Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akisisitiza jambo wakati wa hafla ya maadhimisho ya Siku ya Sheria Zanzibar wakati akihutubia katika ukumbi wa zamani wa baraza la wawakilishi kikwajuni Zanzibar leo.12-2-2018.

RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa utawala wa sheria ndio dira katika utoaji haki na ndio utakaoiwezesha Zanzibar kudumisha amani na utulivu iliyopo ambayo ndio msingi wa maendeleo katika sekta zote za kiuchumi na kijamii.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Baraza la zamani la Wawakilishi, Kikwajuni mjini Unguja katika  hafla ya kuadhimisha Siku ya Sheria Zanzibar.

Alieleza kuwa utawala wa sheria ndio utakaoiwezesha Zanzibar kutekeleza mipango ya kuimarisha viwanda, kukuza sekta ya utalii, kuvutia wawekezaji, kuwa na mfumo mzuri wa biashara, kuendeleza kilimo, uvuvi na ufugaji wa kisasa pamoja na uhifadhi wa mazingira.

Aliongeza kuwa inahitajika kuwa na sheria madhubuti katika ukusanyaji wa mapato na kurahisisha ulipaji kodi, kuwa na mfumo imara wa utoaji huduma za afya, elimu pamoja na maji safi na salama.

Dk. Shein alisema kuwa Mahkama kwa kushirikiana na vyombo vyengine vya sheria ina jukumu kubwa la kuhakikisha utendaji na uendeshaji wa shughuli zao, unapelekea kuimarikamkwa hali ya amani na utulivu, hasa kwa kutoa haki kwa kuzingatia misingi ya usawa na kwa mujibu wa sheria zilizopo.

“Utawala wa sheria ulio madhubuti, ni ule ambao umeelekeza nguvu kubwa zaidi katika kukinga na kuzuwia uvunjaji wa sheria usitokezee, badala ya kujipanga katika kushughulikia kesi na mashauri yanayojitokeza na kuwasilishwa Mahkamani”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk.  Shein alieleza matumaini yake kuwa Mahkama itajitahidi kuchukua muda ulioelezwa katika sheria au chini ya hapo ili kuweza kuwavutia wafanyabiashara kuleta mashauri na kumaliza mashauri yao mapema na kuweza kufanya shughuli za uzalishaji.

Alieleza Mahkama kuwa inatakiwa kushughulikia migogoro ya ardhi, pia, ni vyema kwa Mahakimu wa Mahkama za Ardhi na Mahkama Kuu kutoa kipaumbele kwa migogoro ya ardhi iliyo mbele yao inayohusiana na majengo ya biashara na uwekezaji, ili isichukue muda mrefu jambo ambalo linaweza kuwakatisha tamaa wawekezaji hao.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuvutiwa kwake na kauli mbiu na maudhui ya maadhimisho ya mwaka huu wa sheria inayosema “ Imarisha Utawala wa Sheria kwa Kukuza Uchumi wa Nchi” sambamba na kueleza kuvutika kwake na juhudi za Mahkama.

Alieleza kuwa maudhui hayo, vile vile ynakwenda sambamba na dhamira iliyoelezwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015-2020, kwenye Ibara ya 144, kuhusiana na suala zima la kuimarisha Utawala Bora na Demokrasia nchini.

Pia, alieleza kuwa Mahkama haina budi kushughulikia migogoro ya ajira kwa haraka kuruhusu wafanyakazi waendelee na uzalishaji, na kutoa wito kwa watendaji wa kitengo hicho na Mahkama kutoa kipaumbele kwenye migogoro hiyo.

Alisisitiza matumizi ya TEHAMA ni muhimu sana ili kuongeza ufanisi na tija katika mfumo wa utatuzi wa migogoro na hakuna haja kwamba hata kwa jambo dogo wananchi wafike Mahkamani bali mambo mengine yanaweza kufanyika kwenye mtandao.

Kwa maelezo ya Dk. Shein ni kuwa Serikali itafanya kila iwezalo kwa lengo la kuziwezesha Mahkama ili iweze kufanya shughuli zao ipasavyo za kusikiliza na kuamua mashauri kwa wakati na kuiimarisha miundombinu ya Mahkama katika kuyashughulikia matatizo ya wananchi.

Dk. Shein, pia, alirejea kauli yake aliyoitoa hivi karibuni juu ya ujenzi wa Mahkama Kuu huko Tunguu ambayo kwa maelezo yake panapomajaaliwa amelenga kuifungua yeye mwenyewe mnamo sherehe  za Mapinduzi mnamo mwaka 2020 na kusisitiza kuwa “lazima tuwe na jengo la kisasa la Mahkama linaloendana na hadhi ya Serikali hii”.

Nae Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuhudhuria katika sherehe hizo kwa mwaka wa saba hivi sasa huku akisema kuwa muhimili wa Mahkama umekuwa ukifanya kazi vyema kwa lengo la kuimarisha Muungano.

Alisisitiza suala la amani na umoja kuwa ni nguzo muhimu hapa nchini na ukanda mzima pamoja na dunia kwa jumla huku akitumia fursa hiyo kueleza mafanikio yaliopatikana na Mahkama pamoja na mikakati iliyowekwa katika kuhakikisha Mahkama inaimarika hapa nchini.

Wananchi wanastahili kupata nakla  zao za kesi mapema, Mahkama imedhamiria kuwa wadau wote wanapata nakla za hukumu ndani ya siku 30, ambapo mwaka jana wamepata nakla zao kwa wakati hatua ambayo imewasaidia kupelekea nakla zao katika Mahkama ya Rufaa kwa wakati  huku akieleza lengo lao kuwa hadi kufikia Disemba 2018 suala la kuchelewa hukumu iwe historia.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Haji Ussi Gavu kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora alisisitiza haja ya kuhakikisha haki zote za wananchi zinapatikana na kila mmoja katika taasisi na vyombo husika ili kila mmoja atimize wajibu wake katika kutekeleza hilo.

Mapema Rais wa Chama cha Mawakili Zanzibar Omar Said Shaaban alisema kuwa zipo baadhi ya Taasisi au wakuu wa Taasisi ambao kwao wao kufuata Sheria zilizowekwa wamekuwa wagumu na matokeo yake wanazorotesha ukuaji wa uchumi.

Alisema kuwa wapo wengine hawaoni tabu hata kuagiza kufutwa kwa vibali vya uwekezaji na kupendekeza Mwekezaji aondoshwe nchini bila ya kufata utaratibu uliowekwa na sheria au kufanya mashauriano na mamlaka nyengine zinahusika za kiuchumi kama vile za kodi au uwekezaji.

Alisisitiza kuwa Zanzibar inaongozwa na Katiba lakini pia, kupitia Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeridhia mikataba mbali mbali ya Kimataifa yenye kulinda Wawekezaji na Uwekezaji. Si vyema jitihada za Serikali katika kuwaalika wawekezaji kuja nchini zikatiwa doa na watu wachache ambao hawajui athari za matendo yao.

Katika hafla hiyo, burdai mbali mbali zilitumbuizwa ikiwa ni pamoja na tenzi pamoja na mchezo wa kuigiza kutoka katika Kundi la Black Root chini ya Msanii mahiri Makombora.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.