Habari za Punde

Zanzibar Kufanyika Mkutano wa Kimataifa wa Anga Mwezi Ujao. Kushirikisha Wadau Mbalimbali wa Mashirika ya Usafiri wa Anga Duniani.


Na. Abdi Shamna Zanzibar.
MKUTANO wa Wadau wa Usafiri wa Anga Afrika, unatarajiwa kufanyika hapa Zanzibar  April 8, mwaka huu, ambapo pamoja na mambo mengine utajadili suala la uimarishaji wa biashara ya safari za ndege pamoja na Usalama wa safari za Anga.

Mkutano huo wa siku mbili utahusisha washiriki zaidi ya 400, ikiwemo watengenezaji wa ndege, watoa huduma za ndege (booking, vyakula,mifumo ya viwanja vya ndege) na wamiliki wa mashirika ya ndege.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mashirika ya Ndege Afrika (AFRAA), Abderahmane Berthe, alisema watendaji kutoka  mashirika ya Ndege ya Afrika, yapatayo 40 watashiriki mkutano huo.

Alisema  AFRAA imefikia uamuzi wa kuiteuwa Zanzibar kuwa mwenyeji wa mkutano huo, kwa kigezo kuwa ni kitovu cha utalii, hivyo hatua hiyo itatowa fursa ya kuendeleza sekta hiyo.

Alisema suala la biashara ya safari za Anga litachukuwa nafasi kubwa, ili kuona sekta hiyo inaimarika, ikiwemo wadau (watengenezaji wa ndege) kupata nafsi ya kubainisha ubora wa ndege wanazotengeneza ili kuvutia mashirika kwa ajili ya ununuzi.

Aidha, alisema kwa kuzingatia umuhimu wa sekta ya utalii ya kuhitaji usafiri wa uhakika, suala la usalama wa safari za ndege nalo litapewa kipaumbele.

“Zanzibar ni moja ya nchi za utalii, iwapo suala la usalama wa safari za anga halitapewa kipaumbele, ni dhahiri kuwa watalii hawatakuwa na uhakika wa safari zao, watalii wengi wanaokuja hapa  huinga nchini kupitia njia za anga”, alisema.

Vile vile alisema, mkutano huo utatowa fursa kwa mashirika madogo ya ndege kukutana na wadau wengine na kuongeza ushirikiano katika nyanja hiyo na kuimarisha mashirika yao.

Nae, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ndege Tanzania (Air Tanzania) Ladislaus Matindi, alisema AFRAA imeamuwa mkutano huo kufanyika hapa Zanzibar, ikiwa ni moja ya  hatua ya kuona ‘Air Tanzania’ inaimarika na kurejea katika hadhi yake.

Alisema katika kuhakikisha Shirika hilo linajiimarisha, limeandaa miakati inayolenga liweze kumiliki ndege 12 za aina tofauti hadi ifikapo mwaka 2022.

“Kwa kuwa mkutano huu utawashirikisha wadau mbali  mbali, pia tutapata fursa ya kuwasikiliza watengenezaji wa ndege, hii ni fursa ya kuangalia maeneo mengine zaidi, wapi tunaweza kupata ndege bora  zaidi, tuna mikakati ya kuwa ndeeg nyingi zaidi”, alisema.

Alisema kwa sasa Shirika hilo linaendelea na utaratibu wa kukamilisha ununuzi wa ndege nne aina Bombadier, pamoja na azma ya  kununua ndege moja aina ya Boieng.

Mapema, Naibu Waziri, Wizara ya Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar, Mohammed Ahmada, alisema  mkutano huo wa siku mbili, utasaidia sana kuitangaza Zanzibar kiutalii na kibiashara.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea na juhudi za kuimarisha miundombinu ya usafiri wa anga, ikiwemo kukmailisha  ujenzi wa Termina 11, ili kuweka mazingira bora ya ujio wa watalii na kufikia lengo la kupokea watalii 500,000 ifikapo 2020.

Alisema Serikali  kwa kushirikiana na AFRAA, Kamisheni ya Utalii Zanzibar na ATCL inaendelea na maandalizi ya mkutano huo unaotarajiwa kufana vyema.

Katika hatau nyengine, Katibu Mtendaji Kamisheni ya Utalii Zanzibar, Dk. Vuia Lilla, alisema ujio wa mkutano huo, utatowa fursa adhimu ya kibiashara kwa wadau wa utalii nchini, ikiwemo wamiliki wa hoteli,watembeza watalii, sambamba na wageni kupata fursa ya kutembelea maeneo tofauti ya kihistoria na kuona vivutio vya talii.
  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.