Habari za Punde

KAMISHANA MPYA WA POLISI ZANZIBAR AJITAMBULISHA KWA RAIS

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti  wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia)akisalimiana na Kamishna Mpya wa Jeshi la Polisi Zanzibar Bw.Mohamed Haji Hassan alipofika Ikulu Mjini Zanzibar kujitambulisha baada ya uteuzi wake na dhamana alizopewa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti  wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na Kamishna Mpya wa Jeshi la Polisi Zanzibar Bw.Mohamed Haji Hassan alipofika Ikulu Mjini Zanzibar kujitambulisha baada ya uteuzi wake na dhamana alizopewa.[Picha na Ikulu.]

RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja kwa Jeshi la Polisi kuendelea kufanya kazi zake vyema  hapa Zanzibar ili kuimarisha amani na utulivu iliyopo hasa ikizingatiwa kuwa uchumi wa Zanzibar unategemea Utalii ambao unahitaji kuwepo kwa usalama ambao ndio kivutio kikubwa cha watalii.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mohamed Haji Hassan aliyefika Ikulu kwa ajili ya kujitambulisha kwa Rais ambapo Dk. Shein katika mazungumzo hayo alimuahidi kumpa mashirikiano makubwa Kamishna huyo.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alimueleza Kamishna huyo mpya kuwa uchumi wa Zanzibar unategemea kwa kiasi kikubwa utalii, hivyo ni vyema usalama ukaimarishwa, ili sifa ya Zanzibar ikiunganishwa na vivutio vilivyopo izidi kuimarika na kuendelea kuwavutia watalii kutoka pande zote za duniani.

Alieleza kuwa mapato ya Zanzibar yamezidi kuongezeka sambamba na Pato la Taifa kutokana na kuongezeka kwa watalii kila uchao na kupelekea kukua kwa uchumi wa Zanzibar, ambapo hiyo yote inatokana na kuwepo kwa usalama mkubwa kwa wananchi na wageni wanaokuja kuitembelea Zanzibar.

Hivyo, Dk. Shein alisisitiza haja ya Jeshi hilo kuendeleza doria katika maeneo yote hapa nchini hasa katika ukanda wa hoteli za kitalii sambamba na kuhakikisha watalii hawabughudhiwi na badala yake wanapata huduma zote za kitalii zilizo nzuri na zenye usalama.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Kamishna huyo mpya wa Polisi Zanzibar haja ya kushirikiana vyema na jamii katika kupiga vita suala la udhalilishji wa kijinsia kwa akina mama na watoto hasa ikizingatiwa kuwa Jeshi hilo ndio linaloshughulikia mashauri ya matukio hayo.

Aliongeza kuwa katika kipindi cha hivi karibuni mabadiliko makubwa yametokea katika kupiga vita vitendo hivyo, baada ya kuundwa Kikosi Kazi ambacho kinafanya kazi vizuri sambamba na kuwepo kwa Mahakama ya Watoto huku akimueleza hatua zilizofikiwa na Serikali katika Sheria ya Udhalilishaji  iliyopitishwa na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar hivi karibuni.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Kiongozi huyo haja ya kuwepo kwa mashirikiano katika kupambana na rushwa hapa Zanzibar na kumueleza hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kupambana na suala hilo ikiwemo kutunga Sheria na Sera yake pamoja na kuundwa kwa Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi Zanzibar (ZAECA) ambayo inaendelea na kazi zake vyema.

Dk. Shein pia, alimueleza Kamishna huyo mpya wa Polisi Zanzibar, haja ya kuwepo kwa umakini kwa askari wa usalama barabarani katika kuhakikisha sheria za usalama barabarani zinafuatwa.

Alieleza kuwa kumekuwa na matukio mengi ya ajali za barabara ambazo hupelekea vifo na nyengine husababisha ulemavu wa kudumu kwa wananchi hali ambayo inatokana na baadhi ya madereva kutofuata sheria za usalama barabarani.

Akisisitiza suala hilo, Dk. Shein alieleza kuwa hata yeye mwenyewe kwa upande wake amekwua akisisitiza suala la kufuata sheria za usalama barabarani katika hotuba zake, zikiwemo zile za  Idd El Fitri na Idd El Hajj ambazo huwataka wananchi wakiwemo madereva wa gari kufuata sheria za usalama barabarani katika vipindi vya sikukuu na katika siku za kawaida.

Alieleza kuwa lakini, bado kuna ugumu wa baadhi ya madereva kutofuata sheria hizo, sambamba na baadhi ya askari wa usalama barabarani kutokuwa na kasi ya kuhakikisha sheria hizo zinafuatwa.

Hivyo, alieleza haja ya kuwafundisha wananchi juu ya sheria za barabarani, licha ya juhudi zinazochukuliwa na baadhi ya viongozi wa Jeshi la Polisi kutoa elimu kupitia vyombo vya habari lakini ipo haja ya kuongeza kasi kwani hali hairidhishi katika jambo hilo sambamba na kueleza haja ya kuwepo mashirikiano na Idara husika ya leseni katika kuhakikisha utoaji wa leseni unafanywa kwa taraibu na sheria zilizopo.

Nae Kamishna wa Polisi Zanzibar Mohamed Haji Hassan alimueleza Rais Dk. Shein azma yake ya kuhakikisha anatoa ushirikiano mkubwa na Jeshi la Polisi linaendelea kufanya kazi zake vyema, ili kuendeleza usalama kwa wananchi, mali zao pamoja na wageni wanaokuja kuitembelea Zanzibar.

Sambamba na hayo, Kamishna huyo alitumia fursa hiyo kumueleza Rais Dk. Shein uzoefu wake wa kazi katika Jeshi hilo pamoja na mafunzo yake aliyoyapata ndani na nje ya Tanzania.

Mnamo Februari 10, 2018 Rais, Dk. John Pombe Magufuli alimpandisha Cheo Kamishna Mohamed Haji Hassan kutoka Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) na kuwa Kamishna wa Polisi (CP) na kisha kumteua kuwa Kamishna wa Polisi Zanzibar.

Kufuatia uteuzi wake huo, mnamo Februari 12 mwaka huu, kwa niaba ya Rais Dk. Magufuli Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Simon Nyakoro Sirro alimuapisha Kamishna Hassan kuwa Kamishna wa Polisi Zanzibar na kushika nafasi iliyowachwa wazi na Kamishna wa Polisi ndugu Hamdani Omar Makame ambaye amestaafu.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.