Habari za Punde

Rais Dk Shein akutana na kuzungumza na Mabalozi wapya waliofika kujitambulisha Ikulu

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akisalimiana na Balozi wa Tanzania Nchini Sweden Mhe.Wilbroad Peter Slaa alipofika Ikulu Mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha pia na kumuaga Rais baada ya kuteuliwa kushika nafasi hiyo na Rais waJamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.[Picha na Ikulu.]
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akisalimiana na Balozi wa Tanzania Nchini Nigeria  Mhe.Muhidin Ally Mboweto alipofika Ikulu Mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha pamoja na  kumuaga Rais baada ya kuteuliwa kushika nafasi hiyo na Rais waJamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.[Picha na Ikulu.]
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na  Balozi wa Tanzania Nchini Sweden Mhe.Wilbroad Peter Slaa (katikati) na Balozi wa Tanzania Nchini Nigeria  Mhe.Muhidin Ally Mboweto  walipofika Ikulu Mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha na kumuaga Rais baada ya kuteuliwa kushika nafasi hizo na Rais waJamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.[Picha na Ikulu.]
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akimsikiliza  Balozi wa Tanzania Nchini Sweden Mhe.Wilbroad Peter Slaa (katikati) wakati wa mazungumzo yao na Balozi wa Tanzania Nchini Nigeria  Mhe.Muhidin Ally Mboweto (kushoto)  walipofika Ikulu Mjini Zanzibar   kwa ajili ya kujitambulisha na kumuaga Rais baada ya kuteuliwa kushika nafasi hizo na Rais waJamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.[Picha na Ikulu.]


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akifuatana na Balozi wa Tanzania Nchini Sweden Mhe.Wilbroad Peter Slaa baada ya mazungumzo yao na Balozi wa Tanzania Nchini Nigeria  Mhe.Muhidin Ally Mboweto(hayupo pichani)   walipofika Ikulu Mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha na kumuaga Rais baada ya kuteuliwa  na  Rais waJamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kushika nafasi hizo .[Picha na Ikulu.]


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Zanzibar                                                             26.2.2018
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja kwa Mabalozi wanaokwenda kuiwakilisha Tanzania nchini Sweden na Nigeria kutilia mkazo Sera ya Diplomasia ya Uchumi ili Tanzania iweze kutekeleza malengo iliyojiwekea katika kuimarisha uchumi wake.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar, wakati alipofanya mazungumzo na Mabalozi wanaokwenda kuiwakilisha Tanzania katika nchi hizo, waliofika Ikulu kumuaga Rais pamoja na kujitambulisha na hatimae kufanya nao mazungumzo.

Mabalozi hao ni Balozi Wilbroad Peter Slaa,  Balozi wa Tanzania nchini Sweden na Balozi Muhidin Ally Mboweto, Balozi wa Tanzania nchini Nigeria.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa shabaha kuu ya Serikali zote mbili , Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuimarisha sekta za kiuchumi na huduma za jamii ikiwemo sekta ya  viwanda,utalii, uvuvi pamoja na elimu na utamaduni.

Dk. Shein alieleza kuwa Serikali  zote mbili zimedhamiria kutekeleza Diplomasia ya uchumi katika kuhamasisha uwekezaji hasa katika sekta ya viwanda kwani ndio kiu ya uchumi wa Tanzania hivi sasa.

Akizungumzia kwa upande wa Zanzibar, Dk. Shein alisema kuwa licha ya Zanzibar kuwa ni visiwa ambavyo vimezungukwa na bahari sambamba na kuwa na azma ya kutekeleza uchumi wa bahari lakini bado hakuna viwanda vya samaki au viwanda vyenye kutumia rasilimali za baharini.

Alieleza kuwa eneo la bahari la Zanzibar ni maarufu sana kwa samaki aina ya jodari ambaye ni samaki anaependwa duniani lakini wamekuwa hawavuliwi ipasavyo na badala yake hutokea meli kubwa za kigeni za uvuvi ambazo huja kuwavua kwa kuwaiba na kutolea mfano kuwa hivi karibuni kuna meli zimekamatwa zikifanya uhalifu huo.

Dk. Shein alieleza kuwa kuwepo kwa Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo makamo makuu yake yapo hapa Zanzibar maeneo ya Fumba, ni jitihada maalum za Serikali hiyo katika kuhakikisha Tanzania ikiwemo Zanzibar inaimarisha sekta ya uvuvi na inapata mafanikio kutoka katika sekta hiyo.

Hivyo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwaeleza Mabalozi hao kuwa Zanzibar inawakaribisha wawekezaji kutoka Sweden na Nigeria kuja kuwekeza katika viwanda vya samaki.

Aidha, Dk. Shein alieleza haja ya Mabalozi hao kuitangaza Zanzibar na Tanzania nzima kiutalii ambapo kwa upande wa Zanzibar sekta hiyo imekuwa ni muhimu kutokana na kuchangia asilimia 27 ya pato la Taifa na asilimia 80 ya fedha za kigeni.

Dk. Shein alieleza kuwa lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ifikapo mwaka 2020 ni kupokea watalii zaidi ya laki tano kutokana na mikakati iliyopo hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar inavivutio vingi vya kitalii vikiwemo viungo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwatakia heri na fanaka Mabalozi hao katika utendaji wao  wa kazi kwenye Balozi hizo na kuwaahidi kuwa ataendelea kutoa ushirikiano wake kwa Mabalozi hao kwa lengo la kutekeleza vyema dhamana zao hizo.

Pia, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendeleza uhusiano na ushirikiano na nchi hizo katika kuimarisha sekta ya elimu hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar ina ushirikiano mzuri na Nigeria ambayo imekuwa ikileta walimu wa mafunzo ya Sayansi kwa awamu huku akieleza uhusiano wa kihistoria na Sweden katika kuisaidia Zanzibar kwenye sekta ya elimu.

Nao Mabalozi hao walimthibitishia  Dk. Shein kuwa wamepokea maelekezo na miongozo yote aliyowapa na kumuahidi kuyafanyia kazi hasa kwa maeneo maaluma ya Zanzibar na yale ya Tanzania Bara sambamba na kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na nchi hizo wanazoenda kufanya kazi.

Akitoa maelezo kwa upande wake Balozi Wilbroad Peter Slaa,  Balozi wa Tanzania nchini Sweden alimueleza Dk. Shein kuwa watafanya jitihada kwa nguvu zao zote katika kuhakikisha kuwa lengo la kuimarika kwa Tanzania kiuchumi linafanikiwa.

Aliongeza kuwa kwa vile Zanzibar imezungukwa na Bahari, hivyo suala la kuimarishwa kwa sekta ya uvuvi atalipa kupaumbele hasa ikizingatiwa kuwa nchi anazokwenda kufanya kazi zikiwemo Sweden, Denmark, Norway, Finland zimepiga hatua kubwa katika sekta hiyo .



Nae Balozi Muhidin Ally Mboweto, Balozi wa Tanzania nchini Nigeria alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa atafanya juhudi za makusudi katika kuhakikisha mashirikiano katika sekta ya elimu kati ya Nigeria na Tanzania yanaimarika ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya walimu wa Sayansi kutoka nchini humo  kuja Zanzibar pamoja na kuanzisha mfumo huo kwa upande wa Tanzania Bara ambako kuna changamoto kama hiyo.

Aidha, alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa atachukua juhudi za makusudi katika kuhakikisha anawavutia wawekezaji kuja kuekeza katika sekta mbali mbali za kiuchumi na kijamii ikiwemo viwanda, uvuvi na sekta nyenginezo.

Mabalozi hao walimuhakikishia Dk. Shein kuwa katika wadhifa wao huo juhudi za makusudi watazichukua kwa mashirikiano ya pamoja katika kuhakikisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya nchi hizo na Tanzania unaimarishwa zaidi ikiwa ni pamoja na kuitangaza Tanzania ikiwemo Zanzibar kiutalii kwa azma ya kuimarisha maslahi ya kiuchumi kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.