Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shei, akimsikiliza Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Ardhi Zanzibar Ahmeid Rashid, akitowa maelezo ya eneo linalotarajiwa kujengwa Matenki ya Kuhifadhia Mafuta na Gesi Asilia katika eneo la Mangapwani Wilaya ya Kaskazini B Unguja alipotembelea eneo hilo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein leo amefanya ziara ya kutembelea eneo lililotengwa kwa ajili
ya Mradi wa kuhifadhi mafuta na gesi asilia pamoja na ujenzi wa bandari kwa
ajili ya kusafirishia na kuingiza rasilimali hizo.
Akiwa katika eneo hilo
lililoko Mangapwani-Bumbwini lenye
ukubwa wa hekta 399.25 sawa na hekari 986.5, Rais Dk. Shein aliyeongozana na
viongozi mbali mbali wa Serikali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali
Idd, Mawaziri na viongozi wengine wa Serikali, wakiwemo wajumbe wa Baraza la
Mapinduzi, alipata maelezo kuhusu hatua zinazoendelea katika mradi huo.
Kwa maelezo ya Katibu
wa Kamisheni ya Ardhi Ahmed Abdulrahman Rashid alimueleza Dk. Shein kuwa eneo
hilo lenye ukubwa wa hekta hizo tayari limetengwa kwa ajili ya shughuli zote za
mafuta na gesi asilia, bandari pamoja na bohari kuu ya Serikali ya kuhifadhia
mafuta.
Aidha, alimueleza Rais
Dk. Shein kuwa azma ya mradi huo ni kwamba baada ya kukamilika shughuli zote za
mafuta zinazofanywa katika bohari ya Mtoni zitahamishwa na kuhamia katika eneo
hilo maalum lililolengwa na Serikali.
Kwa mujibu wa maelezo
ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Ali Halil Mirza, hatua
inayoendelea hivi sasa ni kufanywa kwa uchambuzi yakinifu unaotekelezwa na Benki ya Dunia ambao utakamilika kwa muda wa miezi sita
ijayo.
Mirza alieleza kuwa kukamilika
kwa uchambuzi huo yakinifu ndio utaleta mapendekezo ya kulisanifu eneo hilo kwa
ajili ya bandari na majengo mengine ya utawala na shughuli nyengine zinazoenda
sambamba na mradi huo.
Kwa mujibu wa maelezo
ya viongozi wa Wizara hiyo, miongoni mwa sababu ya kutengwa eneo hilo kwa
shughuli hizo ni kutokana na kuwa na kina kirefu cha maji ya bahari ambacho
kitarahisisha kujengwa kwa bandari hiyo muhimu ambayo itatumika kwa ajili ya
kusafirishia gesi asilia na mafuta ndani na nje ya nchi.
Uongozi wa Wizara hiyo,
ulieleza kuwa miongoni mwa faida kubwa za mradi huo mara baada ya kukamilika
kwake ni pamoja na kuondoa kabisa uhaba wa mafuta hapa nchini sambamba na
kuweza kuuza hata nje ya nchi na kuipatia Serikali pato kubwa.
Sambamba na hayo,
uongozi huo wa Wizara hiyo ulieleza kuwa Mradi huo ambao utakuwa na bandari,
matangi ya mafuta kwa kuwa na sehemu ya bohari ya Taifa ya kuhifadhia gesi
asilia na mafuta ni hatua za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuimarisha
sekta ya nishati hapa nchini.
Wakati huo huo, Dk.
Shein akiwa na ujumbe wake alipata fursa ya
kulikagua eneo la Kampuni ya Salama International Trading Co Ltd, linalojengwa maalum kwa ajili ya
kusafisha mafuta na kupata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Kampuni hiyo
Abdallah Said Abdallah na kumueleza hatua zilizofikiwa na Kampuni yake katika
ujenzi huo.
Kwa maelezo ya
Mkurugenzi huyo, alisema kuwa eneo hilo ambalo ni kwa ajili ya kusafisha mafuta
ambalo limefikia asilimia 65 za ujenzi, lina lengo la kujenga jeti kwa ajili ya
kushushia mafuta na kutia kwenye matangi yaliopo katika eneo hilo.
Mkurugenzi huyo
alieleza kuwa Matenki tani elfu 18, sawa na lita milioni 24 ambayo yanaweza
kuhifadhiwa kwa wakati mmoja, huku
akieleza aina za mafuta yatakayohifadhiwa katika matenki hayo yakiwemo mafuta
ya diseli, petroli na mafuta ya taa pamoja na mafuta ya kulainisha mitambo
huku.
Uongozi huo ulieleza
kuwa tayari wanabaraka zote kutoka Serikalini ikiwemo kutoka kwa Mamlaka ya
Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA), na kutoa shukurani kwa Serikali kupitia Idara
zake zote ikiwemo Mazingira, Ardhi pamoja na (ZIPA) na kutoa shukurani kwa Rais
Dk. Shein kwa ziara yake hiyo.
Walieleza kuwa kuanzia
Februari mwaka huu wataendelea na shughuli za ujenzi zilizobaki shughuli ambazo
ziliaza mwaka 2015 kwa awamu tatu ambapo hadi walipofikia washatumia dola
milioni 5 kwa awamu ya kwanza na kueleza kuwa watazalisha tani 600 ambazo
zitawasidia Wazanzibari wenyewe kwa asilimia 70 na asiliamia zilizobaki watauza
nje ya nchi.
Walieleza kuwa Watu wa
Bandari, Uhamiaji na Idara zote muhimu zitakuwepo katika eneo hilo ambalo
tayari wameshaanza ujenzi wa jengo maalum kwa wahusika hao.
Akiwa katika eneo hilo,
Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya uhifadhi wa mazingira katika mchakato wa
usafishaji wa mafuta mara utakapokamilika mradi huo ambapo Mkurugenzi wa
Kampuni hiyo alimtoa wasi wasi na kumueleza kuwa aina ya mafuta wanayokusudia
kusafisha haitakuwa na athari zitakazopelekea uharibifu wa mazingira kutokana
na aina hiyo ya mafuta ambayo watachukua kutoa nchini Oman na Iran.
Pia, Dk. Shein alitembelea
eneo la Kampuni ya Turkey Petrolium (TP), ambalo limetengwa kwa ajili ya gesi
na mafuta ambapo uongozi wa Kampuni hiyo chini ya kiongozi wake Taufiq Salim
Turkey ulieleza kuwa juhudi za makusudi wanazichukuwa katika kuhakikisha Zanzibar
inafaidika kwa gesi mara baada ya kujengwa kwa Chelezo ambapo meli maalum zitaleta
gesi moja kwa moja kuanzia mwezi wa sita hapa Zanzibar.
Aidha, uongozi huo ulieleza
azma ya kujenga jengo maalum ambalo litasaidia kwa ajili ya kuwaweka
wafanyakazi wa Kampuni yao pamoja na Idara nyengine muhimu zinazohusiana na
shughuli hizo zikiwemo Uhamiaji na nyenginezo.
Pamoja na hayo,
uongozi huo uliiomba Serikali kuwezesha azma yao hiyo kutokana na baadhi ya changamoto
zilizopo hivi sasa ikiwemo uhaba wa gesi mara kwa mara kutokana na sehemu
wanayochukulia gesi hiyo.
Uongozi wa Kampuni
hiyo ya Turkey Petrolium (TP), ulieleza kuwa mashirikiano mazuri yamekuwepo kati
yao na Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA), Mamlaka ya Udhibiti
wa Huduma ya Maji na Nishati Zanzibar (ZURA), Wizara ya Fedha na Mipango,
Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Wizara ya Biashara.
Aidha, uongozi huo
ulieleza kuwa wanunuzi wakuu wa gesi katika Kampuni yao hiyo kwa hivi sasa ni wananchi
pamoja na hoteli huku uongozi huo ukisisitiza kuwa kuwepo kwa chelezo kwa ajili
ya kuingizia meli ambazo zitaleta gesi moja kwa moja kutawarahisishia zaidi
uendeshaji wa mradi wao huo.
Nae Mkurugenzi wa
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma ya Maji na Nishati Zanzibar (ZURA), Haji Kali
Haji alieleza mashirikiano yaliopo kati ya Mamlaka yake pamoja na Kampuni hiyo
ambapo mapema alieleza mashirikiano na hatua zinazochukuliwa katika kuhakikisha
eneo maalum lilotengwa na Serikali kwa ajili ya shughuli za mafuta na gesi
asilia linafikia na malengo yaliokusudiwa na Serikali.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment