Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                              18.09.2017
---
SERIKALI ya Jamhuri ya Watu wa China imepongezwa kwa jitihada zake za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendelea kuwajengea uwezo wafanyakazi wa sekta ya umma kwa kuwapatia mafunzo ambayo huwasadia katika kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa zaidi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Haji Gavu  aliyasema hayo  leo Ikulu mjini Zanzibar katika mazungumzo kati yake na  Hung Yutong ambaye ni Makamo wa Rais wa Taasisi ya ‘China National Research Institute of Food Fermentation Industries’ kutoka nchini humo.

Katika mazungumzo hayo, Waziri Gavu alieleza kuwa Serikali ya China ina historia kubwa ya kuisaidia Zanzibar katika kuwajengea uwezo watendaji wake katika sekta mbali mbali za maendeleo na kwa hatua ya mara hii ya wakufunzi kutoka nchini humo kuja kuwapa mafunzo watendaji wanaotoa huduma za upishi na ukarimu kwa viongozi wa wakuu wa nchi pamoja na walimu kutoka Taaasisi ya Utalii iliyopo Maruhubi ni jambo la kupongezwa.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini sana juhudi hizo za Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China  ambazo zimekuwa zikitoa mchango mkubwa kwa watendaji wa serikali kupata kujifunza mambo mbali mbali ambapo baadae elimu yao wanayoipata huifanyia kazi na kuweza kuisaidia Serikali pamoja na kujiongezea ujuzi na maarifa wao wenyewe.

Waziri Gavu alitoa shukurani na pongezi kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa uongozi wa Taasisi hiyo ya China kwa kuwaleta wataalamu wake hapa nchini kwa lengo la kuja kutoa mafunzo hatua ambayo alisema itawawezesha watendaji walio wengi kupata fursa hiyo muhimu.

Akitoa shukurani maalum, Waziri Gavu alieleza kuwa hatua ya mafunzo hayo inatokana na juhudi za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein za kuimarisha uhusiano na ushirkikiano na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China katika kuhakikisha nchi hiyo inatoa mafunzo hayo kwa watendaji hao wa Serikali.

Alieleza kuwa ni matarajio yake na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jumla kuwa walengwa wa mafunzo hayo watayatumia vyema ili waweze kuongeza ujuzi katika shughuli zao za kazi sambamba na kuitumia vyema fursa hiyo waliyopewa na Rais ya kushiriki mafunzo hayo.

Aidha, Waziri Gavu alieleza matumaini yake kuwa mafunzo hayo hayatakuwa ya mwisho na badala yake yatakuwa ni mafunzo endelevu kwa wafanyakazi hao na wengineo.

Aliongeza kuwa kwa vile wakufunzi hao kutoka Chuo hicho kinachuhusiana na masuala la upishi na ukarimu wana uzoefu na utaalamu mkubwa katika kada hizo, hivyo watendaji hao wa Serikali watapata kujivunza na kujijengea uwezo mkubwa katika kazi zao.

Nae Makamo wa Rais wa Taasisi ya ‘China National Research Institute of Food Fermentation Industries’ kutoka nchini China Hung Yutong alieleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China inathamini uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu kati yake na Zanzibar.

Makamo huo wa Rais wa Chuo hicho cha ‘China National Research Institu of Food and Fermentation Industries’ alimueleza Waziri Gavu uzoefu walionao wataalamu wa chuo hicho katika masuala yanoyohusiana na mapishi pamoja na ukarimu.

Alieleza kuwa mafunzo hayo ni mashirikiano ya pamoja kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China ambayo yatatolewa na wakufunzi kutoka chuo hicho huku akieleza uzoefu wa chuo chake kutokana na China kuwa na mahitajio mengi ya kada hiyo.

Kiongozi huyo ambaye amefuatana na Mkurugenzi wa Chuo hicho Bi  Luo Yanqin alieleza kuwa ana matarajio makubwa kuwa wataalamu watakaotoa mafunzo hayo watatumia uzoefu walionao na kuweza kuwasaidia watendaji hao kuelewa mambo kadhaa ya kitaifa na kimataifa yanayohusiana na kada hizo za masuala ya upishi, uhudumu na mambo mengineyo ya ukarimu kwa wageni.

Alisisitiza kuwa suala la masomo katika kada hizo yana umuhimu mkubwa kwa watendaji hao wa Serikali hasa ikizingatiwa kuwa wakati uliopo mambo mengi yanaenda kwa njia za sayansi na teknolojia.

Aliongeza kuwa mafunzo hayo yatawasaidia watendaji hao katika kuendeleza shughuli zao za kazi pamoja na maeneo yao ya kijamii na hata katika kutekeleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya utalii.

Pamoja na hayo, Huang Yutong alieleza kuwa mafunzo hayo yatawasidia watendaji hao kupata kujifunza upishi wa vyakula mbali mbali vya kitaifa na kimataifa vikiwemo vyakula vya kichina huku akisisitiza haja ya kuendeleza mashirikiano zaidi ili utaalamu utakaopatikana uzidi kuleta tija kwa wafanyakazi na Taifa kwa jumla.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.