Hussein Makame - NEC
TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imejiridhisha kuwa
uamuzi wa kuvihamisha vituo 21 vya kupigia kura katika Kata ya Mbweni, jimbo la
Kawe katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, umezingatia Sheria na Kanuni
za Uchaguzi.
NEC imetoa msimamo huo, baada ya kupokea taarifa kutoka
kwa baadhi ya wananchi na vyama vya siasa wakilalamika kuwa tume ya uchaguzi imehamisha
vituo vinane (8) vya kupigia kura na kuvipeleka kwenye Kituo cha Polisi, hatua
waliyoeleza kuwa ni kuwanyima haki wapiga kura katika kutimiza haki ya msingi.
Malalamiko mengine yaliyoifikia NEC ni kwamba tume ilivihamisha
vituo vingine 15 kutoka maeneo ya awali na kuvipeleka maeneo mengine jambo ambalo
baadhi ya vyama havikukubaliana na maamuzi hayo.
Kutokana na malalamiko hayo, jana Jumanne Mkurugenzi
wa Uchaguzi wa NEC, Kailima Ramadhani akiambatana na watendaji wengine wa tume,
walitembelea maeneo hayo na kujiridhisha kuwa mabadiliiko ya vituo yaliyofanywa
na msimamizi wa uchaguzi yamekidhi matakwa ya kisheria.
“Nimefika hapa
jimbo la Kawe kata ya Mbweni, baada ya mwananchi mmoja kunitumia ujumbe
akiniambia kuwa kuna chama kimoja kinachoshiriki Uchaguzi Mdogo wa Madiwani wa
Kata ya Mbweni kinalalamika kwamba tume imehamisha vituo vya kupigia kura
kiholela,” alisema Ramadhani.
Mkurugenzi wa uchaguzi aliongeza kuwa, chama hicho
kimelalamika kuwa vituo hivyo vimepelekwa kwenye eneo la kituo cha Polisi, kwa
hiyo huenda wapigakura wakanyimwa haki yao ya kupiga kura.
Alisema alipowauliza watendaji wa Halmashauri ya
Manispaa ya Kinondoni, majibu yao hayakumridhisha ndipo alipoamua kufika eneo
la tukio.
“Kwanza wanalalamika kwamba vituo vilivyohamishwa ni 27,
lakini ukweli ni vituo 21, vituo hivyo vimehamishwa kwa mujibu wa Sheria kwa
sababu Novemba mosi 2017, Msimamizi wa
Uchaguzi ngazi ya Kata aliviita vyama vinne na kufanya mkutano na aliwaambia
tunavihamisha vituo hivyo kwa sababu mbalimbali.
“Sababu alizozitoa msimamizi wa uchaguzi ni kwamba vituo
vinane vilikuwa shule ya Sekondari New
Era na vituo saba7 vilikuwa jirani na nyumbani kwa mgombea ambaye ni Mwenyekiti
wa Serikali ya Mtaa na vituo sita vilikuwa kwenye eneo la Kanisa,” alifafanua
Ramadhani.
Alibainisha kuwa kifungu cha 20 (2) cha Kanuni za
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura za Mwaka 2015 na Kifungu cha 21
cha Kanuni za Uchaguzi Mkuu wa 2015, vinabainisha kuwa vituo vya kupigia kura
havipaswi kuwa kwenye maeneo ya watu binafsi, kwenye maeneo ya ibada na kwenye kambi
za jeshi.
Kutokana na msingi wa kanuni hizo, Ramadhani
alithibitisha kuwa uamuzi wa kuvihamisha vituo hivyo kwenye maeneo hayo ambao
umefanywa na msimamizi wa uchaguzi wa
jimbo la Kawe ulikuwa sahihi.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya
Kinondoni ambaye ndiye Msimamizi wa
Uchaguzi wa Jimbo la Kawe ilipo kata ya Mbweni, Aron Kagurumjuri alisema
malalamiko kuhusu kuhamishwa kwa vituo hivyo ulitolewa na chama kimoja kati ya
vyama vine ambavyo vitashiriki kwenye uchaguzi mdogo wa diwani wa kata ya
Mbweni.
Uchaguzi mdogo wa kata hiyo unafanyika baada ya mahakama
kutengua uchaguzi wa awali kutokana na ukiukwaji wa baadhi ya taratibu za
Uchaguzi.
“Tuko hapa kwa sababu chama kimoja kati ya vyama vinne
vinavyoshiriki Uchaguzi huu mdogo, kulalamika kwamba tumehamisha vituo na
kuvipelekea kwenye maeneo ambayo sio rafiki kwa wapiga kura,” alisema Kagurumjuri.
Alifafanua kuwa hali halisi inaonesha kwamba kanuni na taratibu za kupigia kura, haziruhusu kuweka
kituo kwenye jengo la mtu binafsi na shule hiyo ambako kulikuwa na vituo kadhaa
ni shule ya mtu binafsi.
“Kwa hiyo kwa Uchaguzi huo wa mwAkaa 2015 kanuni hizo
zilikiukwa sasa kwa uchaguzi huu kwa sababu tunataka tufanye Uchaguzi kwa
kufuata kanuni na sheria za uchaguzi hatukutaka kuingia kwenye uvunjaji wa
kanuni na taratibu,”
“Baada ya kuhamisha vituo na kuvipeleka eneo hilo,
ikazua sintofahamu kwa chama kimoja kati ya vyama vitatu vilivyoridhia ambapo
tulikuwa na mashaka inawezekana kilifaidika na vituo kuwepo maeneo hayo,”
alisema.
Ramadhani alisema vituo vingine vimehamishiwa kwenye eneo
la wazi na lenye usalama zaidi kwa wapiga kura pamoja na vitu vingine, na
kwamba wanaona halina shida.
No comments:
Post a Comment