Habari za Punde

Rais wa Zanzibar la Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Auagiza Uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Kuanda Mkutano Maalum na Walimu wa Skuli Saba za Sekondari Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akiutubia wakati akiufungua Mkutano Mkuu wa Sita wa Chama cha Walimu Zanzibar katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilushi Kikwajuni Zanzibar leo 10-2-2018.   

RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa bila ya kuwa na walimu wenye dhamira ya dhati ya kufundisha katika ngazi zote za elimu itakuwa ni ngumu kupata maendeleo ya kweli yanayokwenda sambamba na mabadiliko na mwelekeo wa karne ya 21.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Baraza la zamani la Wawakilishi, Kikwajuni mjini Unguja katika hotuba yake ya ufunguzi wa Mkutano wa Sita wa Chama cha Walimu Zanzibar (ZATU).

Katika hotuba hiyo, Dk. Shein alieleza  kuwa hakuna mtaalamu duniani ambae hakuandliwa na mwalimu kwa njia rasmi au isiyo rasmi, na kuwaeleza walimu hao jukumu kubwa walionalo katika kuitoa Zanzibar hapa ilipo na kuipeleka kule ambako wananchi wanataka kwenda.

Dk. Shein alieleza kuwa mataifa mengi yaliyopiga hatua za haraka katika karne ya 21, yaliweka mkazo kwa kuwekeza katika elimu kwani fedha pekee yake haiwezeshi Taifa lolote lile kupata wataalamu wazalendo inaowataka.

“Wataalamu wazalendo wahitaji kutayarishwa na walimu wazalendo, kuanzia ngazi ya msingi hadi Chuo Kikuu”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa juhudi zinazofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya  Zanzibar zimepelekea kuanzishwaa vyuo vikuu ambavyo tayari vipo vitatu vinavyoendeshwa na wataalamu wazalendo ambapo kwa mwaka huu wa masomo uliomaliza, vyuo hivyo vimeweza kutoa jumla ya wahitimu 4,287.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliipongeza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali na walimu wote kwa matokeo mazuri yaliopatikana kwa niaba yake na Serikali kwa jumla kutokana na ufaulu wa wanafunzi wote waliofanya mitihani ya Taifa wakiwemo wa darasa la nne, darasa la sita, kidato cha Pili, Kidato cha Nne na Kidato cha Sita.

Hata hivyo, kutokana na ufaulu wa kidato cha nne kushuka, Dk. Shein aliuagiza uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali uandae mkutano maalum na walimu wa skuli saba za sekondari za Zanzibar zilizomo katika orodha ya skuli 10 zilizofanya vibaya kwa Tanzania nzima mwaka 2017.

Alieleza kuwa katika mkutano huo wajadili sababu zilizopelekea skuli hizo zifanye vibaya sambamba na kuandaa mkakati maalum ili kuondokana na tatizo hilo na kumtaka Waziri wa Wizara hiyo kuongoza mkutano huo ambapo alisikitishwa na hali hiyo na kueleza kuwa wanafunzi wa Zanzibar wanaweza kufanya vizuri iwapo watapata maelekezo mazuri kutoka kwa walimu wao kwani Zanzibar ina historia nzuri kielemu.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali imekuwa ikiongeza bajeti ya elimu kwa kila mwaka, ili sekta hiyo izidi kuimarika ambapo TZS Bilioni 120.726 ziliingiziwa Wizara hiyo mnamo mwaka 2015/2016,TZS Bilioni 133.501 mwaka 2016/2017 na TZS Bilioni 197.290 mwaka 2017/2018 na kuahidi kuongeza zaidi kwa mwaka 2018/2019.

Alieleza kuwa wapo baadhi ya walimu wanaharibu fani ya uwalimu ambayo ni fani yenye heshima kubwa kutokana na tamaa zao na wale ambao wanaingiza siasa katika fani hiyo huku akieleza kukerwa na tabia ya baadhi ya walimu kufanya biashara ya urojo na biskuti skuli huku wakisingizia kushuka kwa elimu wakati wao ndio chanzo.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa katika kuongeza ufanisi wa maendeleo ya skuli suala la ukaguzi wa skuli na walimu ni muhimu lakini kwa bahati mbaya suala hilo limekuwa halifanywi vizuri.

Pia, Dk. Shein alieleza kuwa wakati alipofanya ziara za Mikoa mnamo mwezi Agosti 2017 aliagiza uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, ushirikiane na viongozi wa Mikoa na Wilaya katika kuzifanyia kazi changamoto ya kuwepo kwa utoro uliokithiri wa walimu na wanafunzi lakini hadi leo hajapelekewataarifa yoyote.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwaeleza walimu hao kuwa katika ombi lao la kuwapatia posho walimu wakuu la asilimia 50 Serikali haiwezi kufanya hivyo hadi pale walimu hao nao kwa upande wao wajue wajibu wao ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanafunzi wanafanya vizuri katika masomo yao.

Pia, Rais Dk. Shein aliitaka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar kuhakikisha inashirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango inawalipa walimu malimbikizo yao yote wanayodai ili mwakani kwenye mkutano kama huo wasijekuleta madai hayo na badala yake waelezee mafanikio na mambo mengineyo kuhusu chama hicho cha walimu Zanzibar na sio kudai fedha zao za malimbikizo.

Kuhusu Muundo wa Utumishi wa Wizara ya Elimu, Dk. Shein aliitaka wizara hiyo kwa kushirikiana na Wizara ya Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora kuwarudishia walimu na kuhakikisha wanalipwa haki zao zote pamoja na kuziangalia Wizara nyenginezo zote kwani tayari ameshatoa agizo ya kufanyiwa kazi suala hilo. 

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliitaka Wizara ya Elimu kuhakikisha wanakutana na uongozi na wajumbe wa chama hicho angalau mara mbili kwa mwaka na katika mkutano huo watumie fursa hiyo kujadili na kupokea maoni kutoka kwa chama hicho yenye mustakbali wa kuimarisha sekta ya elimu nchini.

Nae Kaimu Waziri wa Wizara hiyo, Mahamoud Thabit Kombo, ambaye pia, ni Waziri wa Afya alieleza kuwa miongoni mwa sababu zinazopelekea kuwepo kwa changamoto katika elimu ikiwemo ya wingi wa wanafunzi madarasani ni kuongezeka kwa idadi ya watu Zanzibar hasa ikizingatiwa kuwa katika nchi za Afrika, idadi ya watu Zanzibar imekuwa ikiongezeka kwa asilimia kubwa.

Nae Rais wa Chama hicho Mwalimu Seif Mohamed alitoa pongezi zake kwa Rais Dk. Shein kutokana na juhudi za makusudi anazozichukua katika kuangalia maslahi ya wafanyakazi wa Serikali wakiwemo walimu.

Mapema Katibu Mkuu wa Chama hicho cha Walimu Zanzibar Mussa Omar Tafurwa alisoma risala ya Walimu na kueleza mafanikio iliyoyapata Jumuiya hiyo sambamba na changamoto zilizopo ikiwa ni pamoja na kueleza haja ya walimu wakuu kupewa posho la asilimia 50 ya mishahara yao, madai yao na malimbikizo wanayodai pamoja na mambo mengineyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.