Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Atembelea Studio za ZBC Rahaleo Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Sheina, akizungumza wakati wa ziara yake alipotembelea Jengo la ZBC Redio Rahaleo Zanzibar kuangalia ujenzi wa Studio. za kutangazia. kushoto Katibu Mkuu Kiongozi Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee, Waziri wa Habari Utalii Utamaduni na Michezo Mhe Rashid Ali Juma na kulia Mkurugenzi Mkuu wa Shrika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) Aiman Duwe.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo amezitembelea studio za ZBC Redio zilizopo Rahaleo na kusisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha studio hizo pamoja na jengo lake vyote vinaimarishwa kama ilivyofanywa kwa ZBC Televisheni.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ziara yake aliyoifanya ya kuzitembelea studio za ZBC Redio zilizopo Rahaleo mjini Zanzibar huku akisisitiza azma ya Serikali ya kuhakikisha studio zote za ZBC zinakuwa za kisasa na zinakwenda na wakati uliopo.

Katika ziara yake hiyo, viongozi wa mbali mbali walishiriki akiwemo Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Rashid Ali Juma ambaye kwa upande wake alieleza kufarajika kwake na ziara hiyo ya Dk. Shein pamoja na kueleza hatua za ukarabati zilizofikiwa ambapo pia, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mahmoud pamoja na Mshauri wa Waziri wa Wizara hiyo Abdalla Mwinyi Khamis na Katibu Mkuu Omar Hassan walishiriki.

Rais Dk. Shein alizitembelea studio zote nne za ZBC Redio zikiwemo zile zilizofanyiwa ukarabati mkubwa pamoja na zile zinazohitajia ukarabati huku akipata fursa ya kukitembelea chumba cha habari na kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa ZBC Redio na muhariri Mkuu wa chumba cha Habari Bi Lulu Mzee pamoja na kuzitembelea sehemu nyengine muhimu za ZBC Redio.

Katika ziara yake hiyo Dk. Shein alizitembelea  studio nne pamoja na studio kubwa na ile ya VIP ambazo hizo bado hazijafanyiwa matengenezo na kupata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa ZBC Aiman Duwe pamoja na Mkuu wa Utangazaji Suzan Kunambi  ambao walieleza hatua kubwa iliyofikiwa katika ukarabati huo mkubwa.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza hatua za haraka ambazo zitachukuliwa  na Serikali katika kuhakikisha changamoto ya usafiri inapatiwa ufumbuzi ili shughuli zote za uendeshaji katika kituo hicho na upatikanaji habari unafanyika kwa ufanisi mzuri zaidi.

Dk. Shein alisisitiza agizo lake la kuwepo kwa watangazaji maalum kwa kutangazia mambo maalum zikiwemo taarifa maalum za Serikali, za kiuchumi, kijamii, za kisiasa pamoja na matukio muhimu ya nchi kama ilivyokwa vyombo vya habari ya Kimataifa kama vile BBC.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza haja ya kuwa na taarifa za habari ambazo zinafanana kati ya ZBC Redio na ZBC Televisheni hasa kwa kuzingatia kuwa Shirika hilo ni moja na watendaji wake ni wale wale hatua ambayo itapendeza na itatoa habari vyema kwa wananchi.

Nao uongozi wa ZBC ulitoa pongezi na shukurani zake kwa Rais Dk. Shein kwa ziara yake hiyo ya kuwatembelea na kuona hatua waliyofikia katika baadhi ya matengenezo yaliyofanywa  kwenye studio hizo za ZBC Redio.

Pamoja na hayo uongozi huo wa ZBC Redio ulieleza changamoto waliyonayo ya usafiri katika kufanya shughuli zao za kila siku huku fundi mitambo wa ZBC Redio Lazaro Joseph akieleza haja ya kuwepo mashine za kisasa za kuhifadhia kumbukumbu za vipindi mbali mbali studioni hapo “Saver”.

Aidha, fundi huyo mitambo alieleza hatua zilizoanza kuchukuliwa hivi sasa katika kuviweka vipindi mbali mbali vya redio, hotuba pamoja na nyimbo kwenye mashine za kuhifadhia kumbukumbu “ Saver” ili ziweze kudumu kwa muda mrefu pamoja na kuwa salama.

Katika maelezo yao walieleza kufarajika na hali iliyopo hivi sasa katika studio hizo ikilinganishwa na hapo kabla wakati Rais Dk. Shein alipozitembelea studio hizo mnamo tarehe 19 mwezi Septemba mwaka 2016 ambapo hazikuwa katika hali ya kuridhisha.

Uongozi huo pia, ulieleza kuwa tayari agizo la Rais Dk. Shein la kuwepo kwa watangazaji maalum wa kutangaza habari maalum wamelifanyia kazi ambapo kwa upande wa ZBC Redio ni Fatma Said Ali na Salum Othman ambapo kwa upande wa ZBC Televisheni ni Mwanajuma Kassim na Ussi Mussa.

Aidha, uongozi huo ulieleza kuwa tayari wameshaanzisha utaratibu wa kubadilishana kwa watangazaji, waandishi na watendaji wengine kati ya ZBC Redio na ZBC Televisheni ili waweze kufanya kazi kwa mashirikiano na ukaribu zaidi katika kuiendesha taasisi hiyo ambayo imeamua kufanya mabadiliko makubwa.

Kwa upande wa “Transmitter”, tayari nne zimeshanunuliwa na zimeshafungwa na zikiwa tayari zinatumika ambapo ushahidi wa hayo yote ni kutokana na hivi sasa Mikoa yote ya Zanzibar na Pwani ya Afrika Mashariki pamoja na ulimwenguni kote wanapata matangazo ya ZBC Redio kwa uhakika kupitia 90.5,97.7,94.7.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.