Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akisalimiana na Balozi wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Sahabi Isa Gada alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kwa ajili ya kujitambulisha kwa Rais
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akimsikiliza mgeni wake Balozi wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Sahabi Isa Gada wakati wa mazungumzo yao alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kwa ajili ya kujitambulisha.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na Balozi wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Sahabi Isa Gada alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kwa ajili ya kujitambulisha
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na mgeni wake Balozi wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Sahabi Isa Gada (wapili kulia) wakati wa mazungumzo yao alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kwa ajili ya kujitambulisha akiwa na ujumbe aliofuatana nao
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akifuatana na mgeni wake Balozi wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Sahabi Isa Gada baada ya mazungumzo yao alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kwa ajili ya kujitambulisha.[Picha na Ikulu.]
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein ameipongeza Serikali ya Nigeria kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar
katika kuimarisha sekta ya elimu na kueleza haja ya kuendelea na hatua hiyo kwa
sekta nyengine ili kuzidisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati
ya Zanzibar na nchi hiyo.
Akizungumza na Balozi
mpya wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Sahabi Isa Gada Ikulu
mjini Zanzibar, Dk. Shein alieleza kuwa
uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Nigeria
na Zanzibar una historia kubwa kwani nchi hiyo ni miongoni mwa nchi za mwanzo
zilizoiunga mkono Zanzibar katika sekta ya elimu mara tu baada ya Mapinduzi matukufu
ya mwaka 1964.
Katika Mazungumzo hayo,
Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa hatua ya ujio wa walimu wa Sayansi kutoka nchini Nigeria kwa ajili ya kuja
kusomesha skuli za Sekondari za Zanzibar ni ushahidi mzuri wa kuonesha
kuimarika kwa uhusiano na ushirikiano kati ya pande mbili hizo
Alieleza kuwa katika juhudi
za kuiunga mkono Zanzibar kwenye sekta ya elimu ujio wa walimu 16 hapo kesho
ambao wanakuja kwa makundi kutasaidia katika kuimarisha sekta ya elimu hapa
nchini.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kutoa pongezi kwa Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari kwa kuendelea
kuiunga mkono Zanzibar katika sekta ya elimu na kueleza kuwa juhudi hizo ni
muendelezo wa uhusiano ulioanzishwa na muasisi wa Taifa la Tanzania Hayati
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Benjamin Nnamdi Azikiwe Rais wa kwanza wa
Nigeria.
Aidha, Dk. Shein
alimueleza Balozi Gada haja ya kuendeleza mahusiano na ushirikiano kupitia vyuo
vikuu vya Nigeria na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) hatua ambayo
itasaidia kubadilishana uzoefu na utaalamu katika ngazi ya vyuo vikuu.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Zanzibar ni visiwa ambavyo vimezungukwa
na bahari sambamba na kuwa na rasilimali za bahari wakiwemo samaki wanaopendwa
duniani aina ya jodari, hivyo inawakaribisha wawekezaji wa Nigeria kuja kuekeza
Zanzibar katika sekta ya viwanda vya samaki.
Alisisitiza kuwa kwa
vile tayari waekezaji wa nchi hiyo akiwemo muekezaji aliyeekeza kiwanda cha
saruji katika maeneo ya Kusini mwa Tanzania hivyo, ni vyema Ubalozi huo
ukaitangaza Zanzibar kwa waekezaji wa nchi hiyo ili waje kuekeza katika sekta nyengine vikiwemo viwanda vya uvuvi.
Aliongeza kuwa tayari
kuundwa kwa Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
ambayo makamo makuu yake yapo hapa Zanzibar maeneo ya Fumba, ni jitihada za
makusudi za Tanzania katika kuhakikisha uvuvi wa bahari kuu unaimarishwa.
Dk. Shein pia,
alisisitiza haja ya mashirikiano katika sekta ya sanaa na utamaduni kati ya
Zanzibar na Nigeria hasa ikizingatiwa kuwa tayari nchi hiyo imepiga hatua
katika sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kujiimarisha katika masuala ya filamu na
maigizo kupitia kiwanda cha uigizaji filamu cha nchi hiyo Nollywood ili Zanzibar
nayo iweze kuwa na kiwanda kama hicho.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza haja ya kuwepo mashirikaino kwa wananchi na wa pande mbili
hizo kutembeleana kwa lengo la kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo sambamba
na kuiimarisha sekta ya utalii kati ya Zanzibar na Nigeria huku akipongeza
hatua za kuendelea kuimarika kwa uchumi wa Nigeria.
Nae Balozi mpya wa
Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Sahabi Isa Gada alimueleza
Rais Dk. Shein kuwa uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya pande mbili hizo si
mpya bali ni wa muda mrefu hivyo aliahidi kuwa nchi yake itauimarisha.
Dk. Gada alimueleza
Rais Dk. Shein kuwa walimu 16 wa Sekondari wa Sayansi wanatarajiwa kuwasili
nchini hapo kesho wakitoa Nigeria ikiwa ni hatua moja wapo ya kuendeleza uhusiano
na ushirikiano uliopo kati ya Zanzibar na nchi hiyo.
Aidha, Balozi huyo
alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa juhudi za makusudi zitaendelea kuchukuliwa
na Ubalozi wake katika kuhakikisha idadi hiyo ya walimu inaongezeka ili kutoa
nafasi nzuri ya kuimarika kwa sekta ya elimu hapa Zanzibar.
Sambamba na hayo,
Balozi Gada alimueleza Rais Dk. Shein kuwa suala zima la kuwakarisha waekezaji
kuja kuekeza Zanzibar atalifanyia kazi kwa kutambua kuwa wapo waekezaji wengi
katika sekta hiyo nchini mwake hasa ikizingatiwa kuwa Nigeria nayo ina uzoefu
katika sekta ya uvuvi.
Katika ujio wa walimu
wa Sayansi kwa ajili kusomesha Skuli za Sekondari hapa Zanzibar kutoka nchini
Nigeria, idadi yao mara hii ni walimu 50 na wote ni walimu wa masomo ya Fizikia
na Hesabati ambapo tayari wameshafika walimu 8 na kesho wanatarajiwa kuwasili
nchini walimu 16 na watakaobaki ambao jumla yao ni 26 watakuja hapo baadae, walimu hao
hufundisha kwa muda wa miaka miwili miwili.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment