana na Singapore kimazingira.

Balozi Hiang, alimuahidi Dk. Shein kuwa atakuwa Balozi mzuri wa kuitangaza Zanzibar katika sekta ya utalii nchini mwake hasa kwa vile Singapore imepiga hatua kubwa katika sekta hiyo huku akiendelea kuahidi kuwa atahakikisha mashirikiano ya karibu katika kuimarisha sekta hiyo kwa pande mbili hizo yanaimarika.

Aidha, Balozi Hiang alisema kuwa nchi yake pia, itazidisha uhusiano na ushirikiano katika sekta ya usafirishaji, uwekezaji, afya na biashara pamoja na kubadilishana utaalamu hasa katika sekta ya afya na kuahidi kusaidia vipaumbele vilivyowekwa na Zanzibar.

Aliongeza kuwa nchi yake inaona haja na umuhimu wa kuwepo kwa mashirikiano katika kubadilishana uzoefu na utaalamu kwa viongozi na wataalamu katika sekta ya afya na kuahidi kuwa Singapore italisiamaia hilo ili kukuza uhusiano mwema uliopo.

Sambamba na hayo, Balozi huyo alipongeza azma ya ujenzi wa Bandari mpya ya Mapigaduri unaofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kueleza kuwa hatua hiyo itazidisha ukuaji uchumi na maendeleo na kuahidi kutoa ushirikiano wake katika kufanikisha juhudi hizo hasa katika sekta hiyo ya miundombinu.

Nae Dk. Shein kwa upande wake alipongeza uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Singapore na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar kwa kipindi kirefu na kusisitiza kuwa Zanzibar itazidisha uhusiano na ushirikiano huo uliopo.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itautumia uzoefu wa Singapore katika kuimarisha sekta zake za maendeleo kutokana na nchi hiyo kupiga hatua kubwa katika uchumi wake ambao unatajika duniani.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikichukua juhudi za makusudi katika kuimarisha sekta zake za maendeleo hasa katika vipaumbele vilivyowekwa kwenye Dira ya 2020 na kuwepo kwa azma ya Singapore kuunga mkono vipaumbele hivyo kutazidisha kufikia malengo yaliowekwa.

Dk. Shein alieleza hatua zinazochukuliwa na serikali katika ujenzi wa Bandari mpya ya Mpigaduri pamoja na juhudi katika kuimarisha sekta ya utalii huku akisisitiza kuwa mafunzo na ubadilishanaji wa utaalamu na uzoefu kwa wataalamu na viongozi wa sekta ya afya ni jambo muhimu katika kuimarisha sekta hiyo.

Wakati huo huo, Dk. Shein amefanya mazungumzo na Mabalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walioteuliwa na kuapishwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli, mazungumzo yaliofanyika Ikulu mjini Zanzibar.

Miongoni mwa Mabalozi hao ni Balozi Pindi Chana anaekwenda nchini Kenya, Balozi Abdalla Kilima, anayekwenda nchini Oman, Balozi Joseph Sokoine anaekwenda Ubelgiji, Balozi Silima Kombo Haji anaekwenda Sudan, Balozi Fatma Rajab anaekwenda Qatar, Balozi Batilda Masuka anekwenda Jamhuri ya Korea na Balozi Grace Mgovano anekwenda nchini Uganda.

Akizungumzo na Mabalozi hao, Dk. Shein aliwapongeza kwa kupata uteuzi wao huo walioupata kutokana na sifa maalum walizonazo katika utendaji wao wa kazi na kujidhatiti kwenda kuutumikia huku akiwataka kutekeleza Diplomasia ya uchumi ambayo ndio mbinu kubwa kwa Tanzania ambayo itaongeza ari katika kufikia azma ya kuimarisha sekta ya viwanda.

Dk. Shein aliwasisitiza Mabalozi hao kutilia mkazo zaidi sekta za maendeleo kwa kuitangaza vyema Tanzania ikiwemo Zanzibar kutokana na sifa zake njema hasa katika sekta ya uwekezaji, utalii, uvuvi, viwanda, usafiri na usafirishaji, kilimo pamoja na mashirikiano ya vyuo vikuu  na hospitali kati ya nchi wanazokwenda kufanyakazi na  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Nao Mabalozi hao walimuhakikishia Dk. Shein kuwa watakuwa mabalozi wema wa Tanzania katika nchi wanazokwenda na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote waliyopewa na Rais Dk. Shein.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.