Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kushoto)akimuapisha Jaji Mkuu Mstaafu wa Zanzibar Mhe.Hamid Mahmoud Hamid kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) katika hafla iliyofanyika leo katika Ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar,ambapo Viongozi mbali mbali walihudhuria.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein leo amemuapisha Jaji
Mkuu Mstaafu wa Zanzibar Hamid Mahmoud Hamid kuwa Mwenyekiti wa Tume ya
Uchaguzi Zanzibar (ZEC).
Wakati huo huo, Rais
Dk. Shein amewaapisha Wajumbe wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), ambao
aliwateua hivi karibuni kushika nyazifa hizo ambapo Wajumbe walioapishwa ni
Mabruki Jabu Makame, Feteh Saad Mgeni, Makame Juma Pandu, Dk. Kombo Khamis
Hassan, Jaji Khamis Ramadhan Abdalla na Jokha Khamis Makame.
Hafla hiyo, ilifanyika
Ikulu mjini Zanzibar na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, akiwemo Makamu wa
Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali
Maulid, Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar
Othman Makungu, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Said Hassan Said, Mawaziri pamoja
na Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya
Mzee.
Viongozi wengine
waliohudhuria ni Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabih, Kadhi Mkuu wa
Zanzibar Sheikh Khamis Haji,Wakuu wa Vikosi vya SMZ, Meya wa Manispaa ya Mji wa
Zanzibar Khatib Abrahman Khatib, Washauri wa Rais wa Zanzibar, viongozi wa
vyama vya siasa pamoja na wanafamilia wa viongozi walioapishwa.
Mara baada ya
kuapishwa viongozi hao wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) walieleza jinsi
walivyoupokea uteuzi huo na kuahidi kutekeleza majukumu yao kwa kufuata Katiba,
Sheria na Kanuni za Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) na kuwaomba Wazanzibari wote
kutoa mashirikiano yao kwa Tume hiyo ili kuweza kufanya kazi zake kwa ufansi sambamba
na kuendelea kudumisha amani na utulivu nchini.
Nae Mwenyekiti wa Tume
ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Hamid Mahmoud Hamid aliahidi kutumia uzoefu alikuwa
nao katika masuala ya uchaguzi kwa muda wa miaka saba akiwa Makamo Mwenyekiti
wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) katika kuhakikisha anatekeleza jukumu hilo
la kuongoza Tume kwa kufuata Katiba, Sheria na Kanuni zilizopo tena bila ya
upendeleo.
Nao viongozi wa vyama
vya siasa wamempongeza Rais Dk. Shein kwa kuheshimu Katiba ya Zanzibar na
kukidhi matakwa ya Katiba hiyo ya mwaka 1984 ambayo inataka miongoni mwa
Wajumbe wawili wa Tume ya Uchaguzi wawe ni kutoka vyama vya upinzani.
Dk. Shein kwa kutumia
uwezo aliopewa chini ya Kifungu 119 cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984
alifanya uteuzi wa Wajumbe wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar akiwemo Mwenyekiti wa
Tume hiyo Jaji Mstaafu Hamid Mahmoud Hamid.
Kuteuliwa na hatimae kuapishwa
kwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) pamoja na Wajumbe hao
kumekuja baada ya Wajumbe wa Tume iliyopita kumaliza muda wao chini ya Mwenyekiti wake Jecha Salim Jecha
ambao walifanya kazi kwa kipindi cha miaka mitano kilichoanzia tarehe 30 April,
2013 hadi tarehe 29 April, 2018 walipofikia ukomo.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address:
2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment