Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia
wakati wa Uzinduzi wa Mwongozo kwa Wapelelezi na Waendesha Mashitaka wa Kesi za
Wanyamapori na Misitu kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere
jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Prof. Jumanne Maghembe akihutubia wakati wa uzinduzi wa mwongozo kwa wapelelezi na waendesha mashitaka wa kesi za wanyamapori na misitu.
Naibu
wa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhandisi Hamad Masauni akizungumza wakati wa uzinduzi wa mwongozo kwa wapelelezi na waendesha mashitaka wa kesi za wanyamapori na misitu uliofanyika jijini Dar es Salaam kwenye ukumbi wa kimataifa wa mikutano wa Mwalimu Julius Nyerere.
Muendesha
Mashtaka Mkuu wa Serikali Biswalo Mganga akizungumzia namna Mwongozo kwa Wapelelezi na Waendesha Mashitaka wa Kesi za Wanyapori utakavyoleta matokeo chanya.
Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akikata
utepe kuashiria Uzinduzi Kitabu cha Mwongozo kwa Wapelelezi na Waendesha
Mashitaka wa Kesi za Wanyamapori na Misitu kwenye ukumbi wa Mikutano wa
Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, wengine pichani ni Waziri wa
Maliasili na Utalii Mhe. Profesa Jumanne Maghembe (kulia),Mratibu Mkazi wa
Umoja wa Mataifa nchini Bw. Alvaro Rodrigues na kushoto ni Muendesha Mashtaka
Mkuu wa Serikali Biswalo Mganga na Naibu wa Waziri wa
Mambo ya Ndani ya Nchi Mhandisi Hamad Masauni
Sehemu ya waliohudhuria wa Uzinduzi Kitabu cha Mwongozo kwa Wapelelezi na Waendesha
Mashitaka wa Kesi za Wanyamapori na Misitu kwenye ukumbi wa Mikutano wa
Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam
Mratibu
Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Bw. Alvaro Rodrigues akizungumza wakati wa uzinduzi wa mwongozo kwa wapelelezi na waendesha mashtaka wa kesi za wanyamapori na misitu.
Makamu wa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan ametoa kauli hiyo
wakati anazindua mwongozo kwa wapelelezi na waendesha mashtaka wa kesi za
wanyamapori na misitu katika ukumbi wa Kimataifa wa Julius Jijini Dar es
Salaam.
Makamu wa Rais amesema mwongozo aliouzindua
utasaidia kwa kiwango kikubwa uboreshwaji wa upelelezi na uendeshaji wa kesi
zinazohusu wanyapori na misitu nchini.
“Uwepo wa mwongozo huu
ni dhahiri unategemewa kutoa matokeo chanya katika mapambano dhidi ya ujangili
na uhalifu misitu yetu” Amesisitiza Makamu wa Rais.
Makamu wa
Rais Mhe Samia Suluhu Hassan amesema kuwa anaimani mwongozo huo aliouzindua
utasaidia kukomesha vitendo uhalifu ambavyo vimekuwa vikilisababishia Serikali
hasara kubwa ikiwemo uharibifu wa rasilimali za taifa na kupoteza mapato ambayo
yangesaidia kuimarisha huduma za kijamii nchini.
Kuhusu sekta
ya utalii nchini, Makamu wa Rais amesema pamoja na sekta hiyo kuliingizia taifa
mapato mazuri lakini inasikitisha kuona kuwa uwepo wa wanyamapori ambao ndio
nguzo kuu ya sekta ya utalii unazidi kupungua kila kukicha hivyo kuwa tishio
kubwa kwa uchumi na nchi.
Amesema
vitendo vya ujangili vimeendelea kuangamiza wanyama hasa tembo hivyo ni muhimu
kwa wapelelezi na waendesha mashtaka kutenda haki bila kuonea mtu kwa watu
wanaokamatwa kufanya vitendo hivyo ili viweze kukomeshwa nchini.
“Wazee wetu walilinda
na kutunza rasilimali zetu kwa faida yetu nasi tuzitunze kwa ajili ya vizazi vijavyo” Ameeleza Makamu wa Rais
Kwa upande
wake, Waziri wa Maliasili na Utalii Profesa Jumanne Maghembe amemhakikishia
Makamu wa Rais kuwa kazi ya kupambana na ujangili na utoroshaji holela wa
wanyama na viumbe wengine itakuwa endelevu na wale wote watakaokamatwa watachukuliwa hatua kali za
kisheria ili kukomesha vitendo hivyo.
Waziri
Profesa Maghembe amemwomba Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini kuendesha oparesheni
ya maalum ya kukusanya silaha zote ambazo zimekuwa zikitumika kwenye ujangili
ili kuhakikisha wanyama hasa tembo wanakuwa salama kwenye maeneo ya Hifadhi za
Taifa nchini.
Naye,
Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali Biswalo Mganga amefafanua kuwa katika
kipindi cha mwaka 2014/2017 ofisi yake imewafikisha mahakamani washtakiwa
wakubwa wa ujangili ambao walikuhumiwa vifungo virefu na faini.
Amesema kuwa
washtakiwa 100 walihukumiwa kulipa faini ya zaidi ya shilingi bilioni 1.1 kwa
kujihusisha na nyara za Serikali kinyume na sheria na faini hizo zimehalipwa
Serikali.
Ameeleza
kuwa kati ya idadi hiyo watuhumiwa zaidi ya 80 walihukumiwa kifungo cha miaka
20 hadi 30 gerezani na faini ya zaidi ya shilingi milioni 164 ambazo bado
hazijalipwa Serikalini.
Mwendesha
Mashtaka Mkuu wa Serikali Biswalo Mganga amesema mafanikio hayo yote
yamechangiwa na usimamizi madhubuti wa kesi hizo kupitia dawati la wanyamapori
katika Divisheni ya Mashtaka pamoja na Mawakili wa Serikali katika Ofisi zote
za mikoani nchini.
Ameeleza
kuwa changamoto kubwa wanayokutana nayo kwenye kazi kwa sasa ni dhamana kwa
watuhumiwa wakubwa wa vitendo vya ujangili ambapo utafiti uliofanywa Mahakama
za mkoa wa Dar es salaam tu katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015 unaonyesha
kuwapo kwa jumla ya mashauri 13 yanayohusishwa na nyara za Serikali zenye
thamani ya zaidi ya shilingi milioni 800 zilizokamatwa ndani na nje ya nchi
ambapo watuhumiwa wake walipewa dhamana na kutoweka.
No comments:
Post a Comment