Kamishna wa wa Idara ya
Uhamiaji Zanzibar, Johari Masoud Sururu, amewapongeza watendaji wa Ofisi ya
Uhamiaji Mkoa wa Kaskazini Unguja, kwa kusogeza huduma za Uhamiaji karibu na
Jamii inayowazunguka. Alitoa pongezi hizo leo alipotembelea Vituo Maalum
“Detached Points” vilivyopo ndani ya maeneo ya Kendwa na Nungwi, Shehia za
Nungwi - Banda Kuu, Mnarani na Kiungani, Wilaya ya Kaskazini “A” na Fukwe za Kiwengwa,
Pongwe na Pwani mchangani, Shehia za Kiwengwa, Moga na Pongwe kwa Wilaya ya
Kaskazini “B” alipofanya ziara ya kikazi katika Wilayani hizo tarehe 05 – 06
Disemba, 2017.
Mkoa wa Kaskazini Unguja ni
kitovu cha shughuli za Biashara na Uwekezaji katika sekta ya Utalii, hali
inayosababisha kuwavuta wageni wengi kutoka Mataifa mbali mbali Duniani
kutembelea maeneo hayo kwa madhumuni tofauti. “katika Mkoa huu Idara yetu ina
kazi kubwa ya kuhudumia wageni wanaoingia na kuishi ndani ya Mkoa huu, kwani ni
Mkoa ambao huwavuta wageni wanaokuja kutembea na kupumzika kwenye fukwe
nadhifu, kuna wanaokuja kwa kuwekeza na wale wanaokuja kufanyakazi na biashara
mbali mbali za
Utalii, hali ambayo huibua
changamoto nyingi za Kiuhamiaji” alisema Kamishna Sururu.
Kutokana na muingiliano huo
wa wageni wa makundi tofauti, Idara ya Uhamiaji yenye dhamana ya kuhakikisha
wageni wote wanaoingia na kuishi nchini wanafanya hivyo kwa mujibu wa Sheria,
Kanuni na Taratibu za Uhamiaji, ina mchango mkubwa katika kuimarisha Ulinzi,
Uchumi na Utamaduni wa watu wa Zanzibar. Kuanzishwa kwa Vituo maalum kwenye
maeneo hayo ni mapinduzi makubwa katika Udhibiti na Usimamizi wa wageni
wanaoingia na kuishi Zanzibar kinyume cha Sheria.
“Kwa kweli Nimefarijika
sana kuona jinsi mlivyojipanga kuweza kuyafikia maeneo yote yenye changamoto za
uwepo wa baadhi ya wageni wanaojipenyeza na kuishi nchini bila ya Kufuata
Sheria za Uhamiaji. Uwepo wa Vituo hivi naamini ni muarobaini wa kuondoa kabisa
tatizo la Uhamiaji haramu” Alisema Kamishna Sururu na kuongeza
“Hatuzuwii
wageni kuja kutembea, hatuzuwii wageni kufanyakazi ama kuwekeza nchini kwetu
bali tunataka wageni wote waingie na kuishi nchini kwa kuheshimu Sheria za Nchi
yetu, kwa kufanya hivyo tutaweza kufikia ile adhma njema ya serikali kufungua
milango ya Biashara na Uwekezaji katika sekta ya Utalii kwa manufaa makubwa
bila ya kuathiri Jamii na Tamaduni zetu”.
Aidha, Kamishna Sururu
aliwahakikishia Masheha wa maeneo hayo kuwa Idara ya Uhamiaji itaendelea
kushirikiana nao kwa vitendo hususan katika kupiga vita Uhalifu wa aina zote
ukiwemo Udhalilishaji, Uuzaji na Usafirishaji wa Madawa ya Kulevya unaofanywa
na baadhi ya wageni hapa Zanzibar.
Kufuatia kauli hiyo, Sheha
wa Shehia ya Nungwi - Banda Kuu, Bw. Mohamed Khamis Haji alisema “Nashukuru
sana kwa ujio wako na hasa msimamo ulioutoa juu ya kuwachukulia hatua stahiki
wageni wanaojihusisha na vitendo vya Uhalifu hapa Nungwi. Hichi ni kilio chetu
cha siku nyingi. Nasi tunaahidi tutaendelea kutoa ushirikiano unaostahiki kwa
Askari wa Uhamiaji ili Shehia zetu ziendelee kupokea wageni wenye manufaa kwa
Jamii zetu na si vinginevyo”.
Kwa upande wake, Afisa
Uhamiaji Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mrakibu Mwandamizi wa Uhamiaji, Muhsin A.
Abdullah alifafanua, lengo kubwa la kuanzisha kwa vituo hivyo maalum vilivyopo
maeneo ya Nungwi na Kiwengwa Wilaya ya Kaskazini “A” na“B” ni mkakati mmojawapo
katika kuimarisha Doria na Misako ili kuwabaini wahamiaji wasiofata sheria.
“Mkoa huu tumekuwa
tukilalamikiwa sana kwamba wageni wengi huzagaa na kufanyakazi kiholela hususan
kutoka Mataifa ya Afrika Mashariki, kumepelekea tusogee karibu tuweze
kushirikiana na watendaji wenzetu wakiwemo Masheha na Wananchi, hatua ambayo
imeanza kuzaa matunda. Tumeongeza wigo wa kuelimishana, kujenga mashirikiano na
kupeana taarifa mbali mbali ambazo husaidia sana utekelezaji wa majukumu yetu”
alisema Mrakibu Mwandamizi Muhsin.
Kwa upande wake Sheha wa
Shehia ya Kiwengwa Bw. Maulid Masoud Ame katika ziara hiyo aliapata fursa ya
kuchangia ambapo alisema “Idara ya Uhamiaji inatusaidia sana katika suala zima
la kuwatambua nani Raia wa Tanzania na nani mgeni. Maana katika maeneo yetu
tuna changamoto kubwa sana ya kuwepo kwa vitendo vya ukiukwaji wa maadili na
udhalilishaji vinavyofanywa na watu mbali mbali wakiwemo wageni. Hivyo kwa
ushirikiano mkubwa tunaopata kutoka kwa Askari wa Uhamiaji unatusaidia sana
kufikia maamuzi.
Tumekuwa tukipokea malalamiko hayo kwa mfano yakihusisha jamii
za Kimasai wanaofanyakazi katika mahoteli mbalimbali hapa Kiwengwa, ambao
baadhi yao ni wamasai kutoka Kenya, ambapo sisi tunaona hao wote ni Watanzania
wenzetu. Askari wa Uhamiaji kwa utaalamu na weledi walionao hutusaidia katika
kuwatambua” alisisitiza Sheha Ame.
Akihitimisha ziara yake
kwenye Wilaya mbili hizo, Kamishna Sururu, alitembelea Bandari ya Mkokotoni
kujionea changamoto mbali mbali zikiwemo, vipenyo vinavyotumiwa na wahamiaji
wasiotaka kufuata Sheria na uwepo wa baadhi ya Manahodha wa vyombo vya usafiri
wanaotumia Bandari hiyo, kutoshusha Abiria kwenye eneo lililotengwa.
Aidha, alitumia fursa hiyo
kuwasisitiza Askari wa Uhamiaji Wilayani humo, kusimamia vyema majukumu yao kwa
mujibu ya Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo. “Nawasihi na kuwataka muelewe
kuwa sisi tumepewa dhamana na Serikali kuwatumikia wananchi, hivyo nidhamu na
heshima ya kazi ndio msingi wa mafanikio katika utekelezaji wa majukumu yetu”. Alimalizia Kamishna Sururu.
Imetolewa na:
KITENGO
CHA UHUSIANO, AFISI KUU YA UHAMIAJI ZANZIBAR.
No comments:
Post a Comment