Habari za Punde

Chukuweni hatua msisubiri wafadhili kukiokoa Makoongwe


NA HAJI NASSOR, PEMBA

WANANCHI shehia ya kisiwa cha Makoongwe wilaya ya Mkoani kisiwani Pemba, wametakiwa wasisubiri wafadhili, juu ya suala la kukikoa, na mbadiliko makubwa ya tabia nchi yaliokikumba kisiwa hicho, na sasa wachukue hatua za haraka wenyewe.

Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa kitengo cha mabadiliko tabia nchi kisiwani Pemba, Ali Abdi Mohamed alipokuwa akifungua mkutano wa wazi kwa wananchi, wenye lengo la kuwahamasisha upandaji miti na uhifadhi wa mazingira, ili kupunguza kasi ya mabadiliko tabia nchi.

Alisema kisiwa cha Makoongwe, ni miongoni mwa visiwa vidogo vidogo ambavyo navyo, zimeshaanza kukumbwa na athari za mabadiliko tabia nchi, sasa lazima wananachi wenyewe wajipange haraka, badala ya kusubiri wafadhili.

Abdi alieleza kuwa, kukatazana kuchukua mchanga pembezoni mwa fukwe, kutokata miti ovyo, kuacha kuchimba mashimo kwenye mikoko ni miongoni mwa hatua, ambazo wananchi hao wa kisiwa cha Makoongwe wanaweza kuzichukua pasi na fedha za mfadhili.

“Kila anaekikumbuka kisiwa cha Makoongwe miaka 25 iliopita, sasa akipata kukitembelea miaka hii, anaweza kuona jinsi kisiwa hicho, kinavyomegwa na maji ya bahari, ndio maana tunahimizana tuchukue hatua sasa’’,alishuari.

Kuhusu kisiwa Panza, ambao wananchi wamepata mradi wa kupunguza kasi ya mabadiliko tabia nchi, ambao wanatarajia kupanda miti ya aina mbali mbali 400,000 amewataka wananchi kuitunza, ili isaidie na kisiwa chao.

Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Mazingira wilaya ya Mkoani, Rashid Abdalla Salum, alisema hali ya kisiwa cha Makoongwe, imeanza kutisha kutokana na kila eneo kuingia maji ya bahari.

“Kila eneo sasa lina mto wa maji ya bahari, lakini na sisi wananchi wa kisiwa hichi, tumekuwa hanasababisha kwa kuchimba mchanga kwenye mashamba ya wakulima na hata pembezoni mwa fukwe’’,alifafanua.

Mapema Katibu wa Jumuia ya Sanaa, Ealimu ya Ukimwi na Mazingira JSEUMA, Juma Ali Mati, alisema kupitia mradi wa Kupunguza kasi ya mabadiliko tabia nchi waliopata, wanakusudia kupanda miti kwenye hekta 200.

Aidha Mati alisema wananchi 110 wameshapewa taaluma ya kupambana na kasi ya mabadiliko tabia nchi, wakiwemo wa Kisiwapanza, Makoongwe, Michenzani, Chokochoko, Kangani, Mwambe na Mtambile.

Wananchi wa kisiwa hicho, wamepongeza hatua ya wao kukumbushwa wajibu wao kama wananchi, katika kupambana na kasi ya mabadiliko tabia nchi.

Ahmed Ali Siasa alisema awali walikuwa hawajui wao kama wananchi nafasi yao katika kupambana na kasi ya mabadiliko tabia nchi.

“Sasa baada ya elimu mliotupa na sisi wananchi tumeshajua wajibu wetu, lazima tuhamasishane maana athari zake humkumba kila mmoja”,alifafanua.


Jumuia ya sanaa, elimu ya ukimwi na mazingira JSEUMA ya kisiwa panza, imeshapanda miti kwenye maeneo ya Kitunga ndege, Maduuni ambapo wakulima 50 wamerejea tena kwenye bonde hilo, baada ya kukihama kutokana na kuvamiwa maji ya bahari.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.