Habari za Punde

Japan Yaonesha Nia Kuijenga Dodoma Kwa Miundombinu ya Kisasa.

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (kushoto) akisalimiana na Mwakilishi Mkazi Mwandamizi wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan –JICA nchini Tanzania Bw. Toshio Nagase, alioambatana na Makamu wa Rais wa Shirika hilo Bw. Hiroshi Kato (katikati) walipowasili katika Ofisi za Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (wa pili kushoto) na  Makamu wa Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Hiroshi Kato (wa pili kulia) wakijadili masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania na Japan katika Nyanja mbalimbali ikiwemo miundombinu, nishati, kilimo na maji, walipokutana Jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Hiroshi Kato akizungumza kuhusu kuwepo kwa ushirikiano mzuri kati ya Tanzania na Japan katika suala la Maendeleo alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), Jijini Dar es Salaam.
Wajumbe walioambatana na Makamu wa Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Hiroshi Kato wakifuatiia kwa makini majadiliano kati ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (hayupo pichani) na mgeni wake ambaye ni Makamu wa Rais wa JICA Bw. Hiroshi Kato, Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (kushoto) akisisitiza jambo alipokutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) Bw. Hiroshi Kato (hayupo pichani) katika Ofisi za Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es Salaam.
Kamishna wa Kodi za Ndani wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Elijah Mwandumbya akizungumzia mabadiliko ya Sheria ya Kodi yaliyofanywa hivi karibuni ambayo yanalenga kutoa misamaha ya kodi yenye tija kwa umma wakati wa Mkutano kati ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) na  Makamu wa Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Hiroshi Kato (hawapo pichani), katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam.
Kamishina Msaidizi wa Sera wa Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Shogholo Msangi akielezea kuhusu masuala ya kodi katika maendeleo ya Taifa katika mkutano kati ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) na  Makamu wa Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Hiroshi Kato (hawapo pichani), katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), wa nne kushoto na Makamu wa Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Hiroshi Kato (wa tano kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango na Serikali ya Japan, katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango)


Na.Benny Mwaipaja, Dar es Salaam
SHIRIKA la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) limesema liko tayari kushirikiana na Serikali kujenga miundombinu ya kisasa ya usafiri, Nishati ya umeme, maji na usafi wa mazingira katika Makao Makuu ya nchi, Dodoma.

Ahadi hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Shirika hilo Bw. Hiroshi Kato wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, Jijini Dar es Salaam.

Bw. Kato alisema kuwa mradi mwingine wanaotaka kuutekeleza katika mji wa Dodoma ni udhibiti wa taka ngumu na kwamba wanachosubiri ni Serikali kuainisha maeneo ya vipaumbele vilivyoko katika mpango mji wa Dodoma.

Aidha Makamu huyo wa Rais wa JICA alisema kuwa Shirika lake litaendelea kusaidia eneo la kilimo hususan kilimo cha mpunga ili kuongeza thamani ya zao hilo na kuwakomboa wakulima.

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango amelishukuru Shirika hilo kwa kuonesha nia ya kusaidia ujenzi wa mji wa Dodoma ambao ndio Makao Makuu ya nchi.

Alisema kuwa mradi huo utasaidia kwa kiasi kikubwa kuupanga mji wa Dodoma mapema ili kuondoa changamoto za msongamano wa huduma za jamii kwenye eneo moja kama ilivyo Jijini Dar es Salaam.

“Pamoja na umuhimu wa miundombinu ya maji, umeme, usafiri wa mjini, lakini pia tunataka tujenge mapema njia za juu (ring roads) ili kudhibiti msongamano wa magari” alisema Dkt. Mpango.

Aliongeza kuwa mradi mwingine wa kipaumbele katika mji huo ni ujenzi wa uwanja wa ndege wa kimataifa katika eneo la Msalato, karibu kilometa 20 kutoka katikati ya mji huo ili kurahisisha usafiri kwa njia ya anga.

Tanzania ni miongoni mwa nchi za Afrika zinazopata ufadhili mkubwa wa miradi mbalimbali ya maendeleo kutoka Japan kupitia Shirika hilo la Kimataifa la Maendeleo (JICA).

Baadhi ya miradi hiyo ni ujenzi wa barabara ya juu (fly over) katika eneo la Tazara Jijini Dar es Salaam, upanuzi wa awamu ya kwanza ya barabara mpya ya Bagamoyo (Mwenge-Tegeta) na ufadhili mpya wa awamu ya pili ya ujenzi wa barabara hiyo kutoka Morocco hadi Mwenge.


Mazungumzo hayo yamehudhuriwa pia na Mwakilishi Mkazi Mwandamizi wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) nchini Tanzania Bw. Toshio Nagase, pamoja na Maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango na Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.