Habari za Punde

Balozi Seif afungua Kongamano la Maadili ya Mtanzania Ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakili Kikwajuni.

 Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi pamoja na Viongozi wa Jumuiya ya Wazazi wakikaribishwa na ngoma ya Utamaduni kwenye Viwanja vya Ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakil kabla ya Kuanza kwa Kongamano la Maadili ya Mtanzania.
 Balozi Seif akipokea Risala ya Jumuiya ya Wazazi iliyosomwa na Katibu wa Jumuiya hiyo Wil;aya ya Mjini Bibi Salama Abass  wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Maadili hapo Ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakili Kikwajuni.
 Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa Mjini Nd. Ali Othman Said akiwatambulisha Viongozi wa ngazi ya juu walioshiriki na kualikwa kwenye kongamano hilo.
 Baadhi ya Wajumbe wa Kongangamo la Maadili ya Mtanzania wakifuatilia Hotuba ya Mgeni rasmi Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Balozi Seif Ali Iddi hayupo pichani.
 Baadhi ya Wajumbe wa Kongangamo la Maadili ya Mtanzania wakifuatilia Houtaba ya Mgeni rasmi Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Balozi Seif Ali Iddi hayupo pichani.
 Balozi Seif akilifungua Kongamano la Maadili ya Mtanzania lililoandaliwa na Jumuiya ya Wazazi wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Mjini  na kufanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakili Kikwajuni.

 Balozi Seif  akiwa kati kati waliokaa vitini katika picha ya pamoja na Viongozi wa CCM na Jumuiya zake walioshiriki Kongamano la Maadili ya Mtanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakil.
Balozi Seif akiagana na baadhi ya Viongozi wa Kidini walioshiriki katika Kongamano la Maadili mara baada ya kulifungua Rasmi Kongamano hilo.
Picha na – OMPR – ZNZ.
Na Othman Khamios, OMPR
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif  Ali Iddi alisema matendo mengi maovu yanayofabnyika na kushuhudiwa ndani ya Jamii katika karne hii yanayochangiwa na mmong’onyoko wa Maadili yanaendselea kuwakosesha Amani ya Roho Wazazi walio wengi Nchini.
Alisema vitendo vya kutumia nguvu, utumiaji wa Dawa za kulevya, Ubakaji, Ulawiti, unyanyasaji wa Wanawake na Watoto vinaonyesha wazi hali isiyo shuwari kwa upande wa Maadili ya Taifa.
Akilifungua Kongamano hukusu Maadili ya Mtanzania kwa Wilaya ya Mjini lililofanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakili Balozi Seif Ali Iddi alisema Maadili ya Taifa taratibu yanaondoka na mahala pake panachukuliwa na matendo maovu.
Balozi Seif alisema hali iliyopo ya mmong’onyoko wa Maadili inayoendelea hivi sasa Jamii yenyewe inapaswa iangalie ilipokosea na kutafuta mbinu za haraka za kuirejesha ili kuepuka kuangamia.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alitahadharisha wazi kwamba Taifa linalokosa Maadili linakuwa sawa na mwili wa Mwanaadamu au kiumbe ye yote asiyekuwa na Roho.
Alieleza mara nyingi Taifa linalotokana na mkusanyiko wa Familia nyingi zilizopata malezi ya msingi hujenga Taifa madhubuti lililosheheni Maadili mema yanayokubalika Kitaifa.
Balozi Seif alielezea masikitiko yake  kutokana na wimbi kubwa la mtikisiko wa maadili uliojichomoza hivi karibuni katika ngazi ya Familia unaosababishwa na uvunjikaji wa ndoa na hatimae husambaratisha Familia husika.
Alisema wimbi hili limeonyesha wazi kutokana na wingi wa kesi za ndoa zinazoripotiwa katika Mahkama za Kadhi zikishuhudiwa ukosefu mkubwa wa maadili kutoka kwa Wanandoa.
Balozi Seif alitolea mfano wa kasoro hiyo ya uvunjiakji wa ndoa iliyopelekea kushuhudiwa kwa kesi za Talaka zipatazo 1,819 zilizotolewa hukumu katika kipindi cha Miaka Mitatu kuanzia Januari 2016 hadi Julai 2018 kwa Mahakama ya Mwanakwerekwe pekee.
Alisema takwimu hizo ni za Wilaya Moja tu ya Zanzibar wala hazihusishi Wilaya nyengine ikiachiliwa mbali talaka zinazoishia Mitaani kwa Viongozi wa Jamii bila ya kufikishwa kwa Makadhi.
Balozi Seif alionyesha wasi wasi wake kutokana na hali hiyo inayoashiria Talaka hapa Nchini zinaendelea kutolewa kama njugu na hicho ni kielelezo cha kushuka kwa Maadili katika Jamii.
Alieleza kwamba katika mazingira kama hayo akina mama wengi hushindwa kuwalea vizuri Watoto walioachiwa na wenza wao na hatimae Watoto hao huishia kupata malezi ya Mitaani.
“  Ukweli usiopingika kwamba  ukosefu wa malezi bora ya Watoto hupelekea kwa kiasi kikubwa uporomokaji wa Maadili hapa Nchini”. Alisema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.
Alisema Watoto hasa wale wanaokosa matunzo ya pamoja ya Wazazi wao wote wawili kwa sababu ya kutelekezwa na Baba zao huishia vijiweni na kulelewa na wanavijiwe ambao mara nyingi sio Watu wema.
Mazingira kama hayo kwa Watoto hao hatimae wanaanza kujitumbukiza  kwenye matumizi ya Dawa za kulevya, wizipamoja na  ubakaji matendo yasiyoleta tija kwa jamii na kuwa kero wakati wote.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliishukuru Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Mjini kwa uamuzi wake wa kufanya Kongamano hilo muhimu kwa uhai wa Taifa hili.
Akitoa Taarifa ya Kongamano hilo Katibu wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Mjini Bibi Salama Abass alisema Wilaya ya Mjini licha ya jitihada zuinazoendelea kuchukuliwa na Viongozi wa Serikali lakini bado inaendelea kukumbwa na matukio mbali mbali yanayosababishwa na mporomoko wa Maadili ya Jamii.
Bibi Salama alisema vitendo vinavyofanywa na watu hasa kundi kubwa la Vijana waliokosa Maadili  vimekuwa kero kubwa na kupelekea Jamii Mitaani kukumbwa na mtafakuru unaotokana na hofu ya matukio ya vitendo hivyo.
Katibu huyo  wa Wazazi Wilaya ya Mjini alieleza kwamba Kongamano hilo limeshirikisha Wajumbe 250 kutoka Matawi, Majimbona Wilaya ya Mjini pamoja na Umoja wa Vijana wa CCM na UWT Wilaya.
Akitoa salamu kwenye Kongamano hilo Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dr. Juma Abdullah Saadala  {MABODI} aliikumbusha  Uongozi wa Jumuiya ya Wazazi kuelewa kwamba wana jukumu na dhima kubwa ya kusimamia malezi bora ya Vijana ili Taifa liwe na wafuasi wenye maadili na nidhamu iliyotukuka.
Dr. Mabodi alitoa ahadi ya kuwa karibu na Jumuia zote katika kuhakikisha malezi yanarejea katika mahala pake akielewa kwamba na yeye pia mzazi wa kutoa mchango wake kwenye juhudi hizo za kurejesha malezi bora ya Vijana.
Kongamano hilo kuhusu Mmong’onyoko wa Maadili ya Mtanzania Wilaya ya Mjini pamoja na mambo mengine liomejadili Mada Nne ambazo ni pamoja na muelekeo wa mapambano dhidi ya mporomoko wa Maadili, Dawa za Kulevya pamoja na Ukimwi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.